Our Lady of Medjugorje Messages - complete list

Wanangu wapendwa, nataka kuongea nanyi tena juu ya upendo. Nimewakusanya kunizunguka kwa Jina la Mwanangu, kwa kadiri ya mapenzi yake. Nataka imani yenu iwe thabiti na iwe inatokana na mapendo, kwa maana wanangu wale wanaoelewa upendo wa Mwanangu na kuufuata, huishi katika mapendo na matumaini. Wamejua upendo wa Mungu. Kwa hiyo, wanangu, salini, salini ili muweze kupenda zaidi muwezavyo na kutenda matendo ya upendo. Kwa maana, imani peke yake, pasipo upendo wala matendo ya upendo, si neno ninaloomba kwenu. Wanangu, ule ni utovu wa imani, ni kujisifu mwenyewe. Mwanangu hutaka imani na matendo, upendo na wema. Mimi ninasali, lakini nawaombeni pia kusali na kuishi upendo, kwa maana nataka ya kuwa Mwanangu, atakapoona mioyo ya wanangu wote, aweze kuona ndani yake upendo na wema, sio chukio na ubaridi. Wanangu, mitume ya upendo wangu, msipoteze tumaini, msikate tamaa: ninyi mnaweza kufanya! Mimi ninawapeni moyo na kuwabariki, maana yote yaliyopo duniani hapa - ambayo kwa bahati mbaya wanangu wengi huweka mahali pa kwanza - yatatoweka na upendo na matendo ya upendo tu zitabaki, nazo zitawafungulia malango ya Ufalme wa Mbinguni. Nitawangojea karibu na malango hayo, karibu na malango hayo nataka kuwangojea na kuwakumbatia wanangu wote. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, leo ninawaalika nyote: salini kwa ajili ya nia zangu. Amani ipo hatarini kwa hiyo wanangu, salini na muwe waletaji wa amani na matumani katika ulimwengu huu wa wasiwasi ambamo shetani anashambulia na kuleta majaribu ya kila aina. Wanangu muwe thabiti katika sala na imara katika imani. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaombea ninyi nyote mbele ya Mwanangu, Yesu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, mimi ni sikuzote pamoja nanyi, kwa maana Mwanangu alinikabidhi ninyi. Nanyi, wanangu, mnanihitaji mimi, mnitafute, mnijie na mfurahishe Moyo wangu wa kimama. Mimi ninawapenda na nitawapenda ninyi mnaoteseka na kutolea mateso yenu kwa ajili ya Mwanangu na kwa ajili yangu. Upendo wangu hutafuta upendo wa wanangu wote na wanangu wote hutafuta upendo wangu. Kwa njia ya upendo Yesu hutafuta ushirika kati ya Mbingu na dunia, kati ya Baba wa mbinguni na ninyi, wanangu, Kanisa lake. Kwa hiyo lazima kusali sana, kusali na kulipenda Kanisa ambalo ninyi ni wake. Sasa Kanisa linateseka na kuhitaji mitume ambao, wakipenda ushirika, wanaposhuhudia na kutoa, waonyeshe njia za Mungu. Kanisa linahitaji mitume ambao, wakiishi Ekaristi kwa moyo, watende matendo makuu. Kanisa linawahitaji ninyi, mitume wangu wa upendo. Wanangu, Kanisa limeteswa na kusalitiwa tangu siku zake za awali, lakini linazidi kukua siku hata siku. Kanisa halitaharibiki, kwa maana Mwanangu alilipa moyo: Ekaristi. Nuru ya ufufuo wake imeng’aa na itang’aa juu yake. Kwa hiyo msiogope! Waombeeni wachungaji wenu, ili wawe na nguvu na upendo kwa kuwa madaraja ya wokovu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, miaka hii yote ambapo Mungu ananijalia kuwepo pamoja nanyi ni ishara ya upendo mwingi sana wa Mungu kwa kila mmoja wenu na ishara ya jinsi alivyowapenda. Wanangu, Yeye Aliye Juu amewapeni neema nyingi na anataka kuwapa neema nyingi zaidi. Lakini, wanangu, mioyo yenu imefungwa, inaishi katika hofu na hayaruhusu upendo wa