Our Lady of Medjugorje Messages containing 'ulimwengu'

Total found: 38
Wanangu wapendwa, maneno yangu ni manyofu lakini yamejaa upendo wa kimama na mahangaiko. Wanangu, juu yenu vivuli vya giza na vya udanganyifu vinaenea zaidi na zaidi, mimi ninawaiteni kuelekea mwanga na ukweli, mimi ninawaita kuelekea Mwanangu. Yeye peke yake huweza kugeuza kukata tamaa na maumivu yetu kuwa amani na utulivu, Yeye peke yake huweza kutoa matumaini katika maumivu makali sana. Mwanangu ni uzima wa ulimwengu, kwa kadiri mtakavyomjua, ndivyo mtakavyomkaribia na kumpenda maana Mwanangu ni upendo, na upendo unageuza yote. Yeye hufanya la ajabu hata neno lisilo la maana bila upendo machoni penu. Kwa hiyo nawaambieni tena ya kwamba mnapaswa kupenda sana ikiwa mnatamani kukua kiroho. Najua, enyi mitume wa upendo wangu, kwamba si rahisi sikuzote, lakini, wanangu, hata njia ngumu ni njia zinazoongoza kwenye ukuaji wa kiroho, wa kiimani na kwa Mwanangu. Wanangu, salini, mfikirie Mwanangu, nyakati zote za siku zenu inueni nafsi zenu kwake nami nitakusanya sala zenu kama maua kutoka bustani nzuri kuliko zote na kumpa Mwanangu. Muwe hakika mitume wa upendo wangu, wapeni wote upendo wa Mwanangu, muwe bustani zenye maua mazuri kuliko yote. Kwa njia ya sala saidieni wachungaji wenu ili waweze kuwa baba za kiroho waliojaa upendo kwa watu wote. Nawashukuru.
Wanangu, ninawaomba kuwa hodari wala kutowayawaya, maana hata mema madogo zaidi, ishara ya upendo mdogo zaidi hushinda maovu yanayoonekana zaidi na zaidi. Wanangu nisikilizeni ili mema yashinde, ili muweze kujua upendo wa Mwanangu ulio furaha mkubwa zaidi kuliko zote. Mikono ya mwanangu inawakumbatia, Yeye, apendaye nafsi, Yeye ambaye amejitolea kwa ajili yenu na kunajitolea sikuzote tena katika Ekaristi, Yeye aliye na maneno ya Uzima wa milele; kujua upendo wake, kufuata hatua zake, maana yake ni kuwa na mali ya kiroho. Huo ni utajiri unaojaza hisia iliyo njema, na unaoona upendo na mema popote. Mitume wa upendo wangu, wanangu, muwe kama mionzi ya jua ambayo kwa joto la upendo wa Mwanangu inawapasha joto wote wale wanaoizunguka. Wanangu, ulimwengu unahitaji mitume wa upendo, ulimwengu unahitaji sala nyingi, lakini sala zinazosaliwa kwa moyo na roho, si kwa midomo tu. Wanangu, muwe na hamu ya utakatifu mkiwa na unyenyekevu unaomwezesha Mwanangu kufanya kazi kwa njia yenu, kama Yeye apendavyo. Wanangu, sala zenu, fikira zenu na matendo yenu, haya yote yawafungulia ama kuwafungia mlango wa Ufalme wa Mbinguni. Mwanangu aliwaonyesha njia na kuwapa tumaini, mimi ninawafariji na kuwapa moyo maana, wanangu, mimi nilijua maumivu, lakini nilikuwa na imani na tumaini, sasa nimepata thawabu ya uzima katika Ufalme wa Mwanangu. Kwa hiyo, nisikilizeni, jipeni moyo, msiwayawaye. Nawashukuru.
