Our Lady of Medjugorje Messages containing 'nanyi'

Total found: 131
Wanangu wapendwa! Leo kwa namna ya pekee nawaalikeni msali. Salini, wanangu, ili muweze kutambua ninyi ni akina nani na ni wapi mnayopaswa kwenda. Muwe watangazaji wa Habari Njema na watu wa matumaini. Muwe upendo kwa wale wote wasio na upendo. Wanangu, mtakuwa yote na kuyatimiza yote iwapo tu mkisali na mkiwa tayari kupokea mapenzi ya Mungu, Mungu ambaye anatamani kuwaongoza katika maisha ya uzima wa milele. Mimi nipo pamoja nanyi na siku hata siku ninawaombeeni kwa Mwanangu Yesu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, zingatieni akilini, kwa maana nawaambia: upendo utashinda! Najua ya kuwa wengi wenu wanapoteza matumaini kwa kuwa wanaona wamezungukwa na mateso, maumivu, husuda na wivu, hata hivyo mimi ni Mama yenu. Mimi nipo katika Ufalme, lakini hata hapa nipo pamoja nanyi. Mwanangu ananituma tena ili niwasaidieni, kwa hiyo msipoteze matumaini ila nifuateni, kwa maana ushindi wa Moyo wangu ni kwa jina la Mungu. Mwanangu mpendwa anawafikiria, kama alivyofanya siku zote: mwaminini na mwishi kama Yeye! Yeye ni uzima wa ulimwengu. Wanangu, kumwishi Mwanangu maana yake ni kuishi Injili. Si kitu rahisi. Ni jambo linalodai upendo, rehema na sadaka. Hayo huwatakasa na kufungua Ufalme: Sala nyofu, isiyo maneno bali itokayo moyoni, itawasaidieni. Vivyo hivyo kufunga, maana hayo huleta ongezeko la upendo, rehema na sadaka. Kwa hiyo msipoteze matumaini, ila nifuateni. Nawaomba tena msali kwa ajili ya wachungaji wenu, ili wamtazame daima Mwanangu, aliyekuwa Mchungaji wa kwanza wa ulimwengu, na ambaye familia yake ilikuwa ulimwengu wote. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa! Katika wakati huu wa neema ninawaalika nyote: salini zaidi na muongee kidogo. Katika kusali tafuteni mapenzi ya Mungu na yaishini kadiri ya amri ambazo Mungu anawaalika kuziishi. Mimi nipo pamoja nanyi na kusali pamoja nanyi. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, ninyi ni nguvu yangu. Ninyi, mitume wangu, ambao, kwa upendo wenu, unyenyekevu na sala ya kimya kimya, mnamwezesha Mwanangu ajulikane. Ninyi mnaishi ndani yangu. Ninyi mnanibeba mioyoni mwenu. Ninyi mnajua ya kuwa mna Mama awapendaye na aliyekuja kuwaletea upendo. Nawatazama katika Baba wa Mbinguni, natazama fikira zenu, maumivu yenu, mateso yenu na kuyaleta kwa Mwanangu. Msiogope! Msipoteze matumaini, maana Mwanangu humsikiliza Mama yake. Yeye hupenda tangu alipozaliwa, na ndio furaha yangu ya kuwa wanangu wote wajue upendo huo; na wote wale ambao, kwa sababu ya maumivu yao na kutoelewa kwao, walimwacha waweze kurudi kwake, na wote wao wasiomjua wamjue. Kwa sababu hiyo ninyi hapa ni mitume wangu, nami pia pamoja nanyi kama Mama yenu. Salini ili kuwa imara katika imani, maana upendo na rehema hutoka katika imani imara. Kwa njia ya upendo na rehema mtawasaidia wale wote wasiofahamu ya kuwa wanachagua giza badala ya nuru. Salini kwa ajili ya wachungaji wenu, maana wao ni nguvu ya Kanisa ambayo Mwanangu aliwaachieni. Kwa njia ya Mwanangu wao ni wachungaji wa roho. