Web address of the page: https://www.medjugorje.ws/sw/messages/highlight?find=hiyo 
www.medjugorje.ws » Our Lady of Medjugorje Messages » Our Lady of Medjugorje Messages containing 'hiyo'

Our Lady of Medjugorje Messages containing 'hiyo'

Total found: 115
Wanangu wapendwa! Salini, salini, mwendelee kusali ili mioyo yenu ifungukie kupokea imani jinsi ua linavyofunguka kuelekea mianga ya joto la jua. Huo ni wakati wa neema ambao Mungu anawajalia kwa njia ya uwepo wangu, lakini ninyi mpo mbali na moyo wangu. Kwa hiyo nawaalikeni kwa uongofu binafsi na kwenye sala katika familia zenu. Maandiko matakatifu yawe daima kichocheo chenu. Nawabariki nyote kwa baraka yangu ya kimama. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, katika wakati huu wa wasiwasi nawaalikeni tena kutembea nyuma ya Mwanangu, na kumfuata. Nayajua maumivu, mateso na taabu zenu, lakini katika Mwanangu mtapumzika, ndani yake mtapata amani na wokovu. Wanangu, msisahau ya kuwa Mwanangu amewakomboa ninyi kwa msalaba wake akawajalieni kuwa tena wana wa Mungu na kuwafundisha kumwita tena "Baba" yenu, Mungu aliye mbinguni. Ili muwe wapenzi wa Mungu Baba, basi muwe na mapendo na msamaha, kwa kuwa Baba yenu ni upendo na msamaha. Salini na fungeni, kwa maana hii ndiyo njia ya kujua na kumfahamu Baba aliye mbinguni. Mtakapomjua huyo Baba, mtafahamu ya kuwa Yeye tu ni muhimu kwenu (Maria Mtakatifu amenena hayo kwa nguvu na amkazo sana). Mimi, nikiwa Mama, nataka wanangu wawe watu wenye umoja ambamo Neno la Mungu husikilizwa na kutekelezwa. Kwa hiyo, enyi wanangu, mfuateni Mwanangu, muwe kitu kimoja naye, muwe wana wa Mungu. Pendeni wachungaji wenu kama vile Mwanangu alivyowapenda alipowaita kuwatumikia ninyi. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa, kwa upendo wa kimama nawaomba mnipe mioyo yenu ili niweze kumtolea Mwanangu, ili naye aweze kuiokoa, kuiokoa kutoka uovu wote unaowafanya daima kuwa watumwa na unaowafanya kuwa mbali na ule Wema wa pekee, yaani Mtoto wangu, anayewaokoa kutoka yote yale yanayowaongoza kwenye njia ya uovu na kuwaondolea amani. Mimi natamani kuwaongoza kwenye uhuru wa ahadi za Mtoto wangu, kwa kuwa natamani hapa yatimizwe hasa hasa mapenzi ya Mungu, ili kwa kupatanishwa na Baba wa Mbinguni, kufunga na kusali, waweze kuzaliwa mitume wa mapendo ya Mungu, yaani mitume watakaoeneza kwa mapendo na uhuru, Mapendo ya Mungu kwa watoto wangu wote, mitume watakaoeneza mapendo aminifu kwa Baba wa Mbinguni na hivyo kufungua milango ya mbingu. Watoto wapenzi, toeni furaha ya mapendo yenu na mshikamano wenu kwa wachungaji wenu kama vile Mtoto wangu alivyowaomba wao kutoa furaha hiyo. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, tafadhali muelewe, muwe tayari wote, kwa matumaini makuu, kufungua mioyo yenu; hivyo mngeelewa yote, mngeelewa kwa upendo gani nawaiteni, kwa upendo gani nataka kuwageuza, ili kuwafurahisha, kwa upendo gani nataka kuwafanya wafuasi wa Mwanangu na kuwapa amani katika ukamilifu wa Mwanangu. Mngeelewa ukuu wa moyo wangu wa kimama, kwa hiyo, wanangu, salini, maana kwa njia ya kusali tu imani yenu hukua na upendo wenu huzaliwa, upendo ambao utapunguza uzito wa msalaba kwa maana hamtakuwa peke yenu kuubeba. Katika umoja na Mwanangu, tukuzeni jina la Baba wa Mbinguni. Salini, salini mpate tuzo la upendo, maana upendo ni ukweli wa pekee, upendo husamehe yote, hutumikia wote na kuwaona wote kama ndugu. Enyi wanangu, mitume wangu, udhamini ambao Baba wa Mbinguni amewawekeni, kwa njia yangu, mtumishi Wake, ni kitu kikubwa, ili kusaidia wale wasiomjua, kusudi zapatanishwe naye, kusudi wamfuate, kwa hiyo nawafundisheni kupenda, maana mkiwa na upendo tu mnaweza kumjibu. Nawaalikeni tena: pendeni wachungaji wenu, salini ili katika wakati huu wa shida jina la Mwanangu atukuzwe kwa njia ya mwongozo wao. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Leo pia Yeye Aliye Juu anijalia neema ya kuwa pamoja nanyi na kuwaongoza mpate kutubu. Siku hata siku Mimi napanda mbegu na kuwaalika kutubu ili muweze kuwa sala, amani, upendo na ngano ambayo ikifa huzaa mara mia. Sipendi, wanangu wapendwa, mpate kujuta kwa yote mliyoweza kufanya wala hamkufanya. Kwa hiyo, enyi wanangu, tena kwa moyo wa furaha semeni: “ Nataka kuwa ishara kwa watu wengine”. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, nawapendeni, ninyi nyote, watoto wangu nyote, muwe wote moyoni mwangu, ninyi nyote mmepata upendo wangu wa kimama na ninatamani kuwaongoza nyote ili mjue furaha ya Mungu. Kwa hiyo nawaalikeni: nahitaji mitume wanyenyekevu ambao, kwa moyo mkunjufu, wanapokea Neno la Mungu na ambao wako tayari kuwasaidia watu wengine ili, kwa njia ya Neno la Mungu, waelewe maana ya maisha yao. Ili muweze kufanya hayo, wanangu, yawapasa, kwa njia ya kusali na kufunga, kusikiliza kwa moyo mkunjufu na kujifunza kujidhili au kujinyenyekesha. Yawapasa kujifunza kukataa yote yanayowatenganisha na Neno la Mungu na kutamani tu yanayowakaribisha. Msiogope, mimi nipo hapa. Ninyi si peke yenu. Namwomba Roho Mtakatifu ili awafanye wapya, ili awaimarishe. Namwomba Roho Mtakatifu, ili mkisaidia wengine, muweze kujiponya nyinyi wenyewe. Naomba ili, kwa njia yake, muwe wana wa Mungu na mitume wangu.
Kisha kwa mahangaiko makubwa Bikira Maria alisema:
Kwa ajili ya Yesu, kwa ajili ya mwanangu, pendeni wale ambao Yeye aliwaita mkitamani baraka ya mikono ile ambayo Yeye tu ameyaweka wakfu. Msiyaruhusu maovu yatawale. Nawaalikeni tena: ni kwa njia ya wachungaji wangu tu moyo wangu utashinda. Msiyaruhusu maovu yawatenganisheni na wachungaji wenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Leo pia nawaalikeni kusali. Uhusiano wenu na kusali uwe wa kila siku. Sala inasababisha miujiza ndani yenu na kwa njia yenu, na kwa hiyo, enyi wanangu, sala basi iwe ni furaha yenu. Hivyo uhusiano wenu na maisha utakuwa wa kina na wazi zaidi, pia mtaelewa kwamba maisha ni zawadi kwa kila mmoja wenu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Leo nawaalikeni mjifungulie kwa sali. Sala itasababisha miujiza ndani yenu na kwa njia yenu. Kwa hiyo, enyi wanangu, kwa moyo mkunjufu mtafuteni Yeye Aliye Juu ili awapeni nguvu ya kuwa wana wa Mungu, na yule Shetani asiwatikiseni kama matawi yatikiswavyo na upepo. Kateni shauri tena, wanangu, kwa Mungu na tafuteni tu mapenzi yake, hapo mtapata furaha na amani. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, kwa moyo wa kimama nawaalikeni tena kupenda, kusali bila kukata tamaa kwa zawadi ya upendo, kumpenda Baba wa Mbinguni zaidi ya yote. Mtakapompenda Yeye, mtajipenda wenyewe na jirani zenu. Mambo hayo hayawezi kutengana. Baba wa Mbinguni yumo katika kila mtu, hupenda kila mtu na kumwita kila mtu kwa jina lake. Kwa hiyo, wanangu, kwa njia ya kusali sikilizeni atakalo Baba wa Mbinguni. Ongeeni na Yeye. Muwe na uhusiano wa binafsi pamoja na Baba, atakayeufanya mkubwa zaidi uhusiano wake nanyi, jumuhiya ya wanangu, mitume wangu. Kama Mama napenda kwamba, kwa njia ya upendo kumwelekea Baba wa Mbinguni, inukeni juu ya ubatili wa malimwengu na muwasaidie wengine kujua na kumjongea polepole Baba wa Mbinguni. Wanangu, salini, salini, salini kwa zawadi ya upendo, kwa sababu upendo ndiye Mwanangu. Muwaombee wachungaji wenu, ili wawapende ninyi siku zote, kama vile Mwanangu alivyowapenda ninyi na kuonyesha akitoa maisha yake kwa wokovu wenu. Nawashukuruni.
