Our Lady of Medjugorje Messages containing 'juu'

Total found: 44
Wanangu wapendwa, nani angeweza kusema nanyi vizuri zaidi kuliko Mimi kuhusu upendo na maumivu ya mwanangu? Niliishi pamoja naye, niliteseka pamoja naye. Nikiishi maisha ya kidunia, nilionja maumivu, maana nilikuwa mama. Mwanangu alipenda michakato na kazi ya Baba wa Mbinguni, Mungu wa kweli; na, kama alivyoniambia, alikuja kusudi awakomboe ninyi. Mimi nilificha maumivu yangu kwa njia ya upendo. Bali ninyi, wanangu, ninyi mnaweka maswali mengi, hamwelewi maumivu, hamwelewi kwamba, kwa njia ya upendo wa Mungu, mnapaswa kupokea maumivu na kuyachukua. Kila mwanadamu, iwe kwa kiwango kikubwa au kidogo, yampasa afanye mang'amuzi. Lakini, tukiwa na amani rohoni na tukiwa na hali ya neema, tumaini moja lipo: ni Mwanangu, Mungu aliyezaliwa na Mungu. Maneno yake ni mbegu ya uzima wa milele: Yanapopandwa katika roho njema, huleta matunda mengi. Mwanangu amechukua maumivu maana amepokea juu yake dhambi zenu. Kwa hiyo ninyi, wanangu, mitume wa upendo wangu, ninyi mnaoteswa: mjue kwamba maumivu yenu yatakuwa mwanga na utukufu. Wanangu, wakati mnapovumilia maumivu, wakati mnapoteswa, Mbingu huingia ndani yenu, nanyi mnawapa watu wote karibu nanyi Mbingu kidogo na matumaini mengi. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nikiwatazama hapa mmekusanyika kunizunguka, Mama yenu, ninaona nafsi safi nyingi. Ninawaona wanangu wengi wanaotafuta upendo na faraja lakini hakuna mtu anayewapa. Ninawaona hata wale wanaotenda mabaya maana hawana mifano myema, maana hawajamjua mwanangu. Mwanangu anawatuma ninyi kwangu, Mama, sawa kwa wote, niwafundisheni kupenda, ili muelewe ya kuwa ninyi ni ndugu. Ninatamani kuwasaidia. Mitume wa upendo wangu, kwa mwanangu yamtosha tamaa hai ya imani na upendo na atayakubali, lakini mnapaswa kustahili, kuwa na tamaa na mioyo wazi, Mwanangu huingia katika mioyo wazi. Mimi kama Mama ninatamani kwamba mjue Mwanangu katika kweli: Mungu aliyezaliwa na Mungu, kwamba mjue ukuu wa Upendo wake, ambao mnahitaji. Yeye amezichukua juu yake dhambi zenu, ameupata Ukombozi wenu, na badala yake anaomba mpendane ninyi kwa ninyi. Mwanangu ni upendo, Yeye anawapenda watu wote bila tofauti, watu wote wa nchi zote, wa mataifa yote. Ikiwa ninyi, wanangu, mngeishi upendo wa Mwanangu, ufalme wake ungekwisha kuwa duniani. Kwa hiyo, Mitume wa upendo wangu, salini, salini ili Mwanangu na upendo wake wawe ndani yenu nanyi muweze kuwa mfano wa upendo na muweze kuwasaidia wote wale ambao hawajamjua Mwanangu. Msisahau kamwe kwamba Mwanangu, mmoja na utatu, anawapendeni. Pendeni na wombeeni wachungaji wenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, ninawaelekea ninyi kama Mama yenu, Mama wa wenye haki, Mama wa wale wanaopenda na kuteseka, Mama wa watakatifu. Wanangu, ninyi pia mnaweza kuwa watakatifu: ni juu yenu. Watakatifu ni wale wanaompenda Baba wa Mbinguni kupita kiasi, wale wanaompenda kupita chochote. Kwa hivyo, wanangu, jaribuni daima kuboreka. Kama ninyi mnajaribu kuwa wema, mtaweza kuwa watakatifu, hata kama hamfikiri hiyo juu yenu. Kama mnafikiri kuwa wema, ninyi sio wanyenyekevu na kiburi huwatenga kutoka utakatifu. Katika ulimwengu huu wa wasiwasi, umejaa vitisho, mikono yako, mitume wa upendo wangu, inapaswa kuwa imenyoshwa katika