Our Lady of Medjugorje Messages containing 'zaidi'

Total found: 49
Wanangu wapendwa, mapenzi na upendo wa Baba wa mbinguni hufanya mimi niwe katikati yenu, ili kusaidia kwa upendo wa kimama ukuaji wa imani katika mioyo yenu, ili kwamba muweze hakika kuelewa lengo la maisha ya kidunia na ukuu wa yale ya kimbingu. Wanangu, maisha ya kidunia ndiyo njia kuelekea umilele, kuelekea ukweli na uzima: kuelekea kwa Mwanangu. Kwa njia hii nataka kuwaongoza. Ninyi, wanangu, ninyi wenye sikuzote kiu ya upendo mkubwa zaidi, ukweli na imani, mjue ya kuwa moja tu ni chemchemi mnakoweza kunywa: imani katika Baba wa mbinguni, imani katika upendo wake. Mtegemee kabisa mapenzi yake wala msiogope: kila lililo bora kwa ajili yenu, kila linalowachukua kwenye uzima wa milele, mtapewa! Mtaelewa ya kuwa lengo la maisha si sikuzote kutaka na kutwaa, lakini kupenda na kutoa; mtakuwa na amani ya kweli na upendo wa kweli, mtakuwa mitume wa upendo. Kwa mfano wenu, mtawafanya wale wanangu wasiomjua Mwanangu na upendo wake watake kumjua. Wanangu, mitume wa upendo wangu, mwabuduni Mwanangu pamoja nami, na mpendeni juu ya vyote. Jaribuni sikuzote kuishi katika ukweli wake. Ninawashukuru.
Wanangu wapendwa, Nawaletea ninyi Mwanangu Yesu ili awabariki na kuwafunulia Upendo wake utokao mbinguni. Moyo wenu unatamani amani inayopungua zaidi na zaidi duniani. Kwa sababu hiyo watu wako mbali na Mungu, nafsi zinaumwa na zinaelekea kifo cha kiroho. Mimi nipo pamoja nanyi, wanangu, niwaongoze kwenye njia hii ya wokovu ambayo Mungu anawaiteni. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, najua kuwepo katika maisha yenu na mioyo yenu. Nahisi upendo wenu, nasikia sala zenu na kuzipeleka kwa Mwanangu. Lakini, wanangu, mimi nataka kwa njia ya upendo wa kimama, kuwepo katika maisha ya wanangu wote. Nataka kukusanya karibu yangu wanangu wangu wote, chini ya joho langu la kimama. Kwa hiyo ninawaalika ninyi na kuwaiteni mitume wa upendo wangu, il mnisaidie. Wanangu, Mwanangu aliyatamka maneno haya: "Baba yetu”, Baba yetu uliye popote na katika mioyo yetu, kwa sababu ataka kuwafundisha kusali kwa maneno na kwa hisia zenu. Ataka muwe bora zaidi kila siku, muishi upendo wenye rehema ulio sala na sadaka isiyo na mipaka kwa ajili ya wengine. Wanangu mpeni Mwanangu upendo kwa jirani; mpeni jirani wenu maneno ya faraja, ya huruma na matendo ya haki. Yote mliyoyatoa kwa wengine, enyi mitume wa upendo wangu, Mwanangu anayapokea kama zawadi. Nami ni pamoja nanyi kwa sababu Mwanangu ataka kwamba upendo wangu, ulio kama mwali wa nuru, uzihuishe nafsi zenu, uwasaidie katika kutafuta amani na uheri wa milele. Kwa hiyo, wanangu, pendaneni, na muunganishwe kwa njia ya Mwanangu, ili muwe wana wa Mungu ambao wote pamoja kwa moyo uliojaa, wazi na safi mkisema kwa pamoja “Baba yetu” pasipo kuogopa! Ninawashukuru.
