Web address of the page: https://www.medjugorje.ws/sw/messages/highlight?find=yeye 
www.medjugorje.ws » Our Lady of Medjugorje Messages » Our Lady of Medjugorje Messages containing 'yeye'

Our Lady of Medjugorje Messages containing 'yeye'

Total found: 72
Wanangu wapendwa, katika wakati huu wa wasiwasi nawaalikeni tena kutembea nyuma ya Mwanangu, na kumfuata. Nayajua maumivu, mateso na taabu zenu, lakini katika Mwanangu mtapumzika, ndani yake mtapata amani na wokovu. Wanangu, msisahau ya kuwa Mwanangu amewakomboa ninyi kwa msalaba wake akawajalieni kuwa tena wana wa Mungu na kuwafundisha kumwita tena "Baba" yenu, Mungu aliye mbinguni. Ili muwe wapenzi wa Mungu Baba, basi muwe na mapendo na msamaha, kwa kuwa Baba yenu ni upendo na msamaha. Salini na fungeni, kwa maana hii ndiyo njia ya kujua na kumfahamu Baba aliye mbinguni. Mtakapomjua huyo Baba, mtafahamu ya kuwa Yeye tu ni muhimu kwenu (Maria Mtakatifu amenena hayo kwa nguvu na amkazo sana). Mimi, nikiwa Mama, nataka wanangu wawe watu wenye umoja ambamo Neno la Mungu husikilizwa na kutekelezwa. Kwa hiyo, enyi wanangu, mfuateni Mwanangu, muwe kitu kimoja naye, muwe wana wa Mungu. Pendeni wachungaji wenu kama vile Mwanangu alivyowapenda alipowaita kuwatumikia ninyi. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa! Leo pia Yeye Aliye Juu anijalia neema ya kuwa pamoja nanyi na kuwaongoza mpate kutubu. Siku hata siku Mimi napanda mbegu na kuwaalika kutubu ili muweze kuwa sala, amani, upendo na ngano ambayo ikifa huzaa mara mia. Sipendi, wanangu wapendwa, mpate kujuta kwa yote mliyoweza kufanya wala hamkufanya. Kwa hiyo, enyi wanangu, tena kwa moyo wa furaha semeni: “ Nataka kuwa ishara kwa watu wengine”. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, nawapendeni, ninyi nyote, watoto wangu nyote, muwe wote moyoni mwangu, ninyi nyote mmepata upendo wangu wa kimama na ninatamani kuwaongoza nyote ili mjue furaha ya Mungu. Kwa hiyo nawaalikeni: nahitaji mitume wanyenyekevu ambao, kwa moyo mkunjufu, wanapokea Neno la Mungu na ambao wako tayari kuwasaidia watu wengine ili, kwa njia ya Neno la Mungu, waelewe maana ya maisha yao. Ili muweze kufanya hayo, wanangu, yawapasa, kwa njia ya kusali na kufunga, kusikiliza kwa moyo mkunjufu na kujifunza kujidhili au kujinyenyekesha. Yawapasa kujifunza kukataa yote yanayowatenganisha na Neno la Mungu na kutamani tu yanayowakaribisha. Msiogope, mimi nipo hapa. Ninyi si peke yenu. Namwomba Roho Mtakatifu ili awafanye wapya, ili awaimarishe. Namwomba Roho Mtakatifu, ili mkisaidia wengine, muweze kujiponya nyinyi wenyewe. Naomba ili, kwa njia yake, muwe wana wa Mungu na mitume wangu.
