Web address of the page: https://www.medjugorje.ws/sw/messages/highlight?find=matumaini 
www.medjugorje.ws » Our Lady of Medjugorje Messages » Our Lady of Medjugorje Messages containing 'matumaini'

Our Lady of Medjugorje Messages containing 'matumaini'

Total found: 42
Wanangu wapendwa, tafadhali muelewe, muwe tayari wote, kwa matumaini makuu, kufungua mioyo yenu; hivyo mngeelewa yote, mngeelewa kwa upendo gani nawaiteni, kwa upendo gani nataka kuwageuza, ili kuwafurahisha, kwa upendo gani nataka kuwafanya wafuasi wa Mwanangu na kuwapa amani katika ukamilifu wa Mwanangu. Mngeelewa ukuu wa moyo wangu wa kimama, kwa hiyo, wanangu, salini, maana kwa njia ya kusali tu imani yenu hukua na upendo wenu huzaliwa, upendo ambao utapunguza uzito wa msalaba kwa maana hamtakuwa peke yenu kuubeba. Katika umoja na Mwanangu, tukuzeni jina la Baba wa Mbinguni. Salini, salini mpate tuzo la upendo, maana upendo ni ukweli wa pekee, upendo husamehe yote, hutumikia wote na kuwaona wote kama ndugu. Enyi wanangu, mitume wangu, udhamini ambao Baba wa Mbinguni amewawekeni, kwa njia yangu, mtumishi Wake, ni kitu kikubwa, ili kusaidia wale wasiomjua, kusudi zapatanishwe naye, kusudi wamfuate, kwa hiyo nawafundisheni kupenda, maana mkiwa na upendo tu mnaweza kumjibu. Nawaalikeni tena: pendeni wachungaji wenu, salini ili katika wakati huu wa shida jina la Mwanangu atukuzwe kwa njia ya mwongozo wao. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Mimi Mama yenu, ninyi mliokusanyika hapa na Mama wa ulimwengu mzima, nawabariki kwa baraka ya kimama na kuwaalika kuanza safari katika njia ya unyenyekevu. Njia hiyo inawaongoza katika ujuzi wa upendo wa Mwanangu. Mwanangu ni Mwenye uwezo. Yeye yumo katika kila kitu. Kama ninyi, wanangu, hamelewi hayo, basi mtambue kuwa katika roho yenu giza na upofu zinatawala. Unyenyekevu tu huweza kuwaponya. Wanangu, mimi nilikuwa nimeishi daima kwa unyenyekevu, kwa uhodari na kwa matumaini. Nilijua, nilikuwa nimeelewa ya kuwa Mungu yu ndani yetu na sisi ndani ya Mungu. Nawaombeni kuelewa vile vile. Nataka ninyi nyote muwe pamoja nami katika umilele, maana ninyi ni sehemu yangu. Katika njia yenu nitawasaidia. Upendo wangu utawafunika kama joho na kuwafanya ninyi mitume wa mwanga wangu, wa mwanga wa Mungu. Kwa upendo utokao katika unyenyekevu, mtaleta mwanga palipotawala giza na upofu. Mtaleta Mwanangu, aliye mwanga wa ulimwengu. Mimi ni sikuzote kando ya wachungaji wenu na kusali ili wawe siku zote kwenu mfano wa unyenyekevu. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa! Leo kwa namna ya pekee nawaalikeni msali. Salini, wanangu, ili muweze kutambua ninyi ni akina nani na ni wapi mnayopaswa kwenda. Muwe watangazaji wa Habari Njema na watu wa matumaini. Muwe upendo kwa wale wote wasio na upendo. Wanangu, mtakuwa yote na kuyatimiza yote iwapo tu mkisali na mkiwa tayari kupokea mapenzi ya Mungu, Mungu ambaye anatamani kuwaongoza katika maisha ya uzima wa milele. Mimi nipo pamoja nanyi na siku hata siku ninawaombeeni kwa Mwanangu Yesu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, zingatieni akilini, kwa maana nawaambia: upendo utashinda! Najua ya kuwa wengi wenu wanapoteza matumaini kwa kuwa wanaona wamezungukwa na mateso, maumivu, husuda na wivu, hata hivyo mimi ni Mama yenu. Mimi nipo katika Ufalme, lakini hata hapa nipo pamoja nanyi. Mwanangu ananituma tena ili niwasaidieni, kwa