Our Lady of Medjugorje Messages containing 'wote'

Total found: 92
Wanangu wapendwa! Leo kwa namna ya pekee nawaalikeni msali. Salini, wanangu, ili muweze kutambua ninyi ni akina nani na ni wapi mnayopaswa kwenda. Muwe watangazaji wa Habari Njema na watu wa matumaini. Muwe upendo kwa wale wote wasio na upendo. Wanangu, mtakuwa yote na kuyatimiza yote iwapo tu mkisali na mkiwa tayari kupokea mapenzi ya Mungu, Mungu ambaye anatamani kuwaongoza katika maisha ya uzima wa milele. Mimi nipo pamoja nanyi na siku hata siku ninawaombeeni kwa Mwanangu Yesu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, zingatieni akilini, kwa maana nawaambia: upendo utashinda! Najua ya kuwa wengi wenu wanapoteza matumaini kwa kuwa wanaona wamezungukwa na mateso, maumivu, husuda na wivu, hata hivyo mimi ni Mama yenu. Mimi nipo katika Ufalme, lakini hata hapa nipo pamoja nanyi. Mwanangu ananituma tena ili niwasaidieni, kwa hiyo msipoteze matumaini ila nifuateni, kwa maana ushindi wa Moyo wangu ni kwa jina la Mungu. Mwanangu mpendwa anawafikiria, kama alivyofanya siku zote: mwaminini na mwishi kama Yeye! Yeye ni uzima wa ulimwengu. Wanangu, kumwishi Mwanangu maana yake ni kuishi Injili. Si kitu rahisi. Ni jambo linalodai upendo, rehema na sadaka. Hayo huwatakasa na kufungua Ufalme: Sala nyofu, isiyo maneno bali itokayo moyoni, itawasaidieni. Vivyo hivyo kufunga, maana hayo huleta ongezeko la upendo, rehema na sadaka. Kwa hiyo msipoteze matumaini, ila nifuateni. Nawaomba tena msali kwa ajili ya wachungaji wenu, ili wamtazame daima Mwanangu, aliyekuwa Mchungaji wa kwanza wa ulimwengu, na ambaye familia yake ilikuwa ulimwengu wote. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa, nipo hapa katikati yenu kama Mama atakaye kuwasaidia kuujua ukweli. Nilipokuwa nikiishi maisha kama yenu duniani, nilikuwa nikijua ukweli na kwa hivyo kuwa na kipande cha Mbinguni duniani. Kwa hiyo, wanangu, nataka ninyi pia muwe washiriki wa hali hivyo. Baba wa Mbinguni ataka mioyo minyofu, ijaayo ujuzi wa ukweli: Ataka muwapende wote mnaokutana nao, maana mimi pia nampenda Mwanangu katika ninyi nyote. Huo ndio mwanzo wa ujuzi wa ukweli. Mtapewa kweli nyingi za uongo. Mtazitambua kwa mioyo iliyotakaswa kwa kufunga, kusali, kwa kufanya toba pamoja na kuishika Injili: Huo ndiyo ukweli wa pekee, nao ni ule ambao Mwanangu aliwaachieni. Msiufanyie utafiti mwingi sana: mnaombwa kuupenda na kuutoa, kama vile nilivyofanya mimi pia. Wanangu, mkipenda, mioyo yenu itakuwa maskani ya Mwanangu na yangu, na maneno ya Mwanangu yatakuwa mwongozo wa maisha yenu. Wanangu, nitawatumia, ninyi mitume wa upendo, kusaidia wanangu wote kuujua ukweli. Wanangu, mimi nimeliombea sikuzote Kanisa la Mwanangu, kwa hiyo nawasihi ninyi pia kufanya vile vile. Salini ili wachungaji wenu waangazwe kwa upendo wa Mwanangu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Hata leo ninawaalika: ishini katika sala mwito wenu. Leo, kama bado haijatokea awali, Shetani atamani kumfunga pumzi binadamu na roho yake kwa njia ya upepo wake