Wanangu wapendwa, kwa upendo wa kimama na uvumilivu wa kimama naona kutangatanga kwenu na kuendelea kupotea kwenu. Kwa sababu hiyo mimi nipo pamoja nanyi. Nataka kwanza kabisa kuwasaidieni kupata kujijua ninyi wenyewe, ili baadaye muweze kuelewa na kutambua yote yanayowazuia kujua bila unafiki na kwa moyo wote upendo wa Baba wa Mbinguni. Wanangu, Baba hujulikana kwa njia ya msalaba: kwa hiyo msikatae msalaba: kwa msaada wangu, mkafanye bidii kuuelewa na kuupokea. Mtakapoweza kuupokea msalaba, mtaelewa pia upendo wa Baba wa Mbinguni. Mtatembea pamoja na Mwanangu na mimi. Mtajipambanua na wale ambao hawakujua upendo wa Baba wa Mbinguni, kujitofautisha na wale wanaomsikiliza lakini hawamwelewi, na wale wasioenda pamoja naye, na wasiomjua. Mimi nataka ninyi mjue ukweli wa Mwanangu na muwe mitume wangu; ili, kama wana wa Mungu, muwe na mawazo yaliyo juu ya mawazo ya kibinadamu na siku zote na katika yote mkatafute kila mara mawazo ya Mungu. Wanangu, salini na fungeni ili muweze kuelewa yote ninayowaombeni. Muombee wachungaji wenu mkatamani kujua, mkishirikiana nao, upendo wa Baba wa Mbinguni. Nawashukuruni.
Wanangu wapendwa! Kwa upendo wa kimama nataka kuwafundisha uadilifu, natamani kwamba katika kutenda kwenu kazi kama mitume wangu muwe wenye haki, maamuzi na hasa waadilifu. Natamani kwamba, kwa neema ya Mungu, muweze kupokea Baraka ya Mungu. Natamani, kwa njia ya kufunga na kusali, muweze kupata kutoka kwa Baba wa Mbinguni ujuzi, uhalali, utakatifu wa kimungu. Kwa ulinzi wa Mwanangu na wangu mtakuwa mitume wangu, ambao wanaweza kueneza neno la Mungu kwa wote wasiolijua, na mtaweza kushinda mapingamizi mtakayokutana nayo njiani. Wanangu, kwa njia ya baraka neema itawashukia, nanyi mtaweza kuilinda neema hiyo kwa kufunga na kusali, kwa kujitakasa na kujipatanisha. Mtakuwa na utendaji fanisi ninaohitaji kutoka kwenu. Waombeeni wachungaji wenu ili mionzi ya neema ya Mungu iangaze njia yao. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Naja kwenu kama Mama na ninatamani kuwa kwangu kama Mama mtapata maskani, faraja na mapumziko. Kwa hiyo, wanangu, mitume wa upendo wangu, salini! Salini kwa moyo mkunjufu, utii na uaminifu kamili kwa Baba wa Mbinguni. Muwe na uaminifu, kama vile mimi pia nilivyokuwa mwaminifu nilipoambiwa ya kuwa nitachukua baraka za ahadi. Basi kutoka mioyo yenu yafike siku zote midomoni mwenu maneno haya "Utakalo lifanyike". Kwa hiyo muwe na uaminifu na salini, ili mimi niweze kuwaombeeni kwa Bwana, ili awape Baraka ya Mbinguni na kuwajaza Roho Mtakatifu. Hapo mtaweza kuwasaidia wale wote wasiomjua Bwana. Ninyi, mitume wa upendo wangu, mtawasaidia kumwita "Baba" kwa uaminifu wote. Salini kwa ajili ya wachungaji wenu na mujiaminishe katika mikono yao iliyobarikiwa. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Kwa upendo wa kimama nataka kuwasaidia ili maisha yenu ya kusali na kutubu iwe juhudi ya kweli ya kumjongea Mwanangu na nuru yake ya kimungu, ili muweze kutengana na dhambi. Kila sala, kila Misa na kila mfungo ni juhudi ya kumjongea Mwanangu, msukumo kwa utukufu wake na kuepukana na dhambi. Ni njia ya muungano mpya wa Baba mwema na wanao. Kwa hiyo, wanangu wapendwa, kwa unyofu wa moyo uliojaa upendo mliite jina la Baba wa Mbinguni, ili awatie nuru ya Roho Mtakatifu. Kwa njia ya Roho Mtakatifu mtakuwa chemchemi ya upendo wa Mungu: kwenye chemchemi hiyo wale wote wasiomjua Mwanangu watakunywa, wote wenye kiu ya upendo na amani ya Mwanangu. Nawashukuru! Salini kwa ajili ya wachungaji wenu. Mimi nawaombee na nataka waonje siku zote baraka ya mikono yangu na tegemeo la Moyo wangu wa kimama.
Wanangu wapendwa! Mimi, Mama yenu, nipo pamoja nanyi kwa ajili yenu, kwa mahitaji yenu na mafundisho yenu binafsi. Baba wa Mbinguni amewapa uhuru wa kuamua peke yenu na kujua peke yenu. Mimi nataka kuwasaidieni. Nataka kuwa Mama kwenu, mwalimu wa ukweli, ili kwa unyofu wa moyo wazi mjue usafi usio na mwisho, na mwanga utokao kwa hiyo ukweli ili kutawanya giza, yaani mwanga uletao tumaini. Mimi, wanangu, naelewa maumivu yenu na mateso yenu. Nani aweza kuwaelewa zaidi kuliko Mama mmoja! Lakini enyi wanangu? Mjue kuwa idadi ya wanaonielewa na kunifuata ni ndogo. Pia ni kubwa idadi ya waliopotea, hao ambao hawajajua ukweli ulio katika Mwanangu. Kwa hiyo, enyi mitume wangu, salini na tendeni kazi. Mbebe mwanga, msipoteze tumaini. Mimi nipo nanyi na hasa pamoja na wachungaji wenu. Nawapenda na kuwalinda kwa Moyo wa kimama, ili kusudi wao wanawaongozeni Paradisini alikowaahidia Mwanangu. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa! Salini na mfahamu ya kwamba pasipo Mungu ninyi ni mavumbi. Kwa hiyo geuzeni fikira zenu na mioyo yenu kwa Mungu na kwa sala. Tegemeeni upendo Wake. Katika Roho ya Mungu ninyi nyote mnaalikwa kuwa mashahidi. Ninyi mna thamani mbele ya Mungu, nami nawaalika, wanangu, kuwa watakatifu, ili mweze kupata uzima wa milele. Kwa hiyo mfahamu ya kwamba maisha haya hupita. Nawapendeni na kuwaalika kwa maisha mapya ya kutubu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Yeye Aliye Juu ananipa neema ya kuweza kuwa tena pamoja nanyi na kuwaongoza katika sala kuelekea njia ya amani. Mioyo yenu na roho zenu zina kiu ya amani na upendo, ya Mungu na ya furaha yake. Kwa hiyo, wanangu, salini, salini, salini na katika sala mtapata hekima ya kuishi. Nawabarikieni na kukuombeeni mbele ya Mwanangu Yesu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Mimi Mama yenu, ninyi mliokusanyika hapa na Mama wa ulimwengu mzima, nawabariki kwa baraka ya kimama na kuwaalika kuanza safari katika njia ya unyenyekevu. Njia hiyo inawaongoza katika ujuzi wa upendo wa Mwanangu. Mwanangu ni Mwenye uwezo. Yeye yumo katika kila kitu. Kama ninyi, wanangu, hamelewi hayo, basi mtambue kuwa katika roho yenu giza na upofu zinatawala. Unyenyekevu tu huweza