Kisha kwa mahangaiko makubwa Bikira Maria alisema:
Kwa ajili ya Yesu, kwa ajili ya mwanangu, pendeni wale ambao Yeye aliwaita mkitamani baraka ya mikono ile ambayo Yeye tu ameyaweka wakfu. Msiyaruhusu maovu yatawale. Nawaalikeni tena: ni kwa njia ya wachungaji wangu tu moyo wangu utashinda. Msiyaruhusu maovu yawatenganisheni na wachungaji wenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Leo nawaalikeni mjifungulie kwa sali. Sala itasababisha miujiza ndani yenu na kwa njia yenu. Kwa hiyo, enyi wanangu, kwa moyo mkunjufu mtafuteni Yeye Aliye Juu ili awapeni nguvu ya kuwa wana wa Mungu, na yule Shetani asiwatikiseni kama matawi yatikiswavyo na upepo. Kateni shauri tena, wanangu, kwa Mungu na tafuteni tu mapenzi yake, hapo mtapata furaha na amani. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, kwa moyo wa kimama nawaalikeni tena kupenda, kusali bila kukata tamaa kwa zawadi ya upendo, kumpenda Baba wa Mbinguni zaidi ya yote. Mtakapompenda Yeye, mtajipenda wenyewe na jirani zenu. Mambo hayo hayawezi kutengana. Baba wa Mbinguni yumo katika kila mtu, hupenda kila mtu na kumwita kila mtu kwa jina lake. Kwa hiyo, wanangu, kwa njia ya kusali sikilizeni atakalo Baba wa Mbinguni. Ongeeni na Yeye. Muwe na uhusiano wa binafsi pamoja na Baba, atakayeufanya mkubwa zaidi uhusiano wake nanyi, jumuhiya ya wanangu, mitume wangu. Kama Mama napenda kwamba, kwa njia ya upendo kumwelekea Baba wa Mbinguni, inukeni juu ya ubatili wa malimwengu na muwasaidie wengine kujua na kumjongea polepole Baba wa Mbinguni. Wanangu, salini, salini, salini kwa zawadi ya upendo, kwa sababu upendo ndiye Mwanangu. Muwaombee wachungaji wenu, ili wawapende ninyi siku zote, kama vile Mwanangu alivyowapenda ninyi na kuonyesha akitoa maisha yake kwa wokovu wenu. Nawashukuruni.
Wanangu wapendwa! Leo nawaalikeni nyote kusali. Fungueni kwa kina mlango wa mioyo yenu, enyi wanangu, kwa sala, sala ya moyo na hivyo Yeye Aliye Juu ataweza kufanya kazi katika uhuru wenu na kuanzisha uongofu wenu. Hivyo imani yenu itakuwa imara kiasi cha kuweza kusema kwa moyo wenu wote: "Mungu wangu na yote yangu". Halafu mtaweza kuelewa, wanangu, ya kuwa duniani hapa yote hupita. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Ninawaletea Mfalme wa amani ili Yeye awapatie amani Yake. Ninyi, wanangu, salini, salini, salini. Matunda ya sala yatajionyesha kwenye nyuso za watu waliojitoa kwa Mungu na Ufalme wake. Mimi pamoja na mwanangu Yesu tunawabariki nyote kwa baraka ya amani. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Ili mpate kuwa mitume wangu na kuweza kusaidia wale walioko katika giza, ili waweze kuujua mwanga wa upendo wa Mwanangu, mnapaswa kuwa na moyo safi na mnyenyekevu. Hamwezi kusaidia ili Mwanangu azaliwe na kutawala mioyoni mwa wale wasiomjua, iwapo Yeye hatawali moyoni mwenu. Mimi nipo pamoja nanyi, natembea pamoja nanyi kama mama, nabisha hodi katika moyo wenu, usioweza kufunguka bila ya kuwa mnyenyekevu. Mimi nasali, lakini salini nanyi pia, wanangu wapendwa, ili muweze kumfungulia Mwanangu moyo wenu safi na mnyenyekevu na hivyo kuweza kupokea vipaji nilivyowaahidi. Hapo ndipo mtakapoongozwa kwa upendo na nguvu za Mwanangu, hapo ndipo mtakuwa mitume wangu, ambao wanaweza kueneza kwa walio karibu yao matunda ya upendo wa Mungu. Kutokana na ninyi na kwa njia yenu Mwanangu atafanya kazi, maana mtakuwa na Yeye kitu kimoja. Moyo wangu wa kimama unatamani muungano wa wanangu wote, kwa njia ya Mwanangu. Kwa upendo mkuu nawabariki na kuwaombea wateule wa Mwanangu, wachungaji wenu, Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Yeye Aliye Juu ananipa neema ya kuweza kuwa tena pamoja nanyi na kuwaongoza katika sala kuelekea njia ya amani. Mioyo yenu na roho zenu zina kiu ya amani na upendo, ya Mungu na ya furaha yake. Kwa hiyo, wanangu, salini, salini, salini na katika sala mtapata hekima ya kuishi. Nawabarikieni na kukuombeeni