unaoambukiza chukio na hofu. Katika mioyo mingi hakuna furaha kwa sababu hakuna Mungu wala sala. Uadui na vita zinaongezeka siku hata siku. Ninawaalika, wanangu, anzisheni upya kwa ari mwelekeo wa kutafuta utakatifu na upendo kwa maana nimekuja katikati yenu kwa ajili hiyo. Tuwe upendo na msamaha kwa wale wote wanaofahamu na kutaka kupenda kwa mapendo ya kibinadamu tu wala siyo kwa ule upendo mkubwa sana wa kimungu ambao Mungu anatualikia. Wanangu, matumaini ya kesho iliyo bora zaidi yawe daima mioyoni mwenu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, nipo hapa katikati yenu. Ninawatazama, ninawapa tabasamu na kuwapenda kama mama peke yake awezavyo kufanya. Kwa neema ya Roho Mtakatifu ajaye kwa njia ya usafi wangu, ninaona mioyo yenu na kuitolea kwa Mwanangu. Tangu muda mrefu nawaombeni muwe mitume wangu, na kusali kwa ajili ya wale wasioujua upendo wa Mungu. Naomba sala inayotokana na upendo, sala itoayo matunda na sadaka. Msipotee muda kutaka kuelewa kama mnastahili kuwa mitume wangu, Baba aliye Mbinguni atahukumu wote, lakini ninyi mpendeni na msikilizeni. Najua ya kuwa mambo hayo yote yanawafadhaisha, hata ujio wangu katikati yenu, lakini upokeeni kwa furaha na salini ili muelewe kwamba mnastahili kufanya kazi kwa ajili ya ufalme wa mbingu. Upendo wangu ni juu yenu. Salini ili upendo wangu udumu ndani ya kila moyo, kwa maana upendo huo unaosamehe ujitolea bila kukata tamaa. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, ninyi ni nguvu yangu. Ninyi, mitume wangu, ambao, kwa upendo wenu, unyenyekevu na sala ya kimya kimya, mnamwezesha Mwanangu ajulikane. Ninyi mnaishi ndani yangu. Ninyi mnanibeba mioyoni mwenu. Ninyi mnajua ya kuwa mna Mama awapendaye na aliyekuja kuwaletea upendo. Nawatazama katika Baba wa Mbinguni, natazama fikira zenu, maumivu yenu, mateso yenu na kuyaleta kwa Mwanangu. Msiogope! Msipoteze matumaini, maana Mwanangu humsikiliza Mama yake. Yeye hupenda tangu alipozaliwa, na ndio furaha yangu ya kuwa wanangu wote wajue upendo huo; na wote wale ambao, kwa sababu ya maumivu yao na kutoelewa kwao, walimwacha waweze kurudi kwake, na wote wao wasiomjua wamjue. Kwa sababu hiyo ninyi hapa ni mitume wangu, nami pia pamoja nanyi kama Mama yenu. Salini ili kuwa imara katika imani, maana upendo na rehema hutoka katika imani imara. Kwa njia ya upendo na rehema mtawasaidia wale wote wasiofahamu ya kuwa wanachagua giza badala ya nuru. Salini kwa ajili ya wachungaji wenu, maana wao ni nguvu ya Kanisa ambayo Mwanangu aliwaachieni. Kwa njia ya Mwanangu wao ni wachungaji wa roho. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nimewachagua ninyi, mitume wangu, kwa maana kila mmoja wenu huchukua ndani yake jambo njema. Ninyi mnaweza kunisaidia ili ule upendo ambao kwao Mwanangu amekufa, na kufufuka baadaye, ushinde tena. Kwa hiyo nawaalika, mitume wangu, kujaribu kuona katika kila kiumbe cha Mungu, katika wanangu wote, kitu chema na kujitahidi kuwaelewa. Wanangu, ninyi nyote ni kaka na dada kwa njia ya huyo Roho Mtakatifu. Ninyi mliojaa