Wanangu wapendwa, Leo ninawaalika kusali tena zaidi ili msikie katika mioyo yenu utakatifu wa msamaha. Katika familia lazima kuwepo utakatifu kwa sababu enyi wanangu, ulimwengu hauna wakati ujao bila upendo na utakatifu, kwa sababu katika utakatifu na katika furaha ninyi mjitolee kwa Mungu Mwumbaji anayewapendeni kwa upendo mkubwa sana. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, upendo wenu safi na wa kweli unavuta Moyo wangu wa kimama. Imani yenu na usadiki wenu katika Baba wa mbinguni ni mawaridi yenye harufu nzuri mnayonitolea: shada la mawaridi mazuri sana, lililotengenezwa kwa sala zenu, kwa matendo ya rehema na ya upendo. Mitume wa upendo wangu, ninyi mnaojaribu kumfuata Mwanangu pasipo unafiki na kwa moyo safi, ninyi ambao pasipo unafiki mnampenda, muwe ninyi wenyewe kusaidia: muwe mfano kwa wale ambao hawajajua upendo wa Mwanangu. Lakini, wanangu, siyo kwa maneno tu, bali hata kwa matendo na hisia safi, ambayo kwa njia yake mnamtukuza Baba wa mbinguni. Mitume wa upendo wangu, ni wakati wa kukesha na ninawaombeni upendo; na msihukumu mtu yeyote, kwa maana Baba wa mbinguni atahukumu wote. Ninawaombeni mpende, na mueneze ukweli, kwa maana ukweli ni wa kale: Ukweli siyo mpya, Ukweli ni wa milele, Ukweli ndiyo ukweli! Ukweli unatolea ushuhuda wa umilele wa Mungu. Bebeni mwanga wa Mwanangu na mpasue giza ambalo linataka kuwakandamiza zaidi na zaidi. Msiwe na hofu: kwa ajili ya neema na upendo wa Mwanangu, mimi nipo pamoja nanyi! Ninawashukuru. ”
Wanangu wapendwa! Katika wakati huu ninawaita kumrudia Mungu na sala. Waiteni watakatifu wote wawasaidie ili wawe mfano na msaada kwenu. Shetani ni mwenye nguvu na anapigania kuivutia kwake mioyo mingi zaidi awezavyo. Anataka vita na chuki. Kwa sababu hiyo Mimi ni pamoja nanyi muda mrefu ili niwaongoze kwenye njia ya wokovu, kwa Yule aliye njia, kweli na uzima. Wanangu, rudini kwa upendo kumwelekea Mungu naye atakuwa nguvu yenu na kimbilio lenu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Katika wakati huo ninawaalika kusali, kufunga na kujikana ili muweze kuwa wenye nguvu zaidi katika imani. Huu ni wakati wa mwamko na wa kuzaliwa upya. Kama vitu vya asili vinavyojitoa nanyi wanangu, fikirini juu ya mambo mliyopokea. Muwe waletaji wa amani na wa upendo wenye furaha ili kuishi vizuri duniani. Tamanini Mbingu kwa sababu Mbinguni hakuna wala huzuni wala machukio. Kwa hiyo, wanangu, amueni tena kuongoka, na utakatifu utawale katika maisha yenu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Ninawatazama na ninamshukuru Mungu kwa kila mmoja wenu, kwa sababu ameniruhusu niwe nanyi tena ili kuwasihi katika utakatifu. Wanangu amani inavurugika na shetani anataka mahangaiko. Kwa hiyo maombi yenu yawe na nguvu zaidi ili kila roho chafu ya utengano na vita itulie. Iweni wajenzi wa amani na wachukuaji wa Aliyefufuka ndani yenu na karibu nanyi ili mema yapate kushinda katika kila mtu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Ongokeni na mvae mavazi ya toba na maombi ya kina ya kibinafsi na kwa unyenyekevu mwombe Aliye Juu amani. Katika wakati huu wa neema Shetani anataka kuwapotosha ninyi, nanyi wanangu, mwangalieni Mwanangu na kumfuata kuelekea Kalvari, kwa kujikana na kufunga. Niko pamoja nanyi kwa sababu Aliye Juu ameniruhusu niwapende ninyi na kuwaongoza kuelekea furaha ya moyo, katika imani inayokua ndani ya wale wote wanaompenda Mungu zaidi ya vitu vyote. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
   




To compare Medjugorje messages with another language versions choose
<<Previous  1 2 3

For God to live in your hearts, you must love.

`