Our Lady of Medjugorje Messages containing 'mmoja'

Total found: 26
Wanangu wapendwa! Kwa furaha moyoni nawapendeni nyote na kuwaalika kuukaribia moyo wangu usio na ndoa, ili moyo wangu uwapeleke karibu zaidi kwa Mwanangu, Yesu Kristo, ili naye awajalieni amani yake na upendo wake ambavyo ni chakula kwa kila mmoja wenu. Jifungueni, wanangu, kwa kusali, na jifungueni kwa upendo wangu. Mimi ndimi Mama yenu nisiyeweza kuwaachieni katika mtawanyiko na katika dhambi peke yenu. Enyi wana, mnaalikwa kuwa wanangu, wanangu wapendwa ili niweze kwakabidhi wote kwa Mwanangu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Leo pia nawaalikeni kusali. Uhusiano wenu na kusali uwe wa kila siku. Sala inasababisha miujiza ndani yenu na kwa njia yenu, na kwa hiyo, enyi wanangu, sala basi iwe ni furaha yenu. Hivyo uhusiano wenu na maisha utakuwa wa kina na wazi zaidi, pia mtaelewa kwamba maisha ni zawadi kwa kila mmoja wenu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Mimi, Mama yenu, nipo pamoja nanyi kwa ajili yenu, kwa mahitaji yenu na mafundisho yenu binafsi. Baba wa Mbinguni amewapa uhuru wa kuamua peke yenu na kujua peke yenu. Mimi nataka kuwasaidieni. Nataka kuwa Mama kwenu, mwalimu wa ukweli, ili kwa unyofu wa moyo wazi mjue usafi usio na mwisho, na mwanga utokao kwa hiyo ukweli ili kutawanya giza, yaani mwanga uletao tumaini. Mimi, wanangu, naelewa maumivu yenu na mateso yenu. Nani aweza kuwaelewa zaidi kuliko Mama mmoja! Lakini enyi wanangu? Mjue kuwa idadi ya wanaonielewa na kunifuata ni ndogo. Pia ni kubwa idadi ya waliopotea, hao ambao hawajajua ukweli ulio katika Mwanangu. Kwa hiyo, enyi mitume wangu, salini na tendeni kazi. Mbebe mwanga, msipoteze tumaini. Mimi nipo nanyi na hasa pamoja na wachungaji wenu. Nawapenda na kuwalinda kwa Moyo wa kimama, ili kusudi wao wanawaongozeni Paradisini alikowaahidia Mwanangu. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa! Ninyi hamjui neema ya namna gani mnayoishi katika wakati huu ambapo Yeye Aliye Juu awapeni ishara ili mjifungue na kutubu. Mwelekeeni Mungu na kusali; sala itawale katika mioyo yenu, familia na jamaa zenu ili Roho Mtakatifu awaongoze na kuhimiza kila siku mjifungue kufanya mapenzi ya Mungu na mpango wake kwa kila mmoja wenu. Mimi nipo pamoja nanyi, na nawaombeeni pamoja na malaika na watakatifu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Salini kwa nia zangu maana Shetani ataka kuangamiza mpango wangu nilio nao hapa na kuwaibia amani: Kwa hiyo, wanangu, salini, salini, salini ili Mungu aweze kutenda kazi kwa njia ya kila mmoja wenu. Mioyo yenu iwe wazi kupokea mapenzi ya Mungu. Mimi nawapendeni na kubariki kwa baraka ya kimama. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Salini katika kipindi hiki cha neema na ombeni maombezi ya Watakatifu wote ambao wapo tayari katika mwanga. Wao wawe mfano na kichocheo kwenu siku hata siku, katika njia ya uwongofu wenu. Wanangu, mfahamu ya kuwa maisha yenu ni mafupi na ya kupita upesi. Kwa hiyo tamanini uzima wa milele na mtayarishe mioyo yenu katika sala. Mimi nipo pamoja nanyi na ninamwomba Mwanangu kwa ajili ya kila mmoja wenu, hasa kwa wale waliojiweka wakfu kwangu na kwa Mwanangu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, nimewachagua