Our Lady of Medjugorje Messages containing 'tamaa'

Total found: 7
Wanangu wapendwa, nawaalikeni tena kupenda na kutohukumu. Mwanangu, kwa mapenzi ya Baba aliye mbinguni, alikuwapo pamoja nanyi ili awaonyesheni njia ya wokovu, awaokoeni si awahukumuni. Na ikiwa mnataka kumfuata Mwanangu, msihukumu na mpende, kama vile Baba aliye mbinguni anavyowapenda ninyi. Hata wakati mnapoteseka sana, au mnapojikwaa chini ya msalaba, msikate tamaa, msihukumu, bali kumbukeni kwamba mnapendwa, na msifuni Baba aliye mbinguni kwa upendo wake. Wanangu, msiiache njia ninayowaongozeni. Msikimbie kwenye maangamizi. Kusali na kufunga itawapa nguvu zaidi ili mweze kuishi kama vile baba wa Mbinguni atakavyo; ili muwe mitume wangu wa imani na upendo; ili maisha yenu iwe na baraka ya wale mnaowaona; ili muwe kitu kimoja na baba aliye mbinguni na Mwanangu. Wanangu, huu ni ukweli wa pekee, ukweli uletao wongofu wenu na kisha wongofu wa wengine wote wasiojua maana ya neno kupenda. Wanangu, Mwanangu aliwapeni wachungaji: muwalinde, na muwaombee. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa, kwa moyo wa kimama nawaalikeni tena kupenda, kusali bila kukata tamaa kwa zawadi ya upendo, kumpenda Baba wa Mbinguni zaidi ya yote. Mtakapompenda Yeye, mtajipenda wenyewe na jirani zenu. Mambo hayo hayawezi kutengana. Baba wa Mbinguni yumo katika kila mtu, hupenda kila mtu na kumwita kila mtu kwa jina lake. Kwa hiyo, wanangu, kwa njia ya kusali sikilizeni atakalo Baba wa Mbinguni. Ongeeni na Yeye. Muwe na uhusiano wa binafsi pamoja na Baba, atakayeufanya mkubwa zaidi uhusiano wake nanyi, jumuhiya ya wanangu, mitume wangu. Kama Mama napenda kwamba, kwa njia ya upendo kumwelekea Baba wa Mbinguni, inukeni juu ya ubatili wa malimwengu na muwasaidie wengine kujua na kumjongea polepole Baba wa Mbinguni. Wanangu, salini, salini, salini kwa zawadi ya upendo, kwa sababu upendo ndiye Mwanangu. Muwaombee wachungaji wenu, ili wawapende ninyi siku zote, kama vile Mwanangu alivyowapenda ninyi na kuonyesha akitoa maisha yake kwa wokovu wenu. Nawashukuruni.
Wanangu wapendwa, nipo hapa katikati yenu. Ninawatazama, ninawapa tabasamu na kuwapenda kama mama peke yake awezavyo kufanya. Kwa neema ya Roho Mtakatifu ajaye kwa njia ya usafi wangu, ninaona mioyo yenu na kuitolea kwa Mwanangu. Tangu muda mrefu nawaombeni muwe mitume wangu, na kusali kwa ajili ya wale wasioujua upendo wa Mungu. Naomba sala inayotokana na upendo, sala itoayo matunda na sadaka. Msipotee muda kutaka kuelewa kama mnastahili kuwa mitume wangu, Baba aliye Mbinguni atahukumu wote, lakini ninyi mpendeni na msikilizeni. Najua ya kuwa mambo hayo yote yanawafadhaisha, hata ujio wangu katikati yenu, lakini upokeeni kwa furaha na salini ili muelewe kwamba mnastahili kufanya kazi kwa ajili ya ufalme wa mbingu. Upendo wangu ni juu yenu. Salini ili upendo wangu udumu ndani ya kila moyo, kwa maana upendo huo unaosamehe ujitolea bila kukata tamaa. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nataka kuongea nanyi tena juu ya upendo. Nimewakusanya kunizunguka kwa Jina la Mwanangu, kwa kadiri ya mapenzi yake. Nataka imani yenu iwe thabiti na iwe inatokana na mapendo, kwa maana wanangu wale wanaoelewa upendo wa Mwanangu na kuufuata, huishi katika mapendo na matumaini. Wamejua upendo wa Mungu. Kwa hiyo, wanangu, salini, salini ili muweze kupenda zaidi muwezavyo na kutenda matendo ya upendo. Kwa maana, imani peke yake, pasipo upendo wala matendo ya upendo, si neno ninaloomba kwenu. Wanangu, ule ni utovu wa imani, ni kujisifu mwenyewe. Mwanangu hutaka imani na matendo, upendo na wema. Mimi ninasali, lakini nawaombeni pia kusali na kuishi upendo, kwa maana nataka ya kuwa Mwanangu, atakapoona mioyo ya wanangu wote, aweze kuona ndani yake upendo na wema, sio chukio na ubaridi. Wanangu, mitume ya upendo wangu, msipoteze tumaini, msikate tamaa: ninyi mnaweza kufanya! Mimi ninawapeni moyo na kuwabariki, maana yote yaliyopo duniani hapa - ambayo kwa bahati mbaya wanangu wengi huweka mahali pa kwanza - yatatoweka na upendo na matendo ya upendo tu zitabaki, nazo zitawafungulia malango ya Ufalme wa Mbinguni. Nitawangojea karibu na malango hayo, karibu na malango hayo nataka kuwangojea na kuwakumbatia wanangu wote. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nikiwatazama hapa mmekusanyika kunizunguka, Mama yenu, ninaona nafsi safi nyingi. Ninawaona wanangu wengi wanaotafuta upendo na faraja lakini hakuna mtu anayewapa. Ninawaona hata wale wanaotenda mabaya maana hawana mifano myema, maana hawajamjua mwanangu. Mwanangu anawatuma ninyi kwangu, Mama, sawa kwa wote, niwafundisheni kupenda, ili muelewe ya kuwa ninyi ni ndugu. Ninatamani kuwasaidia. Mitume wa upendo wangu, kwa mwanangu yamtosha tamaa hai ya imani na upendo na atayakubali, lakini mnapaswa kustahili, kuwa na tamaa na mioyo wazi, Mwanangu huingia katika mioyo wazi. Mimi kama Mama ninatamani kwamba mjue Mwanangu katika kweli: Mungu aliyezaliwa na Mungu, kwamba mjue ukuu wa Upendo wake, ambao mnahitaji. Yeye amezichukua juu yake dhambi zenu, ameupata Ukombozi wenu, na badala yake anaomba mpendane ninyi kwa ninyi. Mwanangu ni upendo, Yeye anawapenda watu wote bila tofauti, watu wote wa nchi zote, wa mataifa yote. Ikiwa ninyi, wanangu, mngeishi upendo wa Mwanangu, ufalme wake ungekwisha kuwa duniani. Kwa hiyo, Mitume wa upendo wangu, salini, salini ili Mwanangu na upendo wake wawe ndani yenu nanyi muweze kuwa mfano wa upendo na muweze kuwasaidia wote wale ambao hawajamjua Mwanangu. Msisahau kamwe kwamba Mwanangu, mmoja na utatu, anawapendeni. Pendeni na wombeeni wachungaji wenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, Baba wa Mbinguni amenifanyia makuu, jinsi anavyowafanyia wale wote wanaompenda sana na kwa wema na uaminifu na wanaomtumikia kwa ibada. Wanangu, Baba wa Mbinguni anawapenda na kwa ajili ya upendo wake mimi nipo hapa pamoja nanyi. Ninasema nanyi: kwa nini hamtaki kuona ishara? Pamoja naye yote ni rahisi zaidi: hata mateso, tunayoishi pamoja naye, ni mepesi zaidi, maana kuna imani. Imani husaidia mateso, na maumivu pasipo imani huongoza katika kukata tamaa. Mateso tunayoyaishi na kuyatolea kwa Mungu, huinua mtu. Je, Mwanangu hakuukomboa ulimwengu kwa njia ya mateso yake makali? Mimi, kama mama yake, katika maumivu na mateso nilikaa pamoja naye, kama vile ninavyokaa pamoja nanyi. Wanangu, mimi nipo pamoja nanyi katika maisha: katika maumivu na mateso, katika furaha na upendo. Kwa hiyo muwe na matumaini: matumaini ndiyo yanayotuwezesha kuelewa ya kuwa hapa, kwenye mateso, ni uhai. Wanangu, mimi nasema nanyi; sauti yangu inasema na nafsi yenu, Moyo wangu unasema na moyo wenu: Enyi, mitume wa upendo wangu, Moyo wangu wa kimama jinsi gani unavyowapenda. Mambo haya nataka kuwafundisha. Jinsi gani Moyo wangu unataka muwe wakamilifu, lakini mtakuwa hivyo tu wakati nafsi, mwili na upendo yatakapoungana ndani yenu. Kama wanangu nawaombeni: salini sana kwa ajili ya Kanisa na kwa wahudumu wake, kwa wachungaji wenu, ili Kanisa liwe kama Mwanangu anavyolitaka: safi kama maji ya chemchemi na limejaa upendo. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, maneno yangu ni manyofu lakini yamejaa upendo wa kimama na mahangaiko. Wanangu, juu yenu vivuli vya giza na vya udanganyifu vinaenea zaidi na zaidi, mimi ninawaiteni kuelekea mwanga na ukweli, mimi ninawaita kuelekea Mwanangu. Yeye peke yake huweza kugeuza kukata tamaa na maumivu yetu kuwa amani na utulivu, Yeye peke yake huweza kutoa matumaini katika maumivu makali sana. Mwanangu ni uzima wa ulimwengu, kwa kadiri mtakavyomjua, ndivyo mtakavyomkaribia na kumpenda maana Mwanangu ni upendo, na upendo unageuza yote. Yeye hufanya la ajabu hata neno lisilo la maana bila upendo machoni penu. Kwa hiyo nawaambieni tena ya kwamba mnapaswa kupenda sana ikiwa mnatamani kukua kiroho. Najua, enyi mitume wa upendo wangu, kwamba si rahisi sikuzote, lakini, wanangu, hata njia ngumu ni njia zinazoongoza kwenye ukuaji wa kiroho, wa kiimani na kwa Mwanangu. Wanangu, salini, mfikirie Mwanangu, nyakati zote za siku zenu inueni nafsi zenu kwake nami nitakusanya sala zenu kama maua kutoka bustani nzuri kuliko zote na kumpa Mwanangu. Muwe hakika mitume wa upendo wangu, wapeni wote upendo wa Mwanangu, muwe bustani zenye maua mazuri kuliko yote. Kwa njia ya sala saidieni wachungaji wenu ili waweze kuwa baba za kiroho waliojaa upendo kwa watu wote. Nawashukuru.
   




To compare Medjugorje messages with another language versions choose

For God to live in your hearts, you must love.

`