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Hata leo pia Yeye Aliye Juu ameniruhusu kuwa pamoja nanyi na kuwaongoza katika njia ya uwongofu. Mioyo mingi imejifunga kwa neema wala haitaki kusikiliza mwaliko wangu. Ninyi wanangu salini na pambaneni na kishawishi na mipango yote ya uovu ambayo anayowapatia shetani kwa njia ya mambo ya kisasa. Muwe hodari katika kusali na mkishika msalaba mikononi salini ili maovu yasiwatumie wala kuwashinda. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaombea. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Mimi nipo pamoja nanyi hata leo niwaongozeni kwenye wokovu. Moyo wenu una wasiwasi maana roho yenu ni dhaifu na imechoka kwa mambo yote ya dunia. Ninyi wanangu, ombeni Roho Mtakatifu awageuze na kuwajaza nguvu yake ya imani na tumaini ili muweze kuwa imara katika kupambana kwenu na maovu. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaombea kwenye Mwanangu Yesu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, fungueni mioyo yenu mkajaribu kuhisi jinsi ninavyowapenda na kutaka mpendeni Mwanangu. Nataka mpende zaidi kwa kuwa haiwezekani kumjua pasipo kumpenda, maana Yeye ndiye upendo. Wanangu, mimi nawajueni: najua maumivu yenu na mateso yenu maana niliyaishi. Nafurahi pamoja nanyi kwa furaha zenu. Nalia machozi pamoja nanyi katika maumivu yenu. Sitawaacheni kamwe. Nitaongea nanyi daima kwa upole wa kimama na, kama mama, nahitaji mioyo yenu ifumbuliwe, ili kwa hekima na unyofu mueneze upendo wa Mwanangu. Nawahitaji ninyi mfumbuliwe na kuwa wepesi kupokea mema na huruma. Nahitaji muungano wenu na Mwanangu, kwa maana nataka mpate kufanikiwa na kumsaidia kuleta heri kwa wanangu wote. Mitume wangu, nawahitaji, ili muwaonyeshe wote ukweli wa Mungu, ili moyo wangu, ulioteswa na kuteswa hata leo kupita kiasi, uweze kushinda katika upendo. Salini kwa ajili ya utakatifu wa wachungaji wenu, ili katika jina la Mwanangu, waweze kutenda maajabu, maana utakatifu hutenda maajabu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Hata leo mimi nipo pamoja nanyi na kwa furaha nawaalikeni nyote: salini na aminini nguvu ya sala. Fungueni mioyo yenu, wanangu, ili Mungu awajaze upendo wake, nanyi mtakuwa furaha ya watu wengine. Ushahidi wenu utakuwa na nguvu na lote mfanyalo litaendana na mapenzi ya Mungu. Mimi nipo pamoja nanyi, nikisali kwa ajili yenu na kwa ajili ya wokovu wenu hata mtakapomweka Mungu mahali pa kwanza. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Hata leo Yeye Aliye Juu ananipa neema ya kuweza kuwapenda na kuwaalika muweze kuongoka. Wanangu, Mungu awe kesho yenu, vita, wasiwasi, huzuni yasiwatawale, ila furaha na amani zitawale mioyoni mwa watu wote, na mjue kuwa pasipo Mungu hamtapata kamwe amani. Kwa hiyo, wanangu, mrudieni Mungu na sala ili mioyo yenu iimbe kwa furaha. Mimi nipo pamoja nanyi na ninawapenda kwa upendo usio na kipimo. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, nawaalika kueneza imani katika Mwanangu, imani yenu. Ninyi wanangu, mlioangazwa na Roho Mtakatifu, mitume wangu, itangazeni imani kwa watu wengine, yaani kwa wasiosadiki, wasioijua na wasiotaka kuijua. Kwa sababu hiyo yawapasa kusali sana kwa ajili ya zawadi ya upendo, maana upendo ndio alama maalum ya imani ya kweli, na ninyi mtakuwa mitume wa upendo wangu. Upendo hufanya upya daima maumivu na furaha ya Ekaristi, hufanya upya maumivu ya Mateso ya Mwanangu, aliyewaonyesha upendo usio na kifani; hufanya upya furaha ya tendo la kuwaachia Mwili wake na Damu yake kwa ajili ya kuwalisha na hivyo kuwa kitu kimoja nanyi. Nikiwaangalia kwa wema nahisi upendo pasipo kiasi, ulioniimarisha katika hamu yangu ya kuwaongoza katika imani thabiti. Imani thabiti itawapa furaha na uchangamfu duniani, na mwishowe kuwaunganisha na Mwanangu. Hiyo ndiyo hamu yake. Kwa hiyo mwishi katika Yeye, na katika upendo, isheni katika nuru iliyowaangaza daima katika Ekaristi. Nawaombeni kusali sana kwa wachungaji wenu, kusali ili kupata upendo mkubwa kwa ajili yao, kwa maana Mwanangu aliwapeni ili waweze kuwalisha kwa Mwili wake na kuwafundisha upendo. Kwa hiyo wapendeni ninyi pia! Lakini, wanangu, kumbukeni: upendo maana yake ni kuvumilia na kutoa na kutohukumu kamwe. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, hata leo kwa furaha nipo pamoja nanyi na ninawaalika wote, wanangu, salini, salini, salini, ili muweze kuelewa upendo nilio nao kwenu. Upendo wangu una nguvu kuliko uovu, kwa hiyo wanangu mjongeeni Mungu ili muweze kuonja furaha yangu kwa Mungu. Pasipo Mungu, wanangu, hamtakuwa na wakati ujao, wala tumaini, wala wokovu, kwa hiyo acheni uovu na chagueni wema: Mimi nipo pamoja nanyi na pamoja nanyi namwomba Mungu kwa mahitaji yenu yote. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, mimi, kama Mama apendaye wanawe, natambua jinsi ulivyo mgumu muda huu mnaouishi. Naona mateso yenu, lakini jueni kwamba hamko peke yenu: Mwanangu yu pamoja nanyi! Yeye yupo popote, asiyeonekana, lakini mtaweza kumwona ikiwa mtamwishi. Yeye ndiye nuru inayoangaza roho yenu na kuleta amani. Yeye ndiye Kanisa, mnalopaswa kulipenda, kuliombea na kulilinda daima: si kwa maneno tu, bali kwa matendo ya upendo. Wanangu, fanyeni yote ili Mwanangu ajulikane kwa watu wote, na aweze kupendwa, kwa maana ukweli ni katika Mwanangu, aliyezaliwa na Mungu, Mwana wa Mungu. Msipoteze muda kwa kufikiri mno; mtajitenganisha na ukweli. Pokeeni Neno lake kwa moyo mnyofu na kuliishi. Mkiishi Neno lake, mtasali. Mkiishi Neno lake, mtapenda kwa upendo wenye huruma, na mtapendana. Kwa kadiri mtakavyokuwa na upendo hivyo ndivyo mtakavyokuwa mbali na kifo. Kwa wale watakaoishi na kulipenda Neno la Mwanangu, kifo kitakuwa uhai kwao. Nawashukuru! Salini kwa ajili ya kuweza kuona Mwanangu katika wachungaji wenu. Salini kwa ajili ya kuweza kumkumbatia katika wao.