upendo kwa ajili ya Mwanangu, mnaweza kuwaeleza wote ambao hawajui cho chote kuhusu upendo huo, yote mnayoyafahamu. Ninyi mmejua upendo wa Mwanangu, mnaelewa ufufuko wake, na mnamgeuzia macho kwa furaha. Haja yangu ya kimama ni kwamba wanangu wote waungane katika upendo wa Yesu. Kwa hiyo nawaalika, mitume wangu, kuishi kwa furaha Ekaristi maana, katika Ekaristi, mwanangu anajitoa kwa ajili yenu tena na tena, na kwa mfano wake, anawaonyesha namna ya kutoa upendo na sadaka kwa jirani. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, fungueni mioyo yenu mkajaribu kuhisi jinsi ninavyowapenda na kutaka mpendeni Mwanangu. Nataka mpende zaidi kwa kuwa haiwezekani kumjua pasipo kumpenda, maana Yeye ndiye upendo. Wanangu, mimi nawajueni: najua maumivu yenu na mateso yenu maana niliyaishi. Nafurahi pamoja nanyi kwa furaha zenu. Nalia machozi pamoja nanyi katika maumivu yenu. Sitawaacheni kamwe. Nitaongea nanyi daima kwa upole wa kimama na, kama mama, nahitaji mioyo yenu ifumbuliwe, ili kwa hekima na unyofu mueneze upendo wa Mwanangu. Nawahitaji ninyi mfumbuliwe na kuwa wepesi kupokea mema na huruma. Nahitaji muungano wenu na Mwanangu, kwa maana nataka mpate kufanikiwa na kumsaidia kuleta heri kwa wanangu wote. Mitume wangu, nawahitaji, ili muwaonyeshe wote ukweli wa Mungu, ili moyo wangu, ulioteswa na kuteswa hata leo kupita kiasi, uweze kushinda katika upendo. Salini kwa ajili ya utakatifu wa wachungaji wenu, ili katika jina la Mwanangu, waweze kutenda maajabu, maana utakatifu hutenda maajabu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nataka kufanya kazi kwa njia yenu, wanangu, mitume wangu, ili mwishowe niweze kukusanya wanangu wote pale ambapo pameandaliwa tayari kwa ajili ya furaha yenu. Nawaombea, kusudi kwa matendo yenu muweze kugeuza, kwani muda umefika kwa matendo ya kweli, kwa ajili ya Mwanangu. Upendo wangu utafanya kazi ndani mwenu, nitawatumia ninyi. Muwe na imani nami, kwani yote ninayotamani, ninayatamani kwa ajili yenu, wema wa milele, ulioumbwa kwa njia ya Baba wa Mbinguni. Ninyi, wanangu, mitume wangu, muishi maisha ya duniani pamoja na wanangu ambao hawafahamu upendo wa Mwanangu, wale ambao hawaniiti mama. Lakini msiogope kushuhudia ukweli, kwa maana ikiwa ninyi hamtaogopa na kushuhudia ukweli kwa uhodari, ukweli utashinda kimuujiza. Kumbukeni: nguvu iko katika upendo. Wanangu, upendo ndio kutubu, kusamehe, kusali, kujitoa sadaka na rehema, maana mkijua kupenda kwa matendo mtawabadilisha na wengine, mtawezesha mwanga wa Mwanangu uingie katika mioyo yao. Nawashukuru. Muwaombee wachungaji wenu, wao ni mali ya Mwanangu. Yeye aliwaita. Salini ili wawe siku zote na nguvu na uhodari wa kung'aa kwa nuru ya Mwanangu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Hata leo Yeye Aliye Juu ananipa neema ya kuweza kuwapenda na kuwaalika muweze kuongoka. Wanangu, Mungu awe kesho yenu, vita, wasiwasi, huzuni yasiwatawale, ila furaha na amani zitawale mioyoni mwa watu wote, na mjue kuwa pasipo Mungu hamtapata kamwe amani. Kwa hiyo, wanangu, mrudieni Mungu na sala ili mioyo yenu iimbe kwa furaha. Mimi nipo pamoja nanyi na ninawapenda kwa upendo usio na kipimo. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, hata leo kwa furaha nipo pamoja nanyi na ninawaalika wote, wanangu, salini, salini, salini, ili muweze kuelewa upendo nilio nao kwenu. Upendo wangu una nguvu kuliko uovu, kwa hiyo wanangu mjongeeni Mungu ili muweze kuonja furaha yangu kwa Mungu. Pasipo Mungu, wanangu, hamtakuwa na wakati ujao, wala tumaini, wala wokovu, kwa hiyo acheni uovu na chagueni wema: Mimi nipo pamoja nanyi na pamoja nanyi namwomba Mungu kwa mahitaji yenu yote. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, mimi, kama Mama apendaye wanawe, natambua jinsi ulivyo mgumu muda huu mnaouishi. Naona mateso yenu, lakini jueni kwamba hamko peke yenu: Mwanangu yu pamoja nanyi! Yeye yupo popote, asiyeonekana, lakini mtaweza kumwona ikiwa mtamwishi. Yeye ndiye nuru inayoangaza roho yenu na kuleta amani. Yeye ndiye Kanisa, mnalopaswa kulipenda, kuliombea na kulilinda daima: si kwa maneno tu, bali kwa matendo ya upendo. Wanangu, fanyeni yote ili Mwanangu ajulikane kwa watu wote, na aweze kupendwa, kwa maana ukweli ni katika Mwanangu, aliyezaliwa na Mungu, Mwana wa Mungu. Msipoteze muda kwa kufikiri mno; mtajitenganisha na ukweli. Pokeeni Neno lake kwa moyo mnyofu na kuliishi. Mkiishi Neno lake, mtasali. Mkiishi Neno lake, mtapenda kwa upendo wenye huruma, na mtapendana. Kwa kadiri mtakavyokuwa na upendo hivyo ndivyo mtakavyokuwa mbali na kifo. Kwa wale watakaoishi na kulipenda Neno la Mwanangu, kifo kitakuwa uhai kwao. Nawashukuru! Salini kwa ajili ya kuweza kuona Mwanangu katika wachungaji wenu. Salini kwa ajili ya kuweza kumkumbatia katika wao.
Wanangu wapendwa, wapendwa mitume wangu wa upendo, waletaji wangu wa ukweli, ninawaalika tena na ninawakusanya karibu nami ili mnisaidie, ili muwasaidie wanangu wote wenye kiu ya upendo na ukweli, wenye kiu ya Mwanangu. Mimi ndimi neema ya Baba wa Mbinguni iliyotumwa kuwasaidieni kuishi neno la Mwanangu. Pendaneni. Nimeyaishi maisha yenu duniani. Najua kwamba si kitu rahisi kila mara lakini, mkipendana, mtasali kwa moyo, mtafikia vilele vya maisha ya roho, na njia ya kwenda mbinguni itafunguliwa mbele yenu. Pale nawangojea mimi, Mama yenu, kwa maana mimi nipo pale. Muwe waaminifu kwa Mwanangu na muwafundishe wengine uaminifu. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwasaidia. Nitawafundisha imani, ili muweze kuwafikishia wengine kwa njia sahihi. Nitawafundisha ukweli, ili muweze kuufahamu. Nitawafundisha upendo, ili mjue upendo wa kweli ni kitu gani. Wanangu, Mwanangu atafanya yote ili aongee kwa njia ya maneno na matendo yenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nataka kuongea nanyi tena juu ya upendo. Nimewakusanya kunizunguka kwa Jina la Mwanangu, kwa kadiri ya mapenzi yake. Nataka imani yenu iwe thabiti na iwe inatokana na mapendo, kwa maana wanangu wale wanaoelewa upendo wa Mwanangu na kuufuata, huishi katika mapendo na matumaini. Wamejua upendo wa