Yesu na amani yake yapate nafasi katika mioyo yenu na kutawala maisha yenu. Kuishi pasipo Mungu ni kuishi gizani wala kutoujua kamwe upendo wa Baba na ulinzi wake kwa kila mmoja wenu. Kwa hiyo wanangu, leo hasa mwombeni Yesu ili tangu leo maisha yenu yapate kuzaliwa upya katika Mungu, na maisha yenu iwe nuru itokayo kwenu. Namna hii mtakuwa mashahidi wa uwepo wa Mungu ulimwenguni hasa kwa kila mtu aishiye gizani. Wanangu, nawapenda na kuwaombeeni kila siku kwake Yeye Aliye Juu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, Leo pia nawaletea Mwanangu Yesu katika mikono yangu, na kwa mikono hiyo nawapeni amani Yake na hamu ya Mbinguni. Ninasali pamoja nanyi kwa ajili ya amani na ninawaalika muwe amani. Nawabariki wote kwa baraka yangu ya kimama na ya amani. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, kama Mama nafurahi ya kuwa katikati yenu, kwa maana nataka kuongea nanyi tena kuhusu maneno ya Mwanangu na upendo wake. Natumaini mtanipokea kwa upendo, maana maneno ya Mwanangu na upendo wake ni nuru na tumaini la pekee katika giza la siku hizi. Huu ni ukweli wa pekee, nanyi mtakaoupokea na kuuishi, mtakuwa na mioyo safi na minyenyekevu. Mwanangu hupenda mioyo safi na minyenyekevu. Mioyo safi na minyenyekevu inahuisha maneno ya Mwanangu: inayaishi, inayaeneza na kufanya hata wote wayasikie. Maneno ya Mwanangu yanaamsha maisha ya wale wanaoyasikiliza, maneno ya Mwanangu hurudisha upendo na matumaini. Kwa hiyo, mitume wangu wapenzi, wanangu, isheni maneno ya Mwanangu. Pendaneni kama Yeye alivyowapenda. Pendaneni katika jina lake na kumbukumbu lake. Kanisa huendelea na kukua kwa ajili ya wale wanaosikiliza maneno ya Mwanangu, kwa sababu ya wanaohuzunika na kuteseka kimyakimya katika tumaini la kukombolewa milele. Kwa hiyo wanangu wapendwa, maneno ya Mwanangu na upendo wake yawe wazo la kwanza na la mwisho la siku yenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, hata leo nawaalika kusali. Pasipo sala hamwezi kuishi maana sala ndiyo mnyororo unaowawezesha kumkaribia Mungu. Kwa hiyo wanangu, kwa unyenyekevu wa moyo mrudieni Mungu na Amri zake ili muweze kusema kwa moyo wote: kama mbinguni lifanyike hata duniani. Wanangu, ninyi ni huru kuamua katika uhuru kuwa wa Mungu ama dhidi yake. Tazameni kama shetani anavyotaka kuwaingiza katika dhambi na utumwa. Kwa hiyo, wanangu, rudini kwa Moyo Wangu ili Mimi niweze kuwaongoza kwa Mwanangu Yesu aliye Njia, na Ukweli na Uzima. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, nimewaalika na ninawaalika tena kumjua Mwanangu, kuujua ukweli. Mimi nipo pamoja nanyi na ninasali ili mfanikiwe. Wanangu, yawapasa kusali sana ili kupata upendo na uvumilivu mwingi kadiri muwezavyo, ili kuweza kuvumilia sadaka na kuwa maskini rohoni. Mwanangu, kwa njia ya Roho Mtakatifu, yu sikuzote pamoja nanyi. Kanisa lake huzaliwa katika kila moyo unaomjua. Salini ili muweze kumjua Mwanangu, salini ili roho yenu iwe kitu kimoja pamoja naye. Hiyo ndiyo sala na huo ndio upendo wa kuwavutia wengine na kuwafanyeni kuwa mitume wangu. Ninawatazama kwa upendo, kwa upendo wa kimama. Ninawajua, najua maumivu yenu na mateso yenu, kwa maana Mimi nami niliteswa kimya. Imani yangu ilinipa upendo na tumaini. Ninawaambieni tena: Ufufuo wa Mwanangu na Kupokewa kwangu mbinguni ni tumaini na upendo kwa ajili yenu. Kwa hiyo, wanangu, salini ili kujua ukweli, ili kupata imani thabiti, ya kuongoza mioyo yenu na kuweza kugeuza mateso yenu na maumivu yenu kuwa upendo na tumaini. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Katika wakati huu wa neema nawaalikeni nyote kuongoka. Wanangu, mnapenda kidogo, na bado mnasali kidogo. Mmepotea wala hamjui lengo lenu ni nini. Chukueni msalaba wenu, mwangalieni Yesu mumfuate. Yeye anajitoa kwenu hata kufa msalabani maana anawapenda. Wanangu, nawaalikeni kurudia kusali kwa moyo kwa maana katika sala mnaweza kupata matumaini na maana ya uwepo wenu. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaombea. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, ujio wangu kwenu ni zawadi ya Baba wa Mbinguni kwa ajili yenu. Kwa njia ya upendo wake ninakuja kuwasaidieni kupata njia inayowangoza kwenye ukweli, na kupata njia inayowaongoza kwa Mwanangu. Ninakuja kuwathibitishia ukweli. Nataka kuwakumbushia maneno ya Mwanangu. Yeye aliyatamka maneno ya wokovu kwa ulimwengu wote, maneno ya upendo kwa watu wote, ule upendo aliouonyesha kwa kujitolea kwake sadaka. Lakini hata leo wanangu wengi hawamjui, hawataki kumjua, hawamjali. Kwa sababu ya kutokujali kwao, moyo wangu unateseka kwa uchungu. Mwanangu amekuwa daima katika Baba. Alipozaliwa duniani, ametuletea Umungu, wakati kutoka kwangu ameuchukua ubinadamu. Kwa njia yake Neno limefika katikati yetu. Kwa njia yake Mwanga, ambao hupenyeza mioyoni, huiangaza, huijaza upendo na faraja, umeingia ulimwenguni. Wanangu, wanaweza kumwona Mwanangu wale wote wanaompenda, kwa kuwa uso wake huonekana kwa njia ya mioyo inayojaa mapendo kumwelekea Yeye. Kwa hiyo, wanangu, mitume wangu, mnisikilize! Acheni uovu na ubinafsi. Msiishi tu kwa ajili ya vitu vya ulimwengu, vinavyoharibika. Mpendeni Mwanangu na muwawezeshe wengine kuutambua uso kwa njia ya mapendo mliyo nayo kwake. Mimi nitawasaidia kumjua zaidi. Mimi nitawaeleza kuhusu Yeye. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Leo ninawaletea upendo wangu. Mungu ameniruhusu kuwapenda ninyi na kwa upendo nawaalika mwongoke. Wanangu, ninyi ni maskini katika upendo, na wala hamjaelewa bado ya kuwa Mwanangu Yesu ametolea maisha Yake ili awaokoeni na kuwapa uzima wa milele. Kwa hiyo salini wanangu, salini ili muweze kuelewa katika sala upendo wa Mungu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, msiwe na mioyo migumu, iliyofungwa na iliyojaa hofu. Pokeeni upendo wangu wa kimama uiangaze na kuijaza mioyo yenu upendo na matumaini, ili, kama Mama, niyalainishe maumivu yenu: ninayajua, na nimeyaonja. Maumivu huinua nayo ni sala kuu kuliko zote. Mwanangu huwapenda hasa wanaopokea maumivu. Alinituma Mimi niyalainishe na kuwaletea matumaini. Mumwamini Yeye. Najua kuwa ni vigumu kwenu, maana mnaona giza linalozidi kuongeza karibu yenu pande zote. Wanangu, giza mtalivunja kwa njia ya sala na upendo. Yule anayesali na kupenda haogopi, ana matumaini na upendo wenye huruma: Anaona mwanga, na anamwona Mwanangu. Kama mitume wangu nawaalika mjaribu kuwa mfano wa upendo wenye huruma na wenye matumaini. Salini sikuzote tena kwa ajili ya kupata upendo mwingi kadiri muwezavyo, maana upendo huleta mwanga unaovunja kila giza, na humleta Mwanangu. Msiogope, ninyi si peke yenu: Mimi nipo pamoja nanyi! Ninawasihi waombeeni wachungaji wenu, ili wawe na upendo kila wakati na wawe na matendo ya upendo kwa Mwanangu, kwa njia yake na kwa kumkumbuka Yeye. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Moyo wangu usio na doa unatoka damu nikiwaangalieni katika dhambi na mazoea mabaya. Nawaalika: mrudieni Mungu na salini ili mpate kufanikiwa duniani. Mungu anawaalika kwa njia yangu ili mioyo yenu iwe tumaini na furaha kwa wale wote walio mbali. Ombi langu liwe kwenu manukato kwa nafsi na moyo ili mtukuze Mungu Mwumbaji anayewapenda na kuwaalika kwa mambo ya milele. Wanangu, maisha ni mafupi, mtumie nafasi hii kwa ajili ya kutenda mema. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, Moyo wangu wa kimama hutaka wongofu wenu mnyofu na ya kuwa muwe na imani thabiti, ili muweze kuwatangazia watu wote wanaowazunguka upendo na amani. Lakini, wanangu, msisahau: kila mmoja wenu mbele ya Baba aliye Mbinguni ni ulimwengu wa pekee! Kwa hiyo nguvu ya Roho Mtakatifu isiyo kifani iweze kutenda kazi ndani mwenu! Muwe wanangu safi kwa kiroho. Katika karama ya kiroho kuna uzuri. Yote yaliyo ya kiroho ni hai na nzuri ajabu. Msisahau ya kuwa katika Ekaristi, iliyo moyo wa imani, Mwanangu yu daima pamoja nanyi. Yeye anawajia na pamoja nanyi humega mkate maana, Mwanangu, kwa ajili yenu amekufa, amefufuka akaja tena. Haya maneno yangu ni ya muhimu kwa maana ni ukweli, na ukweli haubadiliki: lakini wanangu wengi hawayatambui. Wanangu, maneno yangu si mazee wala mapya, ni ya milele. Kwa hiyo nawaalika ninyi, wanangu, kuangalia alama za nyakati, na "kukusanya misalaba yaliyovunjika" na kuwa mitume wa Ufunuo. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Uwepo wangu ni zawadi ya Mungu na kichocheo cha uwongofu wenu. Shetani ana nguvu na anataka kutia moyoni na fikirani mwenu fujo na wasiwasi. Kwa hiyo, ninyi wanangu salini ili Roho Mtakatifu awaongoze katika njia iliyonyoka ya furaha na amani. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaombea ninyi mbele ya Mwanangu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, kama Mama wa Kanisa, kama Mama yenu, ninatabasamu nikiwaona kunijia, kukusanyika kandokando yangu na kunitafuta. Ujio wangu katikati yenu ni onyesho la kadiri Mbingu inavyowapenda. Ujio wangu unawaonyesha njia ya kuelekea kwenye uzima wa milele, kuelekea wokovu. Mitume wangu, ninyi mnaojaribu kuwa na moyo safi na Mwanangu ndani yake, ninyi mpo katika njia njema. Ninyi mnamtafuta Mwanangu, mnatafuta njia njema. Yeye aliacha dalili nyingi za upendo wake. Ameacha tumaini. Ni rahisi kumpata, ikiwa mpo tayari kujitolea na kutubu, ikiwa mtakuwa na uvumilivu, rehema na upendo kwa jirani. Wanangu wengi hawaoni wala hawasikii maana hawataki. Hawapokei maneno na matendo yangu, lakini Mwanangu, kwa njia yangu, anawaalika wote. Roho yake huangaza wote katika mwanga wa Baba wa Mbinguni, katika ushirika kati ya Mbingu na dunia, katika upendano; maana upendo huita upendo na kutenda ili matendo yawe muhimu kuliko maneno. Kwa hiyo, mitume wangu, mliombee Kanisa lenu, lipende na tendeni matendo ya upendo. Ingawa limesalitiwa na kujeruhiwa, lipo hapa kwa sababu hutoka kwa Baba wa Mbinguni. Muwaombeeni wachungaji wenu, ili kuona ndani yao ukuu wa upendo wa Mwanangu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Mshukuruni Mungu kwa zawadi ya kuwepo kwangu pamoja nanyi. Salini, wanangu, mkaishi