Wanangu wapendwa, hata leo ninawaalika: muwe sala. Sala iwe mabawa kwa ajili ya mkutano kati yenu na Mungu. Ulimwengu upo katika wakati wa kujaribiwa, kwa maana umemsahau na kumwacha Mungu. Kwa hiyo wanangu, muwe wale wanaomtafuta na kupenda Mungu kuliko yote. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaongoza kwa Mwanangu, lakini ninyi hamna budi kunena "NDIYO" yenu katika uhuru wa wana wa Mungu. Nawaombeeni na kuwapenda, wanangu, kwa upendo usio na mwisho. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, wapendwa mitume wangu wa upendo, waletaji wangu wa ukweli, ninawaalika tena na ninawakusanya karibu nami ili mnisaidie, ili muwasaidie wanangu wote wenye kiu ya upendo na ukweli, wenye kiu ya Mwanangu. Mimi ndimi neema ya Baba wa Mbinguni iliyotumwa kuwasaidieni kuishi neno la Mwanangu. Pendaneni. Nimeyaishi maisha yenu duniani. Najua kwamba si kitu rahisi kila mara lakini, mkipendana, mtasali kwa moyo, mtafikia vilele vya maisha ya roho, na njia ya kwenda mbinguni itafunguliwa mbele yenu. Pale nawangojea mimi, Mama yenu, kwa maana mimi nipo pale. Muwe waaminifu kwa Mwanangu na muwafundishe wengine uaminifu. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwasaidia. Nitawafundisha imani, ili muweze kuwafikishia wengine kwa njia sahihi. Nitawafundisha ukweli, ili muweze kuufahamu. Nitawafundisha upendo, ili mjue upendo wa kweli ni kitu gani. Wanangu, Mwanangu atafanya yote ili aongee kwa njia ya maneno na matendo yenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, hata leo ninamwomba Roho Mtakatifu ili ajaze mioyo yenu kwa imani thabiti. Sala na imani zitajaza mioyo yenu kwa upendo na furaha, nanyi mtakuwa ishara kwa wale walio mbali na Mungu. Wanangu, mpeane moyo wenyewe kwa wenyewe ili kufanya sala ya moyo, ili sala iweze kujaza maisha yenu na ninyi, wanangu, kila siku muwe mashahidi wa utumishi: kwa Mungu katika kuabudu na kwa majirani zenu katika mahitaji yao. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaombea ninyi nyote. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, nipo hapa katikati yenu kuwatieni moyo, kuwajaza kwa upendo wangu, kuwaalika tena kuwa mashahidi wa upendo wa Mwanangu. Wanangu wengi hawana tumaini, hawana amani, hawana upendo. Wao wanatafuta Mwanangu lakini hawajui jinsi wala wapi ya kumpata. Mwanangu awafungulia mikono Yake, nanyi wasaidieni ili waje mikononi Mwake. Wanangu, kwa hiyo ni lazima msali kwa upendo, lazima msali sana, sana, ili kupata upendo zaidi na zaidi, kwa maana upendo hushinda mauti na hudumisha maisha. Watume wa upendo wangu, wanangu wenye moyo mnyofu na safi, jiungeni zaidi na zaidi katika kusali. Mnatengana sana! Jipeni moyo katika kukua kiroho, kama vile Mimi ninawapeni moyo. Ninawaangalia na nipo karibu nanyi kila mnaponifikiria. Waombeeni wachungaji wenu, wale walioacha yote kwa ajili ya Mwanangu. Wapendeni na waombeeni, Baba wa Mbinguni husikiliza sala zenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nataka kuongea nanyi tena juu ya upendo. Nimewakusanya kunizunguka kwa Jina la Mwanangu, kwa kadiri ya mapenzi yake. Nataka imani yenu iwe thabiti na iwe inatokana na mapendo, kwa maana wanangu wale wanaoelewa upendo wa Mwanangu na kuufuata, huishi katika mapendo na matumaini. Wamejua upendo wa Mungu. Kwa hiyo, wanangu, salini, salini ili muweze kupenda zaidi muwezavyo na kutenda matendo ya upendo. Kwa maana, imani peke yake, pasipo upendo wala matendo ya upendo, si