mbele ya Mwanangu Yesu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Mimi Mama yenu, ninyi mliokusanyika hapa na Mama wa ulimwengu mzima, nawabariki kwa baraka ya kimama na kuwaalika kuanza safari katika njia ya unyenyekevu. Njia hiyo inawaongoza katika ujuzi wa upendo wa Mwanangu. Mwanangu ni Mwenye uwezo. Yeye yumo katika kila kitu. Kama ninyi, wanangu, hamelewi hayo, basi mtambue kuwa katika roho yenu giza na upofu zinatawala. Unyenyekevu tu huweza kuwaponya. Wanangu, mimi nilikuwa nimeishi daima kwa unyenyekevu, kwa uhodari na kwa matumaini. Nilijua, nilikuwa nimeelewa ya kuwa Mungu yu ndani yetu na sisi ndani ya Mungu. Nawaombeni kuelewa vile vile. Nataka ninyi nyote muwe pamoja nami katika umilele, maana ninyi ni sehemu yangu. Katika njia yenu nitawasaidia. Upendo wangu utawafunika kama joho na kuwafanya ninyi mitume wa mwanga wangu, wa mwanga wa Mungu. Kwa upendo utokao katika unyenyekevu, mtaleta mwanga palipotawala giza na upofu. Mtaleta Mwanangu, aliye mwanga wa ulimwengu. Mimi ni sikuzote kando ya wachungaji wenu na kusali ili wawe siku zote kwenu mfano wa unyenyekevu. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa! Ninyi hamjui neema ya namna gani mnayoishi katika wakati huu ambapo Yeye Aliye Juu awapeni ishara ili mjifungue na kutubu. Mwelekeeni Mungu na kusali; sala itawale katika mioyo yenu, familia na jamaa zenu ili Roho Mtakatifu awaongoze na kuhimiza kila siku mjifungue kufanya mapenzi ya Mungu na mpango wake kwa kila mmoja wenu. Mimi nipo pamoja nanyi, na nawaombeeni pamoja na malaika na watakatifu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Sababu ya kukaa kwangu pamoja nanyi, utume wangu, ni kuwasaidieni ili wema ushinde, hata kama kwa sasa haya yaonekana ni kitu kigumu sana. Najua kwamba mambo mengi hamyaelewi, kama vile sikuelewa mengi ambayo Mwanangu alinifundisha akiwa alipokua pamoja nami, lakini mimi nilimsadiki na kumfuata. Haya nawaombea ninyi pia, kunisadiki na kunifuata, lakini, wanangu, kunifuata maana yake ni kupenda mwanangu kuliko wote, kumpenda katika kila mtu pasipo ubaguzi. Ili kuweza kufanya haya yote nawaalikeni tena kujinyima, kusali na kufunga. Nawaalikeni ili maisha ya roho yenu yawe ni Ekaristi. Nawaalikeni muwe mitume wangu wa mwanga, ambao wataueneza upendo na rehema ulimwenguni. Wanangu, maisha yenu ni mpigo tu wa moyo mbele ya uzima wa milele. Mtakapokuwa mbele ya Mwanangu, Yeye ataona katika mioyo yenu kiasi cha upendo mliokuwa nao. Ili kuweza kueneza kwa njia ya haki upendo nitamwomba Mwanangu kusudi kwa njia ya upendo awapeni umoja kati yenu na umoja kati yenu na wachungaji wenu. Mwanangu daima anajitoa upya kwa njia yao na anafanya mioyo yenu mipya. Msisahau hilo. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa, mimi, Mama yenu, naja tena katikati yenu kwa upendo usio na mwisho, kutoka upendo usio na kipimo wa Baba wa Mbinguni asiye na mwisho. Na, nikitazama mioyoni mwenu, naona ya kuwa wengi wenu wanipokea kama Mama na, kwa moyo thabiti na safi, wataka kuwa mitume wangu. Lakini Mimi ni Mama pia wa ninyi ambao hamnipokei na, katika ugumu wa moyo wenu, hamtaki kujua upendo wa Mwanangu. Hamjui jinsi moyo wangu ulivyoteseka na jinsi nilivyowaombeeni Mwanangu. Namwomba aponye roho yenu, kwa maana najua Yeye ana uwezo wa kuwaponya. Namwomba awaangaze kwa mwujiza wa mwanga wa Roho Mtakatifu, ili mwache kumsaliti, kumtukana na kumwumiza siku zote kwa kuendelea. Nasali kwa Moyo wote ili muweze kuelewa ya kuwa Mwanangu tu ni wokovu na mwanga wa ulimwengu. Nanyi, wanangu, mitume wangu wapenzi, mbebeni daima Mwanangu katika moyo na fikira zenu. Hivyo ninyi mtakuwa mnabeba Upendo. Wale wote wasiomjua watamtambua katika upendo wenu. Mimi nipo sikuzote karibu yenu. Nipo hasa karibu na wachungaji wenu, kwa sababu Mwanangu aliwaita kuwaongozeni katika njia kuelekea milele. Nawashukuru, mitume wangu, kwa sadaka na upendo wenu!