Mungu. Kwa hiyo, wanangu, salini, salini ili muweze kupenda zaidi muwezavyo na kutenda matendo ya upendo. Kwa maana, imani peke yake, pasipo upendo wala matendo ya upendo, si neno ninaloomba kwenu. Wanangu, ule ni utovu wa imani, ni kujisifu mwenyewe. Mwanangu hutaka imani na matendo, upendo na wema. Mimi ninasali, lakini nawaombeni pia kusali na kuishi upendo, kwa maana nataka ya kuwa Mwanangu, atakapoona mioyo ya wanangu wote, aweze kuona ndani yake upendo na wema, sio chukio na ubaridi. Wanangu, mitume ya upendo wangu, msipoteze tumaini, msikate tamaa: ninyi mnaweza kufanya! Mimi ninawapeni moyo na kuwabariki, maana yote yaliyopo duniani hapa - ambayo kwa bahati mbaya wanangu wengi huweka mahali pa kwanza - yatatoweka na upendo na matendo ya upendo tu zitabaki, nazo zitawafungulia malango ya Ufalme wa Mbinguni. Nitawangojea karibu na malango hayo, karibu na malango hayo nataka kuwangojea na kuwakumbatia wanangu wote. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, mimi ni sikuzote pamoja nanyi, kwa maana Mwanangu alinikabidhi ninyi. Nanyi, wanangu, mnanihitaji mimi, mnitafute, mnijie na mfurahishe Moyo wangu wa kimama. Mimi ninawapenda na nitawapenda ninyi mnaoteseka na kutolea mateso yenu kwa ajili ya Mwanangu na kwa ajili yangu. Upendo wangu hutafuta upendo wa wanangu wote na wanangu wote hutafuta upendo wangu. Kwa njia ya upendo Yesu hutafuta ushirika kati ya Mbingu na dunia, kati ya Baba wa mbinguni na ninyi, wanangu, Kanisa lake. Kwa hiyo lazima kusali sana, kusali na kulipenda Kanisa ambalo ninyi ni wake. Sasa Kanisa linateseka na kuhitaji mitume ambao, wakipenda ushirika, wanaposhuhudia na kutoa, waonyeshe njia za Mungu. Kanisa linahitaji mitume ambao, wakiishi Ekaristi kwa moyo, watende matendo makuu. Kanisa linawahitaji ninyi, mitume wangu wa upendo. Wanangu, Kanisa limeteswa na kusalitiwa tangu siku zake za awali, lakini linazidi kukua siku hata siku. Kanisa halitaharibiki, kwa maana Mwanangu alilipa moyo: Ekaristi. Nuru ya ufufuo wake imeng’aa na itang’aa juu yake. Kwa hiyo msiogope! Waombeeni wachungaji wenu, ili wawe na nguvu na upendo kwa kuwa madaraja ya wokovu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, Leo pia nawaletea Mwanangu Yesu katika mikono yangu, na kwa mikono hiyo nawapeni amani Yake na hamu ya Mbinguni. Ninasali pamoja nanyi kwa ajili ya amani na ninawaalika muwe amani. Nawabariki wote kwa baraka yangu ya kimama na ya amani. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, kama Mama nafurahi ya kuwa katikati yenu, kwa maana nataka kuongea nanyi tena kuhusu maneno ya Mwanangu na upendo wake. Natumaini mtanipokea kwa upendo, maana maneno ya Mwanangu na upendo wake ni nuru na tumaini la pekee katika giza la siku hizi. Huu ni ukweli wa pekee, nanyi mtakaoupokea na kuuishi, mtakuwa na mioyo safi na minyenyekevu. Mwanangu hupenda mioyo safi na minyenyekevu. Mioyo safi na minyenyekevu inahuisha maneno ya Mwanangu: inayaishi, inayaeneza na kufanya hata wote wayasikie. Maneno ya Mwanangu yanaamsha maisha ya wale