amri za Mungu mweze kuwa na heri duniani. Leo, katika siku hii ya neema nataka kuwapeni baraka yangu ya kimama ya amani na ya upendo wangu. Ninawaombeeni kwa Mwanangu na kuwaalika kudumu katika sala ili pamoja nanyi niweze kutimiza mipango yangu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, uwepo wangu halisi na wa uhai katikati yenu uwafanye kuwa wenye furaha kwani huo ni upendo mkuu wa Mwanangu. Yeye ananituma katikati yenu ili, kwa upendo wa kimama, Mimi niwaimarishe; ili muelewe kwamba maumivu na furaha, mateso na mapendo husaidia nafsi yenu kuishi kwa bidii zaidi; ili niwaalike tena kuadhimisha Moyo wa Yesu, moyo wa imani: Ekaristi. Mwanangu, siku kwa siku, hurudi hai katikati yenu: huwarudia, hata kama hakuwaacha kamwe. Wakati mmoja wenu, wanangu, anamrudia, Moyo wangu wa kimama hushtuka kwa furaha. Kwa hiyo Wanangu, irudieni Ekaristi, mrudieni Mwanangu. Njia ya kumrudia Mwanangu ni ngumu na imejaa kujinyima lakini mwishowe, kuna mwanga siku zote. Naelewa maumivu yenu na mateso yenu, na kwa upendo wa kimama, ninapangusa machozi yenu. Mtumainini Mwanangu, kwa maana Yeye atawafanyieni neno msilojua hata kuomba. Ninyi, wanangu, fikirieni nafsi yenu tu, kwani nafsi ni kitu cha pekee mliyo nayo duniani. Chafu ama safi, mtaichukua mbele ya Baba aliye Mbinguni. Kumbukeni: imani katika upendo wa Mwanangu hulipwa siku zote. Nawaambieni kuwaombea hasa wale ambao Mwanangu aliwaita kuishi wakimfuata na kulipenda kundi lao. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Ninawaangalia na ninawaona mmepotea, hamna wala sala wala furaha ndani ya mioyo yenu. Rudini, wanangu, kusali na wekeni Mungu katika mahali pa kwanza na si mtu. Msipoteze tumaini ninalowaletea. Wanangu, wakati huu uwe kwenu kila siku kumtafuta Mungu katika kimya ya moyo wenu na salini, salini, salini mpaka sala iwe furaha kwenu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, nimekuja kwenu, katikati yenu, ili mnipe mahangaiko yenu, niweze kuyaleta mbele ya Mwanangu na kuwaombeeni kwake kwa manufaa yenu. Najua kuwa kila mmoja wenu ana mahangaiko yake, majaribu yake. Kwa hiyo kwa moyo wa kimama nawaalikeni: Njooni kwenye Meza ya Mwanangu! Yeye humega mkate kwa ajili yenu, huwapa Yeye mwenyewe. Huwapa matumaini. Anawaomba kuwa na imani zaidi, matumaini zaidi, utulivu zaidi. Anawaomba mpigane ndani yenu dhidi ya ubinafsi, hukumu na udhaifu wa kibinadamu. Kwa hiyo Mimi, kama Mama, nawaambieni: salini, maana sala huwapa nguvu ya kupigana ndani yenu. Mwanangu, alipokuwa mtoto, aliniambia mara nyingi ya kuwa wengi watanipenda na kuniita "Mama". Mimi hapa, katikati yenu, nasikia upendo na kuwashukuru! Kwa njia ya upendo huu namwomba Mwanangu ili hakuna hata mmoja wenu, wanangu, arudiye nyumbani jinsi alivyokuja. Ili mlete matumaini, rehema na upendo kadiri muwezavyo; ili muwe mitume wa upendo wangu, wanaoshuhudia kwa maisha yao kwamba Baba aliye Mbinguni ni chemchemi ya uzima si ya mauti. Wanangu wapendwa, nawaomba tena kwa moyo wa kimama: waombeeni wateule wa Mwanangu, kwa ajili ya mikono yao iliyobarikiwa, kwa ajili ya wachungaji wenu, ili waweze kumhubiri Mwanangu kwa upendo mwingi wawezavyo, na hivyo kusababisha wongofu. Nawashukuru.
   




To compare Medjugorje messages with another language versions choose

For God to live in your hearts, you must love.

`