kuwaponya. Wanangu, mimi nilikuwa nimeishi daima kwa unyenyekevu, kwa uhodari na kwa matumaini. Nilijua, nilikuwa nimeelewa ya kuwa Mungu yu ndani yetu na sisi ndani ya Mungu. Nawaombeni kuelewa vile vile. Nataka ninyi nyote muwe pamoja nami katika umilele, maana ninyi ni sehemu yangu. Katika njia yenu nitawasaidia. Upendo wangu utawafunika kama joho na kuwafanya ninyi mitume wa mwanga wangu, wa mwanga wa Mungu. Kwa upendo utokao katika unyenyekevu, mtaleta mwanga palipotawala giza na upofu. Mtaleta Mwanangu, aliye mwanga wa ulimwengu. Mimi ni sikuzote kando ya wachungaji wenu na kusali ili wawe siku zote kwenu mfano wa unyenyekevu. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa! Salini kwa nia zangu maana Shetani ataka kuangamiza mpango wangu nilio nao hapa na kuwaibia amani: Kwa hiyo, wanangu, salini, salini, salini ili Mungu aweze kutenda kazi kwa njia ya kila mmoja wenu. Mioyo yenu iwe wazi kupokea mapenzi ya Mungu. Mimi nawapendeni na kubariki kwa baraka ya kimama. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Salini katika kipindi hiki cha neema na ombeni maombezi ya Watakatifu wote ambao wapo tayari katika mwanga. Wao wawe mfano na kichocheo kwenu siku hata siku, katika njia ya uwongofu wenu. Wanangu, mfahamu ya kuwa maisha yenu ni mafupi na ya kupita upesi. Kwa hiyo tamanini uzima wa milele na mtayarishe mioyo yenu katika sala. Mimi nipo pamoja nanyi na ninamwomba Mwanangu kwa ajili ya kila mmoja wenu, hasa kwa wale waliojiweka wakfu kwangu na kwa Mwanangu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, mimi nipo pamoja nanyi kwa baraka ya Mwanangu, pamoja nanyi mnaonipenda na mnaotafuta kunifuata. Mimi natamani kuwa pia pamoja nanyi ambao hamtaki kunipokea. Kwenu nyote nafungua moyo wangu wote wa mapendo na kuwabariki kwa mikono yangu ya kimama. Mimi ni Mama ninayewaelewa: nilikuwa nimeishi maisha yenu na kujaribu mateso na furaha yenu. Ninyi mnaoishi katika mateso, mnafahamu maumivu yangu na mateso yangu kwa ajili ya wale wanangu wasiokubali kuangazwa na mwanga wa Mwanangu, kwa wale wanangu wanaoishi gizani. Kwa hiyo nawahitaji ninyi, ninyi mlioangazwa na mwanga na kuufahamu ukweli. Nawaalika kumwabudu Mwanangu, ili moyo wenu ukue na kuyafikia kweli maisha ya kiroho. Basi mitume wangu, natumaini mtaweza kunisaidia. Kunisaidia maana yake ni kuwaombea wale ambao hawajajua upendo wa Mwanangu. Mkiwaombea, mtamwonyesha Mwanangu ya kuwa mnampenda na kumfuata. Mwanangu aliniahidi kwamba uovu hautashinda kamwe, kwa sababu hapo mpo ninyi, roho za wenye haki: ninyi mnaojaribu kusali sala zenu kwa moyo wote; ninyi mnaotolea maumivu na mateso yenu kwa Mwanangu; ninyi mnaofahamu ya kuwa maisha ni kufumba na kufumbua tu; ninyi mnaotamani Ufalme wa mbinguni. Hayo yote huwafanya muwe mitume wangu na kuwaongoza kwenye shangwe ya Moyo wangu. Kwa hiyo wanangu, takaseni mioyo yenu mkamwabudu Mwanangu. Nawashukuru!
1 2 3 4 5 6 Next>>