ninyi, mitume wangu, kwa maana kila mmoja wenu huchukua ndani yake jambo njema. Ninyi mnaweza kunisaidia ili ule upendo ambao kwao Mwanangu amekufa, na kufufuka baadaye, ushinde tena. Kwa hiyo nawaalika, mitume wangu, kujaribu kuona katika kila kiumbe cha Mungu, katika wanangu wote, kitu chema na kujitahidi kuwaelewa. Wanangu, ninyi nyote ni kaka na dada kwa njia ya huyo Roho Mtakatifu. Ninyi mliojaa upendo kwa ajili ya Mwanangu, mnaweza kuwaeleza wote ambao hawajui cho chote kuhusu upendo huo, yote mnayoyafahamu. Ninyi mmejua upendo wa Mwanangu, mnaelewa ufufuko wake, na mnamgeuzia macho kwa furaha. Haja yangu ya kimama ni kwamba wanangu wote waungane katika upendo wa Yesu. Kwa hiyo nawaalika, mitume wangu, kuishi kwa furaha Ekaristi maana, katika Ekaristi, mwanangu anajitoa kwa ajili yenu tena na tena, na kwa mfano wake, anawaonyesha namna ya kutoa upendo na sadaka kwa jirani. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, miaka hii yote ambapo Mungu ananijalia kuwepo pamoja nanyi ni ishara ya upendo mwingi sana wa Mungu kwa kila mmoja wenu na ishara ya jinsi alivyowapenda. Wanangu, Yeye Aliye Juu amewapeni neema nyingi na anataka kuwapa neema nyingi zaidi. Lakini, wanangu, mioyo yenu imefungwa, inaishi katika hofu na hayaruhusu upendo wa Yesu na amani yake yapate nafasi katika mioyo yenu na kutawala maisha yenu. Kuishi pasipo Mungu ni kuishi gizani wala kutoujua kamwe upendo wa Baba na ulinzi wake kwa kila mmoja wenu. Kwa hiyo wanangu, leo hasa mwombeni Yesu ili tangu leo maisha yenu yapate kuzaliwa upya katika Mungu, na maisha yenu iwe nuru itokayo kwenu. Namna hii mtakuwa mashahidi wa uwepo wa Mungu ulimwenguni hasa kwa kila mtu aishiye gizani. Wanangu, nawapenda na kuwaombeeni kila siku kwake Yeye Aliye Juu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, Moyo wangu wa kimama hutaka wongofu wenu mnyofu na ya kuwa muwe na imani thabiti, ili muweze kuwatangazia watu wote wanaowazunguka upendo na amani. Lakini, wanangu, msisahau: kila mmoja wenu mbele ya Baba aliye Mbinguni ni ulimwengu wa pekee! Kwa hiyo nguvu ya Roho Mtakatifu isiyo kifani iweze kutenda kazi ndani mwenu! Muwe wanangu safi kwa kiroho. Katika karama ya kiroho kuna uzuri. Yote yaliyo ya kiroho ni hai na nzuri ajabu. Msisahau ya kuwa katika Ekaristi, iliyo moyo wa imani, Mwanangu yu daima pamoja nanyi. Yeye anawajia na pamoja nanyi humega mkate maana, Mwanangu, kwa ajili yenu amekufa, amefufuka akaja tena. Haya maneno yangu ni ya muhimu kwa maana ni ukweli, na ukweli haubadiliki: lakini wanangu wengi hawayatambui. Wanangu, maneno yangu si mazee wala mapya, ni ya milele. Kwa hiyo nawaalika ninyi, wanangu, kuangalia alama za nyakati, na "kukusanya misalaba yaliyovunjika" na kuwa mitume wa Ufunuo. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, uwepo wangu halisi na wa uhai katikati yenu uwafanye kuwa wenye furaha kwani huo ni upendo mkuu wa Mwanangu. Yeye ananituma katikati yenu ili, kwa upendo wa kimama, Mimi niwaimarishe; ili muelewe kwamba maumivu na furaha, mateso na mapendo husaidia nafsi yenu kuishi kwa bidii zaidi; ili niwaalike tena kuadhimisha Moyo wa Yesu, moyo wa imani: Ekaristi. Mwanangu, siku kwa siku, hurudi hai katikati yenu: huwarudia, hata kama hakuwaacha kamwe. Wakati mmoja wenu, wanangu, anamrudia, Moyo wangu wa kimama hushtuka kwa furaha. Kwa hiyo Wanangu, irudieni Ekaristi, mrudieni Mwanangu. Njia ya kumrudia Mwanangu ni ngumu na imejaa kujinyima lakini mwishowe, kuna mwanga siku zote. Naelewa maumivu yenu na mateso yenu, na kwa upendo wa kimama, ninapangusa machozi yenu. Mtumainini Mwanangu, kwa maana Yeye atawafanyieni neno msilojua hata kuomba. Ninyi, wanangu, fikirieni nafsi yenu tu, kwani nafsi ni kitu cha pekee mliyo nayo duniani. Chafu ama safi, mtaichukua mbele ya Baba aliye Mbinguni. Kumbukeni: imani katika upendo wa Mwanangu hulipwa siku zote. Nawaambieni kuwaombea hasa wale ambao Mwanangu aliwaita kuishi wakimfuata na kulipenda kundi lao. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nimekuja kwenu, katikati yenu, ili mnipe mahangaiko yenu, niweze kuyaleta mbele ya Mwanangu na kuwaombeeni kwake kwa manufaa yenu. Najua kuwa kila mmoja wenu ana mahangaiko yake, majaribu yake. Kwa hiyo kwa moyo wa kimama nawaalikeni: Njooni kwenye Meza ya Mwanangu! Yeye humega mkate kwa ajili yenu, huwapa Yeye mwenyewe. Huwapa matumaini. Anawaomba kuwa na imani zaidi, matumaini zaidi, utulivu zaidi. Anawaomba mpigane ndani yenu dhidi ya ubinafsi, hukumu na udhaifu wa kibinadamu. Kwa hiyo Mimi, kama Mama, nawaambieni: salini, maana sala huwapa nguvu ya kupigana ndani yenu. Mwanangu, alipokuwa mtoto, aliniambia mara nyingi ya kuwa wengi watanipenda na kuniita "Mama". Mimi hapa, katikati yenu, nasikia upendo na kuwashukuru! Kwa njia ya upendo huu namwomba Mwanangu ili hakuna hata mmoja wenu, wanangu, arudiye nyumbani jinsi alivyokuja. Ili mlete matumaini, rehema na upendo kadiri muwezavyo; ili muwe mitume wa upendo wangu, wanaoshuhudia kwa maisha yao kwamba Baba aliye Mbinguni ni chemchemi ya uzima si ya mauti. Wanangu wapendwa, nawaomba tena kwa moyo wa kimama: waombeeni wateule wa Mwanangu, kwa ajili ya mikono yao iliyobarikiwa, kwa ajili ya wachungaji wenu, ili waweze kumhubiri Mwanangu kwa upendo mwingi wawezavyo, na hivyo kusababisha wongofu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Leo nawaalika kusali. Sala na iwe maisha kwenu. Hivyo tu moyo wenu utajaa amani na furaha. Mungu atakuwa karibu nanyi, nanyi mtamhisi moyoni mwenu kama rafiki. Mtaongea naye kama na mmoja mjuaye na, wanangu, mtaona hitaji la kutoa ushuhuda maana Yesu atakuwa moyoni mwenu na ninyi mtaambatana naye. Mimi ni pamoja nanyi na kuwapenda nyote kwa upendo wangu wa kimama. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Katika tokeo la mwisho wa kila siku la tarehe 12 Septemba 1998 Mama Maria alimwambia Yakobo ya kuwa ataona tokeo lake mara moja kila mwaka, tarehe 25 Desemba, siku ya Kristmasi. Hivyo ikatokea na mwaka huu. Mama Maria ametokea pamoja na Mtoto Yesu mikononi mwake. Tokeo likaanza saa nane adhuhuri na dakika ishirini na kudumu dakika kumi. Yakobo, baadaye, akatoa ujumbe ufuatao:
Wanangu wapendwa, Leo katika siku hii ya neema nawaalika hasa kusali kwa ajili ya amani. Wanangu, nimekuja hapa kama Malkia wa Amani na mara nyingi nimewaalika kusali kwa ajili ya amani. Lakini wanangu, mioyo yenu imefadhaika. Dhambi inawazuia kufunguliwa kabisa kwa neema na amani ambayo Mungu ataka kuwapeni. Ili kuishi amani, wanangu, yawapasa kuwa kwanza na amani mioyoni mwenu na kujiachia kabisa kwa Mungu na mapenzi Yake. Msitafute amani na furaha katika mambo ya dunia hii maana haya yote hupita. Muelekee rehema ya kweli, amani itokayo kwa Mungu tu na hivyo mioyo wenu hivyo tu itajaa furaha ya kweli; hivyo tu mtaweza kuwa mashahidi wa amani katika dunia hii ya hofu. Mimi ni mama yenu na ninawaombea kila mmoja wenu mbele ya Mwanangu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Pendeni, salini na shuhudieni uwepo wangu kwa ajili ya wale wote walio mbali. Kwa njia ya ushuhuda wenu na mfano wenu mnaweza kuvuta mioyo iliyo mbali na Mungu na neema yake. Mimi nipo pamoja nanyi na kukuombeeni kila mmoja wenu ili kwa upendo na uhodari muweze kushuhudia na kuwahimiza wale wote walio mbali na Moyo wangu usio na doa. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, nawashukuru kwa kuitikia miito yangu na kukusanyika karibu nami, Mama yenu wa mbinguni. Najua kwamba mnanifikiri kwa upendo na matumaini. Mimi ninawapendeni nyote kama vile anavyowapendeni Mwanangu ambaye, kwa upendo wake wenye huruma, ananituma nije kwenu, mara nyingi pia. Yeye, aliyekuwa mtu na aliye Mungu, Mmoja na Utatu; Yeye aliyeteswa kwa ajili yenu mwilini na nafsini. Yeye aliyejifanya Mkate ailishe nafsi zenu na hivyo kuziokoa. Wanangu, nawafundisha jinsi ya kustahili upendo wake, kumwelekeza mawazo yenu, kumwishi Mwanangu. Mitume wa upendo wangu, ninawafunika kwa joho langu kwa sababu, kama Mama yenu, nataka kuwalinda. Nawasihi: mwuombee ulimwengu wote: moyo wangu unateswa. Dhambi zinaongezeka, ni nyingi mno. Lakini kwa msaada wenu – mlio wanyenyekevu, wanyofu, wenye upendo, watawa na watakatifu – moyo wangu utashinda. Mpendeni Mwanangu kupita wote na ulimwengu wote kwa njia yake. Msisahau kabisa ya kuwa kila ndugu yenu ana ndani yake kitu cha thamani: nafsi. Kwa hiyo, wanangu, pendeni wale wote wasiomjua Mwanangu ili kwa njia ya maombi na upendo utokao katika maombi, wawe wema zaidi. Ili wema uweze kushinda ndani yao. Ili nafsi zao ziweze kuokoka na kupata uzima wa milele. Enyi mitume wangu, wanangu. Mwanangu aliwaambieni mpendane. Hiyo iandikwe mioyoni mwenu na kwa kusali jaribuni kuishi upendo huu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nikiwatazama hapa mmekusanyika kunizunguka, Mama yenu, ninaona nafsi safi nyingi. Ninawaona wanangu wengi wanaotafuta upendo na faraja lakini hakuna mtu anayewapa. Ninawaona hata wale wanaotenda mabaya maana hawana mifano myema, maana hawajamjua mwanangu. Mwanangu anawatuma ninyi kwangu, Mama, sawa kwa wote, niwafundisheni kupenda, ili muelewe ya kuwa ninyi ni ndugu. Ninatamani kuwasaidia. Mitume wa upendo wangu, kwa mwanangu yamtosha tamaa hai ya imani na upendo na atayakubali, lakini mnapaswa kustahili, kuwa na tamaa na mioyo wazi, Mwanangu huingia katika mioyo wazi. Mimi kama Mama ninatamani kwamba mjue Mwanangu katika kweli: Mungu aliyezaliwa na Mungu, kwamba mjue ukuu wa Upendo wake, ambao mnahitaji. Yeye amezichukua juu yake dhambi zenu, ameupata Ukombozi wenu, na badala yake anaomba mpendane ninyi kwa ninyi. Mwanangu ni upendo, Yeye anawapenda watu wote bila tofauti, watu wote wa nchi zote, wa mataifa yote. Ikiwa ninyi, wanangu, mngeishi