maombi na rehema. Kwangu, wanangu, nipeni zawadi ya Rozari, mawaridi ninayopenda sana! Mawaridi yangu ni maombi yenu msemayo kwa moyo wote, na sio yale msemayo kwa midomo yenu tu. Mawaridi yangu ni matendo yenu ya maombi, imani na upendo. Wakati alipokuwa mtoto, mwanangu aliniambia kwamba watoto wangu watakuwa wengi na wataniletea mawaridi mengi. Sikuelewa, sasa najua kwamba ninyi ni watoto wale, wanaoniletea mawaridi wakati mnapompenda mwanangu kupita yote, wakati mnaposali kwa moyo wote, wakati mnapowasaidia walio maskini zaidi. Hayo ndiyo mawaridi yangu! Hii ndiyo imani, inayosababisha kila kitu katika maisha kifanyike kwa upendo; na kiburi hakijulikani; na muwe tayari daima, kusamehe upesi, bila kuhukumu na daima mjaribu kuelewa ndugu yako. Kwa hiyo, mitume wa upendo wangu, muwaombeeni wale wasiojua kupenda, wale wasiowapenda, wale waliowatenda mabaya, wale ambao hawakujua upendo wa Mwanangu. Wanangu, ninawaomba haya, kwa sababu kumbukeni: kuomba maana yake ni kupenda na kusamehe. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, wakati duniani upendo unapopunguka, wakati njia ya wokovu haipatikani, Mimi, Mama yenu, naja kuwasaidieni kujua imani ya kweli, iliyo hai na ya kina, na kuwasaidieni kupenda kabisa. Kama Mama ninatamani mpendane, muwe wema na safi. Ni hamu yangu muwe wenye haki na mpendane. Wanangu, muwe wafurahivu rohoni, muwe safi, muwe watoto. Mwanangu alisema kwamba anapenda kukaa kati ya wenye mioyo safi, maana wenye mioyo safi ni daima vijana na wafurahivu. Mwanangu aliwaambieni msameheane na mpendane. Najua kwamba si rahisi sikuzote. Mateso husababisha kukua rohoni. Ili kukua rohoni kadiri iwezekanavyo, lazima msamehe na kupenda kwa dhati na kwa kweli. Wana wangu wengi duniani hawamjui Mwanangu, hawampendi. Lakini ninyi mnaompenda Mwanangu na kumchukua moyoni salini, salini, na mkisali mumhisi Mwanangu karibu yenu. Nafsi yenu ipumue Roho yake! Mimi nipo kati yenu na kuongea juu ya mambo madogo na makubwa. Sitachoka kuwasimulieni habari ya Mwanangu, aliye upendo wa kweli. Kwa hiyo, wanangu, nifungulieni mioyo yenu, acheni niwaongoze kama mama. Muwe mitume wa upendo wa Mwanangu na wangu. Kama Mama nawasihi: msisahau wale walioitwa na Mwanangu wawaongoze. Wachukueni moyoni na muwaombee. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Kipindi hiki kiwe kwenu kipindi cha sala ili Roho Mtakatifu, kwa njia ya sala, ashuke juu yenu na awape wongofu. Fungueni mioyo yenu na someni Maandiko Matakatifu ili, kwa njia ya ushahidi, ninyi pia muweze kuwa karibu zaidi na Mungu. Wanangu, tafuteni hasa Mungu na vitu vya Mungu na acheni duniani vile vya dunia, maana Shetani huwavuta kwa mavumbi na dhambi. Ninyi mnaalikwa katika njia ya utakatifu na mmeumbwa kwa ajili ya Mbingu. Tafuteni, kwa hiyo, Mbingu na vitu vya mbinguni. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, katika wakati huo wa wasiwasi ninawaalika kumwamini zaidi Mungu aliye Baba yenu mbinguni na anayenituma kuwaongozeni kwake. Ninyi, mfungulieni mioyo yenu kwa zawadi ambazo Yeye ataka kuwapeni na katika kimya ya moyo wenu mwabuduni Mwanangu, aliyetolea maisha Yake ili muishi katika milele anakotaka kuwaongoza. Matumaini yenu na yawe furaha ya kukutana na Yule Aliye juu katika maisha ya kila siku. Kwa hiyo ninawaalika: msiache sala maana sala hutenda miujiza. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, Mimi ni Mama wa ninyi nyote na kwa hiyo msiogope kwa sababu mimi ninasikia sala zenu, najua kwamba mnanitafuta na kwa hiyo ninamwomba Mwanangu kwa ajili yenu; Mwanangu ambaye yu katika mwuungo pamoja na Baba wa mbinguni na pamoja na Roho Mfariji, Mwanangu anayewaongoza roho katika Ufalme alikotoka, ambao ni Ufalme wa amani na wa mwanga. Wanangu, mmepewa uhuru wa kuchagua, kwa hiyo mimi kama Mama ninawasihi mchague uhuru kwa mema, na kwa moyo safi na mnyofu mnaelewa, ingawa pengine hamwelewi maneno yote, ndani yenu mng'amue ukweli ni nini. Wanangu, msipoteze ukweli na maisha ya kweli kwa kufuata maneno ya uongo. Kwa njia ya maisha ya kweli Ufalme wa mbinguni huingia katika mioyo yenu, ni Ufalme wa upendo, wa amani na wa maelewano. Katika Ufalme ule, wanangu, hautakuwa na ubinafsi wa kuwaondoa kutoka kwa Mwanangu, kutakuwa na upendo na maelewano na jirani yako. Kwa hiyo kumbukeni, ninawaambieni tena, kusali maana yake ni kuwapenda wengine, kumpenda jirani yako, kujitoa kwa ajili yao; pendeni na toeni kwa jina la Mwanangu, hapo Yeye atatenda kazi ndani yenu na kwa ajili yenu. Wanangu, fikirini daima juu ya Mwanangu, mpendeni bila kipimo na hapo mtakuwa na maisha ya kweli, yatakayokuwa ya milele. Nawashukuru enyi Mitume wa upendo wangu!
Wanangu wapendwa, maneno yangu ni manyofu lakini yamejaa upendo wa kimama na mahangaiko. Wanangu, juu yenu vivuli vya giza na vya udanganyifu vinaenea zaidi na zaidi, mimi ninawaiteni kuelekea mwanga na ukweli, mimi ninawaita kuelekea Mwanangu. Yeye peke yake huweza kugeuza kukata tamaa na maumivu yetu kuwa amani na utulivu, Yeye peke yake huweza kutoa matumaini katika maumivu makali sana. Mwanangu ni uzima wa ulimwengu, kwa kadiri mtakavyomjua, ndivyo mtakavyomkaribia na kumpenda maana Mwanangu ni upendo, na upendo unageuza yote. Yeye hufanya la ajabu hata neno lisilo la maana bila upendo machoni penu. Kwa hiyo nawaambieni tena ya kwamba mnapaswa kupenda sana ikiwa mnatamani kukua kiroho. Najua, enyi mitume wa upendo wangu, kwamba si rahisi sikuzote, lakini, wanangu, hata njia ngumu ni njia zinazoongoza kwenye ukuaji wa kiroho, wa kiimani na kwa Mwanangu. Wanangu, salini, mfikirie Mwanangu, nyakati zote za siku zenu inueni nafsi zenu kwake nami nitakusanya sala zenu kama maua kutoka bustani nzuri kuliko zote na kumpa Mwanangu. Muwe hakika mitume wa upendo wangu, wapeni wote upendo wa Mwanangu, muwe bustani zenye maua mazuri kuliko yote. Kwa njia ya sala saidieni wachungaji wenu ili waweze kuwa baba za kiroho waliojaa upendo kwa watu wote. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Wakati huu ndio wakati wa neema na sala, wakati wa kungojea na wa majitoleo. Mungu anajitolea kwenu ili mumpende juu ya kila jambo. Kwa hiyo, wanangu, fumbueni mioyo yenu na jamaa zenu ili kungojea huko kugeuke kuwa sala na upendo na hasa majitoleo. Mimi nipo pamoja nanyi, wanangu, na ninawasihi msiache mema maana matunda yaonekana, yasikika, na yafika mbali. Kwa hiyo adui amekasirika na anafanya kila njia kuwaondoa ninyi katika sala. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, mapenzi na upendo wa Baba wa mbinguni hufanya mimi niwe katikati yenu, ili kusaidia kwa upendo wa kimama ukuaji wa imani katika mioyo yenu, ili kwamba muweze hakika kuelewa lengo la maisha ya kidunia na ukuu wa yale ya kimbingu. Wanangu, maisha ya kidunia ndiyo njia kuelekea umilele, kuelekea ukweli na uzima: kuelekea kwa Mwanangu. Kwa njia hii nataka kuwaongoza. Ninyi, wanangu, ninyi wenye sikuzote kiu ya upendo mkubwa zaidi, ukweli na imani, mjue ya kuwa moja tu ni chemchemi mnakoweza kunywa: imani katika Baba wa mbinguni, imani katika upendo wake. Mtegemee kabisa mapenzi yake wala msiogope: kila lililo bora kwa ajili yenu, kila linalowachukua kwenye uzima wa milele, mtapewa! Mtaelewa ya kuwa lengo la maisha si sikuzote kutaka na kutwaa, lakini kupenda na kutoa; mtakuwa na amani ya kweli na upendo wa kweli, mtakuwa mitume wa upendo. Kwa mfano wenu, mtawafanya wale wanangu wasiomjua Mwanangu na upendo wake watake kumjua. Wanangu, mitume wa upendo wangu, mwabuduni Mwanangu pamoja nami, na mpendeni juu ya vyote. Jaribuni sikuzote kuishi katika ukweli wake. Ninawashukuru.
Wanangu wapendwa! Mimi ni pamoja nanyi kwa muda mrefu kwa maana Mungu ni mkuu katika upendo wake na katika uwepo wangu. Wanangu, ninawaalika kurudi kwa Mungu na kwa sala. Kipimo cha kuishi kwenu kiwe upendo na msisahau, wanangu, kwamba maombi na kufunga hufanya miujiza ndani yenu na kuwazunguka. Yote mnayoyafanya yawe kwa ajili ya utukufu wa Mungu na hapo Mbingu itajaza moyo wenu na furaha mkahisi ya kuwa Mungu anawapenda na kunituma ili kuokoa ninyi na Dunia ambayo juu yake mnaishi. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Huu ni wakati wa upendo, wa uchangamfu, wa sala na wa furaha. Salini, wanangu, ili Mtoto Yesu azaliwe katika mioyo yenu. Fungueni mioyo yenu kwa Yesu anayejitoa kwa kila mmoja wenu. Mungu amenialika ili mimi niwe furaha na matumaini katika wakati huu nami ninawaambia: bila Mtoto Yesu hamna wala huruma wala hisia ya Mbingu, zinazofichika katika yule Mtoto mchanga. Kwa hiyo, wanangu, fanyeni kazi juu ya nafsi zenu wenyewe. Mkisoma Maandiko Matakatifu, mtagundua kuzaliwa kwa Yesu na furaha kama ile ya siku za kwanza ya matokeo ya Medjugorje iliyotolea kwa ubinadamu. Historia itakuwa ukweli, ambao hata leo unajirudia ndani yenu na kuwazunguka. Fanyeni kazi na jengeni amani kwa njia ya sakramenti ya Kitubio. Jipatanisheni na Mungu, wanangu, na mtaona miujiza inawazunguka. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Katika wakati huo ninawaalika kusali, kufunga na kujikana ili muweze kuwa wenye nguvu zaidi katika imani. Huu ni wakati wa mwamko na wa kuzaliwa upya. Kama vitu vya asili vinavyojitoa nanyi wanangu, fikirini juu ya mambo mliyopokea. Muwe waletaji wa amani na wa upendo wenye furaha ili kuishi vizuri duniani. Tamanini Mbingu kwa sababu Mbinguni hakuna wala huzuni wala machukio. Kwa hiyo, wanangu, amueni tena kuongoka, na utakatifu utawale katika maisha yenu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Mungu ameniruhusu kuwa pamoja nanyi leo pia kwa kuwaalika kusali na kufunga. Ishini wakati huu wa neema na muwe mashahidi wa tumaini maana, ninawaambia tena wanangu, kwa kusali na kufunga hata vita vinaweza kuisha. Wanangu, aminini na kuishi katika imani na kwa imani wakati huu wa neema na Moyo wangu usio na dhambi ya asili haumwachi yeyote kati yenu katika wasiwasi ikiwa ananikimbilia. Ninawaombea mbele ya Yeye aliye juu na ninasali ili amani iwepo katika mioyo yenu na kwa ajili ya tumaini katika wakati ujao. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Hata leo mimi ni pamoja nanyi ili kuwaambieni: wanangu, yule anayesali hana hofu ya wakati ujao wala hapotezi tumaini. Mmechaguliwa kwa kuleta furaha na amani, kwa maana ni wangu. Nimekuja hapa pamoja na jina: Malkia wa Amani kwa sababu ibilisi anataka kuleta wasiwasi na vita, anataka kuijaza mioyo yenu kwa hofu ya wakati ujao na wakati ujao ni wa Mungu. Kwa hiyo muwe wanyenyekevu, salini na acheni yote katika mikono ya Yeye aliye Juu aliyewaumba. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Ombeni, shuhudieni na mfurahi pamoja nami kwa sababu Mwenyezi Aliye Juu ananituma tena kuwaongoza katika njia ya utakatifu. Mjitambue, wanangu, kwamba maisha yenu ni mafupi na umilele unawasubiri ili kwamba pamoja na watakatifu wote mmtukuze Mungu kwa nafsi yenu. Msiwe na wasiwasi, wanangu, kwa mambo ya kidunia lakini tamanini Mbingu. Mbingu itakuwa lengo lenu na furaha itatawala moyoni mwenu. Niko pamoja nanyi na ninawabariki nyote kwa baraka yangu ya kimama. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Niko pamoja nanyi katika wakati huu wa rehema na ninawaalika nyote kuwa waleta amani na upendo katika ulimwengu huu, ambapo, wanangu, Mungu anawaalika kupitia Kwangu kuwa sala, upendo na kielelezo cha Paradiso, hapa duniani. Mioyo yenu na ijazwe na furaha na imani katika Mungu ili, wanangu, muwe na imani kamili katika mapenzi yake matakatifu. Hii ndiyo sababu mimi niko pamoja nanyi kwa sababu Yeye, Aliye Juu, ananituma kati yenu ili kuwahimiza ninyi kuwa na matumaini na mtakuwa waleta amani katika ulimwengu huu wenye wasiwasi. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Aliye juu aliniruhusu niwe pamoja nanyi; kuwa furaha kwenu na njia katika matumaini kwa sababu ubinadamu umeamua kifo. Kwa hiyo amenituma niwaelekeze kwamba bila Mungu hamna wakati ujao. Wanangu, muwe vyombo vya upendo kwa wale wote ambao hawajamjua Mungu wa upendo. Kwa furaha toeni ushuhuda wa imani yenu na msipoteze matumaini katika mabadiliko ya moyo wa mwanadamu. Niko pamoja nanyi na ninawabariki kwa baraka yangu ya mama. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Aliye juu amenituma kwenu ili niwafundishe jinsi ya kuomba. Sala hufungua mioyo na kutoa tumaini; imani huzaliwa na kuimarishwa. Wanangu, nawaiteni kwa upendo: mrudieni Mungu kwa maana Mungu ni upendo wenu na tumaini lenu. Msipoamua kwa ajili ya Mungu hamna mustakabali na kwa hiyo niko pamoja nanyi kuwaongoza ili muamue uongofu na uzima na sio kifo. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Ongokeni na mvae mavazi ya toba na maombi ya kina ya kibinafsi na kwa unyenyekevu mwombe Aliye Juu amani. Katika wakati huu wa neema Shetani anataka kuwapotosha ninyi, nanyi wanangu, mwangalieni Mwanangu na kumfuata kuelekea Kalvari, kwa kujikana na kufunga. Niko pamoja nanyi kwa sababu Aliye Juu ameniruhusu niwapende ninyi na kuwaongoza kuelekea furaha ya moyo, katika imani inayokua ndani ya wale wote wanaompenda Mungu zaidi ya vitu vyote. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
   




To compare Medjugorje messages with another language versions choose

For God to live in your hearts, you must love.

`