neno ninaloomba kwenu. Wanangu, ule ni utovu wa imani, ni kujisifu mwenyewe. Mwanangu hutaka imani na matendo, upendo na wema. Mimi ninasali, lakini nawaombeni pia kusali na kuishi upendo, kwa maana nataka ya kuwa Mwanangu, atakapoona mioyo ya wanangu wote, aweze kuona ndani yake upendo na wema, sio chukio na ubaridi. Wanangu, mitume ya upendo wangu, msipoteze tumaini, msikate tamaa: ninyi mnaweza kufanya! Mimi ninawapeni moyo na kuwabariki, maana yote yaliyopo duniani hapa - ambayo kwa bahati mbaya wanangu wengi huweka mahali pa kwanza - yatatoweka na upendo na matendo ya upendo tu zitabaki, nazo zitawafungulia malango ya Ufalme wa Mbinguni. Nitawangojea karibu na malango hayo, karibu na malango hayo nataka kuwangojea na kuwakumbatia wanangu wote. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, leo ninawaalika nyote: salini kwa ajili ya nia zangu. Amani ipo hatarini kwa hiyo wanangu, salini na muwe waletaji wa amani na matumani katika ulimwengu huu wa wasiwasi ambamo shetani anashambulia na kuleta majaribu ya kila aina. Wanangu muwe thabiti katika sala na imara katika imani. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaombea ninyi nyote mbele ya Mwanangu, Yesu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, mimi ni sikuzote pamoja nanyi, kwa maana Mwanangu alinikabidhi ninyi. Nanyi, wanangu, mnanihitaji mimi, mnitafute, mnijie na mfurahishe Moyo wangu wa kimama. Mimi ninawapenda na nitawapenda ninyi mnaoteseka na kutolea mateso yenu kwa ajili ya Mwanangu na kwa ajili yangu. Upendo wangu hutafuta upendo wa wanangu wote na wanangu wote hutafuta upendo wangu. Kwa njia ya upendo Yesu hutafuta ushirika kati ya Mbingu na dunia, kati ya Baba wa mbinguni na ninyi, wanangu, Kanisa lake. Kwa hiyo lazima kusali sana, kusali na kulipenda Kanisa ambalo ninyi ni wake. Sasa Kanisa linateseka na kuhitaji mitume ambao, wakipenda ushirika, wanaposhuhudia na kutoa, waonyeshe njia za Mungu. Kanisa linahitaji mitume ambao, wakiishi Ekaristi kwa moyo, watende matendo makuu. Kanisa linawahitaji ninyi, mitume wangu wa upendo. Wanangu, Kanisa limeteswa na kusalitiwa tangu siku zake za awali, lakini linazidi kukua siku hata siku. Kanisa halitaharibiki, kwa maana Mwanangu alilipa moyo: Ekaristi. Nuru ya ufufuo wake imeng’aa na itang’aa juu yake. Kwa hiyo msiogope! Waombeeni wachungaji wenu, ili wawe na nguvu na upendo kwa kuwa madaraja ya wokovu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, miaka hii yote ambapo Mungu ananijalia kuwepo pamoja nanyi ni ishara ya upendo mwingi sana wa Mungu kwa kila mmoja wenu na ishara ya jinsi alivyowapenda. Wanangu, Yeye Aliye Juu amewapeni neema nyingi na anataka kuwapa neema nyingi zaidi. Lakini, wanangu, mioyo yenu imefungwa, inaishi katika hofu na hayaruhusu upendo wa Yesu na amani yake yapate nafasi katika mioyo yenu na kutawala maisha yenu. Kuishi pasipo Mungu ni kuishi gizani wala kutoujua kamwe upendo wa Baba na ulinzi wake kwa kila mmoja wenu. Kwa hiyo wanangu, leo hasa mwombeni Yesu ili tangu leo maisha yenu yapate kuzaliwa upya katika Mungu, na maisha yenu iwe nuru itokayo kwenu. Namna hii mtakuwa mashahidi wa uwepo wa Mungu ulimwenguni hasa kwa kila mtu aishiye gizani. Wanangu, nawapenda na kuwaombeeni kila siku kwake Yeye Aliye Juu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
   




To compare Medjugorje messages with another language versions choose

For God to live in your hearts, you must love.

`