Wanangu wapendwa, kwa upendo wa kimama nawaombeni: pendaneni! mioyoni mwenu muwe kama Mwanangu alitaka tangu awali: kwanza kabisa kumpenda Baba wa Mbinguni na kuwa na upendo kwa jirani yenu, kuliko yote yaliyopo hapa duniani. Wanangu wapendwa, hamtambui dalili za nyakati hizi? Hamtambui ya kuwa yote yanayotokea kando kando yenu, hutokea kwa sababu hakuna upendo? Fahamuni kwamba wokovu hupatikana katika thamani za kweli, pokeeni uweza wa Baba wa Mbinguni, mpendeni na kumheshimu. Fuateni njia ya Mwanangu. Ninyi, wanangu, mitume wangu wapenzi, mnakusanyika siku zote daima kunizunguka maana mna kiu, mna kiu ya amani, ya upendo na ya furaha. Kateni kiu yenu katika mikono yangu! Mikono yangu yawatolea Mwanangu, aliye chemchemi ya maji safi. Yeye atafufua imani yenu na kusafisha mioyo yenu, kwa sababu Mwanangu hupenda kwa moyo safi na mioyo iliyo safi humpenda Mwanangu. Mioyo safi tu ndiyo minyenyekevu na yenye imani thabiti. Wanangu, nawaombeni ya kuwa na mioyo ya namna hii! Mwanangu aliniambia ya kuwa Mimi ni Mama wa ulimwengu wote: nawaombeni ninyi, mnaonipokea kama Mama, ili kwa maisha yenu, sala na sadaka nisaidieni ili wanangu wote wanipokee kama Mama, niweze kuwaongoza kwenye chemchemi ya maji safi. Nawashukuru! Wanangu wapenzi, wachungaji wenu wanapowatolea mwili wa Mwanangu, mshukuruni Mwanangu daima moyoni mwenu kwa sadaka yake na kwa wachungaji anayewajalia siku zote.
Wanangu wapendwa, zingatieni akilini, kwa maana nawaambia: upendo utashinda! Najua ya kuwa wengi wenu wanapoteza matumaini kwa kuwa wanaona wamezungukwa na mateso, maumivu, husuda na wivu, hata hivyo mimi ni Mama yenu. Mimi nipo katika Ufalme, lakini hata hapa nipo pamoja nanyi. Mwanangu ananituma tena ili niwasaidieni, kwa hiyo msipoteze matumaini ila nifuateni, kwa maana ushindi wa Moyo wangu ni kwa jina la Mungu. Mwanangu mpendwa anawafikiria, kama alivyofanya siku zote: mwaminini na mwishi kama Yeye! Yeye ni uzima wa ulimwengu. Wanangu, kumwishi Mwanangu maana yake ni kuishi Injili. Si kitu rahisi. Ni jambo linalodai upendo, rehema na sadaka. Hayo huwatakasa na kufungua Ufalme: Sala nyofu, isiyo maneno bali itokayo moyoni, itawasaidieni. Vivyo hivyo kufunga, maana hayo huleta ongezeko la upendo, rehema na sadaka. Kwa hiyo msipoteze matumaini, ila nifuateni. Nawaomba tena msali kwa ajili ya wachungaji wenu, ili wamtazame daima Mwanangu, aliyekuwa Mchungaji wa kwanza wa ulimwengu, na ambaye familia yake ilikuwa ulimwengu wote. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa, ninyi ni nguvu yangu. Ninyi, mitume wangu, ambao, kwa upendo wenu, unyenyekevu na sala ya kimya kimya, mnamwezesha Mwanangu ajulikane. Ninyi mnaishi ndani yangu. Ninyi mnanibeba mioyoni mwenu. Ninyi mnajua ya kuwa mna Mama awapendaye na aliyekuja kuwaletea upendo. Nawatazama katika Baba wa Mbinguni, natazama fikira zenu, maumivu yenu, mateso yenu na kuyaleta kwa Mwanangu. Msiogope! Msipoteze matumaini, maana Mwanangu humsikiliza Mama yake. Yeye hupenda tangu alipozaliwa, na ndio furaha yangu ya kuwa wanangu wote wajue upendo huo; na wote wale ambao, kwa sababu ya maumivu yao na kutoelewa kwao, walimwacha waweze kurudi kwake, na wote wao wasiomjua wamjue. Kwa sababu hiyo ninyi hapa ni mitume wangu, nami pia pamoja nanyi kama Mama yenu. Salini ili kuwa imara katika imani, maana upendo na rehema hutoka katika imani imara. Kwa njia ya upendo na rehema mtawasaidia wale wote wasiofahamu ya kuwa wanachagua giza badala ya nuru. Salini kwa ajili ya wachungaji wenu, maana wao ni nguvu ya Kanisa ambayo Mwanangu aliwaachieni. Kwa njia ya Mwanangu wao ni wachungaji wa roho. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Hata leo pia Yeye Aliye Juu ameniruhusu kuwa pamoja nanyi na kuwaongoza katika njia ya uwongofu. Mioyo mingi imejifunga kwa neema wala haitaki kusikiliza mwaliko wangu. Ninyi wanangu salini na pambaneni na kishawishi na mipango yote ya uovu ambayo anayowapatia shetani kwa njia ya mambo ya kisasa. Muwe hodari katika kusali na mkishika msalaba mikononi salini ili maovu yasiwatumie wala kuwashinda. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaombea. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, fungueni mioyo yenu mkajaribu kuhisi jinsi ninavyowapenda na kutaka mpendeni Mwanangu. Nataka mpende zaidi kwa kuwa haiwezekani kumjua pasipo kumpenda, maana Yeye ndiye upendo. Wanangu, mimi nawajueni: najua maumivu yenu na mateso yenu maana niliyaishi. Nafurahi pamoja nanyi kwa furaha zenu. Nalia machozi pamoja nanyi katika maumivu yenu. Sitawaacheni kamwe. Nitaongea nanyi daima kwa upole wa kimama na, kama mama, nahitaji mioyo yenu ifumbuliwe, ili kwa hekima na unyofu mueneze upendo wa Mwanangu. Nawahitaji ninyi mfumbuliwe na kuwa wepesi kupokea mema na huruma. Nahitaji muungano wenu na Mwanangu, kwa maana nataka mpate kufanikiwa na kumsaidia kuleta heri kwa wanangu wote. Mitume wangu, nawahitaji, ili muwaonyeshe wote ukweli wa Mungu, ili moyo wangu, ulioteswa na kuteswa hata leo kupita kiasi, uweze kushinda katika upendo. Salini kwa ajili ya utakatifu wa wachungaji wenu, ili katika jina la Mwanangu, waweze kutenda maajabu, maana utakatifu hutenda maajabu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nataka kufanya kazi kwa njia yenu, wanangu, mitume wangu, ili mwishowe niweze kukusanya wanangu wote pale ambapo pameandaliwa tayari kwa ajili ya furaha yenu. Nawaombea, kusudi kwa matendo yenu muweze kugeuza, kwani muda umefika kwa matendo ya kweli, kwa ajili ya Mwanangu. Upendo wangu utafanya kazi ndani mwenu, nitawatumia ninyi. Muwe na imani nami, kwani yote ninayotamani, ninayatamani kwa ajili yenu, wema wa milele, ulioumbwa kwa njia ya Baba wa Mbinguni. Ninyi, wanangu, mitume wangu, muishi maisha ya duniani pamoja na wanangu ambao hawafahamu upendo wa Mwanangu, wale ambao hawaniiti mama. Lakini msiogope kushuhudia ukweli, kwa maana ikiwa ninyi hamtaogopa na kushuhudia ukweli kwa uhodari, ukweli utashinda kimuujiza. Kumbukeni: nguvu iko katika upendo. Wanangu, upendo ndio kutubu, kusamehe, kusali, kujitoa sadaka na rehema, maana mkijua kupenda kwa matendo mtawabadilisha na wengine, mtawezesha mwanga wa Mwanangu uingie katika mioyo yao. Nawashukuru. Muwaombee wachungaji wenu, wao ni mali ya Mwanangu. Yeye aliwaita. Salini ili wawe siku zote na nguvu na uhodari wa kung'aa kwa nuru ya Mwanangu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Hata leo Yeye Aliye Juu ananipa neema ya kuweza kuwapenda na kuwaalika muweze kuongoka. Wanangu, Mungu awe kesho yenu, vita, wasiwasi, huzuni yasiwatawale, ila furaha na amani zitawale mioyoni mwa watu wote, na mjue kuwa pasipo Mungu hamtapata kamwe amani. Kwa hiyo, wanangu, mrudieni Mungu na sala ili mioyo yenu iimbe kwa furaha. Mimi nipo pamoja nanyi na ninawapenda kwa upendo usio na kipimo. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
1 2 3 4 Next>>