upendo wa Mwanangu, ufalme wake ungekwisha kuwa duniani. Kwa hiyo, Mitume wa upendo wangu, salini, salini ili Mwanangu na upendo wake wawe ndani yenu nanyi muweze kuwa mfano wa upendo na muweze kuwasaidia wote wale ambao hawajamjua Mwanangu. Msisahau kamwe kwamba Mwanangu, mmoja na utatu, anawapendeni. Pendeni na wombeeni wachungaji wenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Hii ni siku ambayo Bwana amenipa kwa kumshukuru kwa kila mmoja wenu, kwa wale walioongoka na waliokubali habari zangu na walioshika njia ya wongofu na ya utakatifu. Wanangu, furahini, maana Mungu ni mwenye rehema na anawapenda wote kwa Upendo wake mkubwa sana na kuwaongoza kuelekea njia ya wokovu kwa msaada wa kuja kwangu hapa. Mimi ninawapenda wote na ninawapa mwanangu ili Yeye awape amani. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, kwa upendo wa kimama ninawaalika kuifunua mioyo kwa imani, kuifunua mioyo kwa Mwanangu, ili katika mioyo yenu upendo kwa Mwanangu uimbe. Hakika, kutoka upendo huo tu, amani huingia nafsini. Wanangu, najua kwamba mna wema, najua kwamba mna upendo, upendo wenye rehema. Wanangu wangu wengi, lakini, wana moyo uliofungwa. Wanadhani kuweza kutenda pasipo kumwelekezea mawazo yao Baba wa mbinguni anayeangaza, pasipo kumwelekezea Mwanangu aliye daima pamoja nanyi katika Ekaristi na ataka kuwasikiliza. Wanangu, mbona hamzungumzi naye? Maisha ya kila mmoja wenu ni muhimu na ya thamani, maana ni zawadi ya Baba wa mbinguni kwa umilele. Kwa hiyo msisahau kamwe kumshukuru. Zungumzeni naye! Najua, enyi wanangu, ya kuwa mambo yatakayokuja hayajulikani kwenu lakini, mambo yenu ya mbele yatakapotokea, mtapata majibu yote. Upendo wangu wa kimama unataka muwe tayari. Wanangu, kwa maisha yenu wekeni katika mioyo ya watu mnaokutana hisia za amani, za mema, za upendo na msamaha. Kwa ajili ya sala, sikilizeni yanayowaambieni Mwanangu na tendeni namna hiyo. Ninawaalika tena kuwaombea wachungaji wenu, wale ambao Mwanangu aliwaita. Kumbukeni ya kuwa wanahitaji sala na upendo. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Wakati huu ndio wakati wa neema, wakati wa rehema kwa kila mmoja wenu. Wanangu, msiruhusu upepo wa chukio na hofu utawale ndani yenu na karibu nanyi. Ninyi, wanangu, mmealikwa kuwa upendo na sala. Ibilisi ataka hofu na fujo lakini ninyi, wanangu, muwe furaha ya Yesu Mfufuka ambaye amekufa na kufufuka kwa ajili ya kila mmoja wenu. Yeye ameshinda kifo kwa kuwapeni uzima, uzima wa milele. Kwa hiyo, wanangu, mshuhudieni na muwe wenye fahari kwa kufufuliwa katika Yeye. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, Namshukuru Mungu kwa kila mmoja wenu. Hasa, wanangu, asanteni kwa kuitikia wito wangu. Mimi ninawatayarisha kwa nyakati mpya ili muwe imara katika imani na kusali daima, ili Roho Mtakatifu atende kwa njia yenu na afanye upya uso wa nchi. Ninasali pamoja nanyi kwa amani, karama ya thamani kuliko zote, hata ingawa shetani hutaka vita na machukio. Ninyi, wanangu, muwe mikono yangu inayonyoshwa na tembeeni katika kujivunia pamoja na Mungu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
   




To compare Medjugorje messages with another language versions choose
1 2 Next>>

For God to live in your hearts, you must love.

`