hiyo msipoteze matumaini ila nifuateni, kwa maana ushindi wa Moyo wangu ni kwa jina la Mungu. Mwanangu mpendwa anawafikiria, kama alivyofanya siku zote: mwaminini na mwishi kama Yeye! Yeye ni uzima wa ulimwengu. Wanangu, kumwishi Mwanangu maana yake ni kuishi Injili. Si kitu rahisi. Ni jambo linalodai upendo, rehema na sadaka. Hayo huwatakasa na kufungua Ufalme: Sala nyofu, isiyo maneno bali itokayo moyoni, itawasaidieni. Vivyo hivyo kufunga, maana hayo huleta ongezeko la upendo, rehema na sadaka. Kwa hiyo msipoteze matumaini, ila nifuateni. Nawaomba tena msali kwa ajili ya wachungaji wenu, ili wamtazame daima Mwanangu, aliyekuwa Mchungaji wa kwanza wa ulimwengu, na ambaye familia yake ilikuwa ulimwengu wote. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa! Hata leo ninawaalika: ishini katika sala mwito wenu. Leo, kama bado haijatokea awali, Shetani atamani kumfunga pumzi binadamu na roho yake kwa njia ya upepo wake unaoambukiza chukio na hofu. Katika mioyo mingi hakuna furaha kwa sababu hakuna Mungu wala sala. Uadui na vita zinaongezeka siku hata siku. Ninawaalika, wanangu, anzisheni upya kwa ari mwelekeo wa kutafuta utakatifu na upendo kwa maana nimekuja katikati yenu kwa ajili hiyo. Tuwe upendo na msamaha kwa wale wote wanaofahamu na kutaka kupenda kwa mapendo ya kibinadamu tu wala siyo kwa ule upendo mkubwa sana wa kimungu ambao Mungu anatualikia. Wanangu, matumaini ya kesho iliyo bora zaidi yawe daima mioyoni mwenu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, ninyi ni nguvu yangu. Ninyi, mitume wangu, ambao, kwa upendo wenu, unyenyekevu na sala ya kimya kimya, mnamwezesha Mwanangu ajulikane. Ninyi mnaishi ndani yangu. Ninyi mnanibeba mioyoni mwenu. Ninyi mnajua ya kuwa mna Mama awapendaye na aliyekuja kuwaletea upendo. Nawatazama katika Baba wa Mbinguni, natazama fikira zenu, maumivu yenu, mateso yenu na kuyaleta kwa Mwanangu. Msiogope! Msipoteze matumaini, maana Mwanangu humsikiliza Mama yake. Yeye hupenda tangu alipozaliwa, na ndio furaha yangu ya kuwa wanangu wote wajue upendo huo; na wote wale ambao, kwa sababu ya maumivu yao na kutoelewa kwao, walimwacha waweze kurudi kwake, na wote wao wasiomjua wamjue. Kwa sababu hiyo ninyi hapa ni mitume wangu, nami pia pamoja nanyi kama Mama yenu. Salini ili kuwa imara katika imani, maana upendo na rehema hutoka katika imani imara. Kwa njia ya upendo na rehema mtawasaidia wale wote wasiofahamu ya kuwa wanachagua giza badala ya nuru. Salini kwa ajili ya wachungaji wenu, maana wao ni nguvu ya Kanisa ambayo Mwanangu aliwaachieni. Kwa njia ya Mwanangu wao ni wachungaji wa roho. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nataka kuongea nanyi tena juu ya upendo. Nimewakusanya kunizunguka kwa Jina la Mwanangu, kwa kadiri ya mapenzi yake. Nataka imani yenu iwe thabiti na iwe inatokana na mapendo, kwa maana wanangu wale wanaoelewa upendo wa Mwanangu na kuufuata, huishi katika mapendo na matumaini. Wamejua upendo wa Mungu. Kwa hiyo, wanangu, salini, salini ili muweze kupenda zaidi muwezavyo na kutenda matendo ya upendo. Kwa maana, imani peke yake, pasipo upendo wala matendo ya upendo, si neno ninaloomba kwenu. Wanangu, ule ni utovu wa imani, ni kujisifu mwenyewe. Mwanangu hutaka imani na matendo, upendo na wema. Mimi ninasali, lakini nawaombeni pia kusali na kuishi upendo, kwa maana nataka ya kuwa Mwanangu, atakapoona