wanaoyasikiliza, maneno ya Mwanangu hurudisha upendo na matumaini. Kwa hiyo, mitume wangu wapenzi, wanangu, isheni maneno ya Mwanangu. Pendaneni kama Yeye alivyowapenda. Pendaneni katika jina lake na kumbukumbu lake. Kanisa huendelea na kukua kwa ajili ya wale wanaosikiliza maneno ya Mwanangu, kwa sababu ya wanaohuzunika na kuteseka kimyakimya katika tumaini la kukombolewa milele. Kwa hiyo wanangu wapendwa, maneno ya Mwanangu na upendo wake yawe wazo la kwanza na la mwisho la siku yenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, hata leo nawaalika kusali. Pasipo sala hamwezi kuishi maana sala ndiyo mnyororo unaowawezesha kumkaribia Mungu. Kwa hiyo wanangu, kwa unyenyekevu wa moyo mrudieni Mungu na Amri zake ili muweze kusema kwa moyo wote: kama mbinguni lifanyike hata duniani. Wanangu, ninyi ni huru kuamua katika uhuru kuwa wa Mungu ama dhidi yake. Tazameni kama shetani anavyotaka kuwaingiza katika dhambi na utumwa. Kwa hiyo, wanangu, rudini kwa Moyo Wangu ili Mimi niweze kuwaongoza kwa Mwanangu Yesu aliye Njia, na Ukweli na Uzima. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, ujio wangu kwenu ni zawadi ya Baba wa Mbinguni kwa ajili yenu. Kwa njia ya upendo wake ninakuja kuwasaidieni kupata njia inayowangoza kwenye ukweli, na kupata njia inayowaongoza kwa Mwanangu. Ninakuja kuwathibitishia ukweli. Nataka kuwakumbushia maneno ya Mwanangu. Yeye aliyatamka maneno ya wokovu kwa ulimwengu wote, maneno ya upendo kwa watu wote, ule upendo aliouonyesha kwa kujitolea kwake sadaka. Lakini hata leo wanangu wengi hawamjui, hawataki kumjua, hawamjali. Kwa sababu ya kutokujali kwao, moyo wangu unateseka kwa uchungu. Mwanangu amekuwa daima katika Baba. Alipozaliwa duniani, ametuletea Umungu, wakati kutoka kwangu ameuchukua ubinadamu. Kwa njia yake Neno limefika katikati yetu. Kwa njia yake Mwanga, ambao hupenyeza mioyoni, huiangaza, huijaza upendo na faraja, umeingia ulimwenguni. Wanangu, wanaweza kumwona Mwanangu wale wote wanaompenda, kwa kuwa uso wake huonekana kwa njia ya mioyo inayojaa mapendo kumwelekea Yeye. Kwa hiyo, wanangu, mitume wangu, mnisikilize! Acheni uovu na ubinafsi. Msiishi tu kwa ajili ya vitu vya ulimwengu, vinavyoharibika. Mpendeni Mwanangu na muwawezeshe wengine kuutambua uso kwa njia ya mapendo mliyo nayo kwake. Mimi nitawasaidia kumjua zaidi. Mimi nitawaeleza kuhusu Yeye. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Moyo wangu usio na doa unatoka damu nikiwaangalieni katika dhambi na mazoea mabaya. Nawaalika: mrudieni Mungu na salini ili mpate kufanikiwa duniani. Mungu anawaalika kwa njia yangu ili mioyo yenu iwe tumaini na furaha kwa wale wote walio mbali. Ombi langu liwe kwenu manukato kwa nafsi na moyo ili mtukuze Mungu Mwumbaji anayewapenda na kuwaalika kwa mambo ya milele. Wanangu, maisha ni mafupi, mtumie nafasi hii kwa ajili ya kutenda mema. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
   




To compare Medjugorje messages with another language versions choose

For God to live in your hearts, you must love.

`