mioyo ya wanangu wote, aweze kuona ndani yake upendo na wema, sio chukio na ubaridi. Wanangu, mitume ya upendo wangu, msipoteze tumaini, msikate tamaa: ninyi mnaweza kufanya! Mimi ninawapeni moyo na kuwabariki, maana yote yaliyopo duniani hapa - ambayo kwa bahati mbaya wanangu wengi huweka mahali pa kwanza - yatatoweka na upendo na matendo ya upendo tu zitabaki, nazo zitawafungulia malango ya Ufalme wa Mbinguni. Nitawangojea karibu na malango hayo, karibu na malango hayo nataka kuwangojea na kuwakumbatia wanangu wote. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, kama Mama nafurahi ya kuwa katikati yenu, kwa maana nataka kuongea nanyi tena kuhusu maneno ya Mwanangu na upendo wake. Natumaini mtanipokea kwa upendo, maana maneno ya Mwanangu na upendo wake ni nuru na tumaini la pekee katika giza la siku hizi. Huu ni ukweli wa pekee, nanyi mtakaoupokea na kuuishi, mtakuwa na mioyo safi na minyenyekevu. Mwanangu hupenda mioyo safi na minyenyekevu. Mioyo safi na minyenyekevu inahuisha maneno ya Mwanangu: inayaishi, inayaeneza na kufanya hata wote wayasikie. Maneno ya Mwanangu yanaamsha maisha ya wale wanaoyasikiliza, maneno ya Mwanangu hurudisha upendo na matumaini. Kwa hiyo, mitume wangu wapenzi, wanangu, isheni maneno ya Mwanangu. Pendaneni kama Yeye alivyowapenda. Pendaneni katika jina lake na kumbukumbu lake. Kanisa huendelea na kukua kwa ajili ya wale wanaosikiliza maneno ya Mwanangu, kwa sababu ya wanaohuzunika na kuteseka kimyakimya katika tumaini la kukombolewa milele. Kwa hiyo wanangu wapendwa, maneno ya Mwanangu na upendo wake yawe wazo la kwanza na la mwisho la siku yenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Katika wakati huu wa neema nawaalikeni nyote kuongoka. Wanangu, mnapenda kidogo, na bado mnasali kidogo. Mmepotea wala hamjui lengo lenu ni nini. Chukueni msalaba wenu, mwangalieni Yesu mumfuate. Yeye anajitoa kwenu hata kufa msalabani maana anawapenda. Wanangu, nawaalikeni kurudia kusali kwa moyo kwa maana katika sala mnaweza kupata matumaini na maana ya uwepo wenu. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaombea. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, msiwe na mioyo migumu, iliyofungwa na iliyojaa hofu. Pokeeni upendo wangu wa kimama uiangaze na kuijaza mioyo yenu upendo na matumaini, ili, kama Mama, niyalainishe maumivu yenu: ninayajua, na nimeyaonja. Maumivu huinua nayo ni sala kuu kuliko zote. Mwanangu huwapenda hasa wanaopokea maumivu. Alinituma Mimi niyalainishe na kuwaletea matumaini. Mumwamini Yeye. Najua kuwa ni vigumu kwenu, maana mnaona giza linalozidi kuongeza karibu yenu pande zote. Wanangu, giza mtalivunja kwa njia ya sala na upendo. Yule anayesali na kupenda haogopi, ana matumaini na upendo wenye huruma: Anaona mwanga, na anamwona Mwanangu. Kama mitume wangu nawaalika mjaribu kuwa mfano wa upendo wenye huruma na wenye matumaini. Salini sikuzote tena kwa ajili ya kupata upendo mwingi kadiri muwezavyo, maana upendo huleta mwanga unaovunja kila giza, na humleta Mwanangu. Msiogope, ninyi si peke yenu: Mimi nipo pamoja nanyi! Ninawasihi waombeeni wachungaji wenu, ili wawe na upendo kila wakati na wawe na matendo ya upendo kwa Mwanangu, kwa njia yake na kwa kumkumbuka Yeye. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nimekuja kwenu, katikati yenu, ili mnipe mahangaiko yenu, niweze kuyaleta mbele ya Mwanangu na kuwaombeeni kwake kwa manufaa yenu. Najua kuwa kila mmoja wenu ana mahangaiko yake, majaribu yake. Kwa hiyo kwa moyo wa kimama nawaalikeni: Njooni kwenye Meza ya Mwanangu! Yeye humega mkate kwa ajili yenu, huwapa Yeye mwenyewe. Huwapa matumaini. Anawaomba kuwa na imani zaidi, matumaini zaidi, utulivu zaidi. Anawaomba mpigane ndani yenu dhidi ya ubinafsi, hukumu na udhaifu wa kibinadamu. Kwa hiyo Mimi, kama Mama, nawaambieni: salini, maana sala huwapa nguvu ya kupigana ndani yenu. Mwanangu, alipokuwa mtoto, aliniambia mara nyingi ya kuwa wengi watanipenda na kuniita "Mama". Mimi hapa, katikati yenu, nasikia upendo na kuwashukuru! Kwa njia ya upendo huu namwomba Mwanangu ili hakuna hata mmoja wenu, wanangu, arudiye nyumbani jinsi alivyokuja. Ili mlete matumaini, rehema na upendo kadiri muwezavyo; ili muwe mitume wa upendo wangu, wanaoshuhudia kwa maisha yao kwamba Baba aliye Mbinguni ni chemchemi ya uzima si ya mauti. Wanangu wapendwa, nawaomba tena kwa moyo wa kimama: waombeeni wateule wa Mwanangu, kwa ajili ya mikono yao iliyobarikiwa, kwa ajili ya wachungaji wenu, ili waweze kumhubiri Mwanangu kwa upendo mwingi wawezavyo, na hivyo kusababisha wongofu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Leo nataka kushirikiana pamoja nanyi furaha ya mbinguni. Ninyi wanangu fungueni mlango wa moyo ili katika moyo wenu matumaini, amani na mapendo ambazo Mungu peke yake anaweza kutoa ziweze kukua. Wanangu, mnapenda mno dunia na mambo ya dunia, kwa hiyo Shetani huwatikisa kama upepo ufanyavyo na mawimbi ya bahari. Kwa hiyo mnyororo wa maisha yenu uwe sala ya moyo na kumwabudu Mwanangu Yesu. Kwake mtolee maisha yenu yajayo ili muwe ndani Yake furaha na mfano kwa watu wengine kwa njia ya matendo yenu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, kulingana na mapenzi ya Mwanangu na upendo wangu wa kimama naja kwenu, wanangu, hasa kwa wale ambao hawajajua bado upendo wa Mwanangu. Ninakuja kwenu mnaonifikiria, mnaoomba msaada wangu. Ninawapa upendo wangu wa kimama na kuwaletea baraka ya Mwanangu. Mnayo mioyo safi na wazi? Mnaona dalili za uwepo wangu na upendo wangu? Wanangu, katika maisha yenu ya dunia igieni moyo na mfano wangu. Maisha yangu yalikuwa maumivu, ukimya, imani na matumaini pasipo mipaka katika Baba wa Mbinguni. Hakuna kitu cha bahati: si maumivu, si furaha, si mateso, si upendo. Hizo zote ni neema ambazo Mwanangu anawapeni na zinazowaongoza kwenye uzima wa milele. Mwanangu anawaomba mapendo na sala ndani yake. Kupenda na kusali ndani yake maana yake — kama Mama nataka kuwafundisha — ni kusali katika ukimya wa nafsi zenu, si kusema kwa midomo tu. Ni tendo dogo zuri litendwalo kwa jina la Mwanangu; ni uvumilivu, rehema, upokeaji wa maumivu na kujitolea kwa ajili ya wengine. Wanangu, Mwanangu huwatazama. Ombeni ili ninyi pia muuone uso wake, na ili uso huo uweze kufunuliwa kwenu. Wanangu, mimi nawafunulia ukweli halisi wa pekee. Salini kwa kuyaelewa na kuweza kueneza mapendo na matumaini, kwa kuweza kuwa mitume wa upendo wangu. Moyo wangu wa kimama hupenda hasa wachungaji. Iombeeni mikono yao iliyobarikiwa. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, Roho Mtakatifu, kwa njia ya Baba wa Mbinguni, amenifanya Mama: Mama wa Yesu na, kwa hiyo, Mama yenu vilivile. Kwa hiyo nawajilia niwasikilize, niwafungulie mikono yangu ya kimama, niwapeni Moyo wangu na kuwaalika kukaa pamoja nami, kwa maana kutoka juu ya msalaba Mwanangu amenikabidhi ninyi. Kwa bahati mbaya wanangu wengi hawakujua upendo wa Mwanangu, wengi hawataka kumjua. Loo, wanangu, mabaya mengi yatoka kwa wale ambao hawana budi ya kuona na kuelewa ili kuamini! Kwa hiyo, wanangu, mitume wangu, katika kimya ya moyo wenu sikilizeni sauti ya Mwanangu, ili moyo wenu uwe makazi yake wala usiwe giza na huzuni, bali uangaziwe na mwanga wa Mwanangu. Tafuteni matumaini kwa imani, maana imani ni maisha ya roho. Ninawaalika tena: salini! Salini ili kuishi imani katika unyenyekevu, katika amani ya kiroho na mkiangaziwa na mwanga. Wanangu, msijaribu kuelewa yote mara moja, maana Mimi nami sikuelewa yote mara moja, lakini niliyaamini maneno ya kimungu aliyoyasema Mwanangu, Yeye aliyekuwa mwanga wa kwanza na mwanzo wa Ukombozi. Enyi mitume wa moyo wangu, ninyi mnaosali, mnaojitolea, mnaopenda wala msiohukumu: ninyi nendeni mkaeneze ukweli, maneno ya Mwanangu, Injili. Ninyi kweli, ni Injili iliyo hai, ninyi ni miali ya mwanga wa Mwanangu. Mwanangu na mimi tutakuwa karibu nanyi, tutawatia moyo na kuwajaribu. Wanangu, ombeeni daima na hasa baraka ya wale ambao Mwanangu amebariki mikono yao, yaani Wachungaji wenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, Moyo wangu wa kimama unalia machozi ninapoyaona yale wanayoyafanya wanangu. Dhambi zinaongezeka, usafi wa moyo unaendelea kupoteza umuhimu wake. Mwanangu amesahauliwa na upendo kwake unaendelea kupunguka na wanangu wanateswa. Kwa hiyo, wanangu, mitume wa moyo wangu, iteni jina la Mwanangu kwa nafsi na kwa moyo: Yeye atakuwa na maneno ya mwanga kwenu. Naye atajionyesha kwenu, anashiriki Mkate pamoja nanyi na anawapa maneno ya upendo, ili myageuze kuwa matendo ya huruma na muwe hivyo mashahidi ya ukweli. Kwa hiyo, wanangu, msiogope! Acheni Mwanangu awe ndani yenu. Yeye atawatumia ninyi ili kuzitibu nafsi zinazojeruhiwa na kuziongoka zile zinazopotea. Kwa hiyo, wanangu, rudieni kusali Rozari. Mwisali kwa roho ya ukarimu, ya sadaka na ya huruma. Salini si kwa maneno tu, ila kwa matendo ya huruma. Salini kwa upendo kwa watu wote. Mwanangu amekuza kimaadili upendo kwa njia ya sadaka yake. Kwa hiyo isheni pamoja naye mpate nguvu na matumaini, mpate upendo ulio uhai wa kuongoza kwenye uzima wa milele. Kwa njia ya upendo wa Mungu mimi nami ni pamoja nanyi, na nitawaongoza kwa upendo wa kimama. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Kwa furaha kubwa leo nawaletea Mwanangu Yesu ili Yeye awapeni amani Yake. Wanangu, fungueni mioyo yenu na muwe wafurahivu, ili muweze kuipokea. Mbingu ni pamoja nanyi na zinapambana kwa ajili ya amani mioyoni mwenu, katika jamaa na ulimwenguni na ninyi, wanangu, msaidieni kwa sala zenu ili iwe hivyo. Ninawabariki pamoja na Mwanangu Yesu na kuwaomba msikose matumaini, na mtazamo wenu na moyo wenu yaelekee daima mbinguni na uzima wa milele. Hivyo mtafunguliwa kwa Mungu na mipango Yake. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, ninyi mnaojaribu kumtolea Mwanangu kila siku ya maisha yenu, ninyi mnaojaribu kuishi pamoja naye, ninyi mnaosali na kujitolea, ninyi ni matumaini katika ulimwengu huu wenye udhia. Ninyi ni miali ya mwanga wa Mwanangu, Injili iliyo hai, na ninyi ni mitume wangu wapenzi wa upendo. Mwanangu ni pamoja nanyi. Vili vile, lakini, Yeye anawangojea kwa uvumilivu wale wasiomjua. Kwa hiyo ninyi, mitume wa upendo wangu, salini kwa moyo na onyesheni kwa matendo upendo wa Mwanangu. Kwenu ninyi hiyo ni matumaini ya pekee, na njia ya pekee kuelekea uzima wa milele. Mimi, kama Mama, ni hapa pamoja nanyi. Sala zenu mnazoniomba ni kwangu mawaridi ya upendo mazuri kuliko yote, Siwezi kutokuwapo pale ninapohisi harufu ya mawaridi. Kuna matumaini! Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, kama vile katika mahali pengine nilipokuja, vivyo hivyo hapa pia nawaalika kusali. Salini kwa ajili ya wale wasiomjua Mwanangu, kwa ajili ya wale ambao hawajaujua upendo wa Mungu, dhidi ya dhambi, kwa ajili ya waliowekwa wakfu, kwa ajili ya wale ambao Mwanangu aliwaita ili wawe na upendo na roho yenye nguvu, kwa ajili yenu na kwa ajili ya Kanisa. Mwombeni Mwanangu, na upendo mnaohisi kwa ajili ya ukaribu, utawapa nguvu na utawatayarisha kwa matendo mema mtakayofanya kwa Jina lake. Wanangu muwe tayari. Wakati huu ni njia panda ya maisha. Kwa hiyo nawaalika tena kwa imani na matumaini, ninawaonyesha njia ya kushika. Hayo ni maneno ya Injili: Mitume wangu, ulimwengu unahitaji sana mikono yenu iliyoinuliwa mbinguni, kuelekea kwa Mwanangu na kwa Baba wa mbinguni. Ni lazima kuwa na unyenyekevu mwingi na usafi wa moyo. Mumwamini Mwanangu na jueni ya kuwa mnaweza kuwa bora zaidi daima. Moyo wangu wa kimama unatamani kwamba ninyi, mitume wa upendo wangu, muwe sikuzote mianga midogo ya ulimwengu. Mtie nuru pale giza inapotaka kutawala na kwa sala yenu na upendo wenu, muonyeshe sikuzote njia ya kweli, ziokoeni nafsi. Mimi nipo pamoja nanyi. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Leo nataka kuwashukuru kwa uvumilivu wenu na kuwaalika kujifungua kwa sala ya ndani. Wanangu, sala ni moyo wa imani na wa matumaini katika uzima wa milele. Kwa hiyo salini kwa moyo mpaka moyo wenu umwimbie Mungu Mwumbaji aliyewapa maisha kwa shukrani. Wanangu, Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaletea baraka yangu ya amani ya kimama. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, nawashukuru kwa kuitikia miito yangu na kukusanyika karibu nami, Mama yenu wa mbinguni. Najua kwamba mnanifikiri kwa upendo na matumaini. Mimi ninawapendeni nyote kama vile anavyowapendeni Mwanangu ambaye, kwa upendo wake wenye huruma, ananituma nije kwenu, mara nyingi pia. Yeye, aliyekuwa mtu na aliye Mungu, Mmoja na Utatu; Yeye aliyeteswa kwa ajili yenu mwilini na nafsini. Yeye aliyejifanya Mkate ailishe nafsi zenu na hivyo kuziokoa. Wanangu, nawafundisha jinsi ya kustahili upendo wake, kumwelekeza mawazo yenu, kumwishi Mwanangu. Mitume wa upendo wangu, ninawafunika kwa joho langu kwa sababu, kama Mama yenu, nataka kuwalinda. Nawasihi: mwuombee ulimwengu wote: moyo wangu unateswa. Dhambi zinaongezeka, ni nyingi mno. Lakini kwa msaada wenu – mlio wanyenyekevu, wanyofu, wenye upendo, watawa na watakatifu – moyo wangu utashinda. Mpendeni Mwanangu kupita wote na ulimwengu wote kwa njia yake. Msisahau kabisa ya kuwa kila ndugu yenu ana ndani yake kitu cha thamani: nafsi. Kwa hiyo, wanangu, pendeni wale wote wasiomjua Mwanangu ili kwa njia ya maombi na upendo utokao katika maombi, wawe wema zaidi. Ili wema uweze kushinda ndani yao. Ili nafsi zao ziweze kuokoka na kupata uzima wa milele. Enyi mitume wangu, wanangu. Mwanangu aliwaambieni mpendane. Hiyo iandikwe mioyoni mwenu na kwa kusali jaribuni kuishi upendo huu. Nawashukuru.
1 2 3 Next>>