Wanangu, Moyo wangu wa kimama unateseka wakati ninapotazama wanangu wasiopenda ukweli, wanaouficha; wakati ninapotazama wanangu wasiosali kwa moyo wala kwa matendo. Nimesikitika wakati ninapomwambia Mwanangu ya kuwa wana wangu wengi hawana imani tena, ya kuwa hawamjui Yeye, Mwanangu. Kwa hiyo ninawaalika, mitume wa upendo wangu: mjaribu kutazama mpaka ndani ya mioyo ya watu, na kule bila shaka mtapata hazina ndogo iliyofichwa. Kutazama hivyo ni rehema ya Baba wa mbinguni. Kutafuta mema hata palipo maovu makubwa zaidi, kutafuta kuwaelewana wala kutohukumiana: hilo ni neno ambalo Mwanangu anawaombeni. Nami, kama Mama, ninawaalika kumsikiliza. Wanangu, roho ni yenye nguvu kuliko mwili na, ikichukuliwa na upendo na matendo hushinda vikwazo vyote. Msisahau: Mwanangu aliwapendeni na anawapenda. Upendo wake ni pamoja nanyi na ndani yenu, wakati mpo kitu kimoja pamoja naye. Yeye ni mwanga wa ulimwengu, na hakuna mtu wala kitu kiwezacho kumsimamisha katika utukufu wa mwisho. Kwa hiyo, mitume wa upendo wangu, msiwe na hofu ya kushuhudia ukweli! Ushuhudieni kwa hamu, kwa matendo, kwa upendo, kwa sadaka yenu, lakini hasa kwa unyenyekevu. Shuhudieni ukweli kwa wale ambao hawajajua Mwanangu. Mimi nitakuwa karibu nanyi, mimi nitawatia moyo. Shuhudieni upendo usioishi tena, maana huja kutoka Baba wa mbinguni ambaye ni wa milele na anawatolea wana wangu wote umilele. Roho wa Mwanangu itakuwa karibu nanyi. Ninawaalika tena, wanangu: muwaombee wachungaji wenu, ombeni ili upendo wa Mwanangu uweze kuwaongoza. Nawashukuru.
Wanangu, Wakati mnaponijia kama Mama kwa moyo safi na wazi, mjue ya kuwa ninawasikiliza, ninawatia moyo, ninawafariji na hasa ninawaombeeni kwa Mwanangu. Najua ya kuwa mnataka kuwa na imani thabiti na kuionyesha kwa njia inayofaa. Neno analotaka Mwanangu kutoka kwenu ni imani ya kweli, thabiti na kubwa. Hivyo kila njia mnavyoielezea ni ya kufaa. Imani ni fumbo la ajabu tunalohifadhi moyoni. Inakaa baina ya Baba wa Mbinguni na wana wake wote. Hutambulika kwa matunda na kwa upendo ambao sisi tunao kwa viumbe vyote vya Mungu. Enyi mitume wa upendo wangu, wanangu, mtumaini Mwanangu! Saidieni ili wanangu wote wajue upendo wake. Ninyi ni matumaini yangu, ninyi mnaojitahidi kupenda Mwanangu pasipo unafiki. Kwa jina la upendo, kwa wokovu wenu, kulingana na mapenzi ya Baba wa Mbinguni na kwa njia ya Mwanangu, nipo hapa katikati yenu. Mitume wa upendo wangu, kwa njia ya sala na sadaka mioyo yenu iangazwe na upendo na mwanga wa Mwanangu. Mwanga ule na upendo ule uangaze wote wale mnaokutana na uwarudishe kwa Mwanangu! Mimi nipo nanyi. Hasa nipo pamoja na wachungaji wenu: kwa upendo wangu wa kimama ninawaangaza na kuwatia moyo, ili, kwa njia ya mikono iliyobarikiwa na Mwanangu, wabariki ulimwengu mzima. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, inasikitisha kwamba katikati yenu, wanangu, yapo mashindano mengi, chuki, masilahi yenu wenyewe na ubinafsi. Wanangu, hivi kwa urahisi mnamsahau Mwanangu, maneno Yake na upendo Wake. Imani inazimika katika roho nyingi na mioyo imetekwa na vitu vya ulimwenguni. Lakini moyo wangu wa kimama unajua ya kuwa katikati yenu kuna wale wanaoamini na kupenda, wale ambao wanajaribu kumkaribia Mwanangu zaidi na zaidi, ambao wanamtafuta bila kuchoka na namna hii, wananitafuta hata mimi. Hawa ndio wanyenyekevu na wapole ambao, pamoja na maumivu na mateso wanayoyachukua katika kimya, pamoja na tumaini lao na hasa pamoja na imani yao, ni mitume wa upendo wangu. Wanangu, mitume wa upendo wangu, ninawafundisha ya kuwa Mwanangu hatafuti sala tu pasipo kuchoka bali hata matendo na hisia. Salini ili katika sala mpate kuzidi katika imani na katika upendo. Mpendane wenyewe kwa wenyewe: hilo ndilo analotaka Yeye, hiyo ndiyo ni njia ya uzima wa milele. Wanangu, msisahau ya kuwa Mwanangu ameleta mwanga kwa ulimwengu huu. Ameuleta kwa wale ambao walitaka kuuona na kuupokea. Hawa muwe ninyi, maana huu ndio mwanga wa ukweli, wa amani na wa upendo. Mimi ninawaongoza kama mama kumwabudu Mwanangu, kumpenda pamoja nami. Fikira zenu, maneno na matendo yenu yamwelekee Mwanangu, yawe katika jina Lake: hapo tu moyo wangu utajazwa. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, kama Mama ambaye anajua wana wake, ninajua ya kuwa mnamtamani Mwanangu. Ninajua ya kuwa mnatamani ukweli, amani, na kilicho chema wala si uovu. Kwa sababu hiyo mimi, kama Mama, kwa njia ya upendo wa Mungu ninawaita ninyi na kuwaalika ili, mkisali kwa moyo safi na wazi, mmtambue ninyi wenyewe Mwanangu, upendo wake, na Moyo wake wenye rehema. Mwanangu alikuwa akiona uzuri katika vitu vyote. Yeye anatafuta mema, hata yale mema madogo yanayofichika, katika roho zote, ili kusamehe maovu. Kwa hiyo, wanangu, mitume wa upendo wangu, ninawaalika kumwabudu, kumshukuru daima na kumstahili. Maana yeye aliwaambieni maneno ya kimungu, maneno ya Mungu, maneno yaliyo kwa watu wote na hata milele. Kwa hiyo, wanangu, ishini uchangamfu, umakini, umoja na muwe na mapenzi baina yenu. Haya mnapaswa kuwa nayo katika ulimwengu wa leo: hivyo mtakuwa mitume wa upendo wangu, hivyo mtashuhudia Mwanangu kwa jinsi ya haki. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, kwa upendo wa kimama ninawaalika ili kwa moyo safi na wazi, kwa imani kabisa, mpokee upendo mkubwa wa Mwanangu. Mimi ninajua ukuu wa upendo wake, mimi nilimchukua ndani yangu, Hostia moyoni, Mwanga na Upendo wa ulimwengu. Wanangu, hata kuelekea kwangu kwenu ninyi ni ishara ya upendo na ya huruma ya Baba wa Mbinguni, ni tabasamu kilichojaa upendo wa Mwanangu, ni mwaliko kwa uzima wa milele. Damu ya Mwanangu ilimwagika kwa ajili yenu kwa upendo. Ile Damu yenye thamani ni kwa wokovu wenu, kwa ajili ya uzima wa milele. Baba wa mbinguni aliumba mtu kwa ajili ya furaha ya milele. Haiwezekani ninyi kufa, ninyi mnaojua upendo wa Mwanangu, ninyi mnaomfuata. Uzima umeshinda: Mwanangu yu hai! Kwa hiyo, wanangu, mitume wa upendo wangu, sala iwaonyeshe njia, jinsi ya kueneza upendo wa Mwanangu kwa jinsi ilivyo bora zaidi. Wanangu, hata wakati mnapojaribu kuishi maneno ya Mwanangu, ninyi mnasali. Wakati mnapowapenda watu mnaokutana nao, mnaeneza upendo wa Mwanangu. Upendo ni neno linalofungua milango ya Uzima. Wanangu, tangu awali nimesali kwa ajili ya Kanisa. Kwa hiyo ninawaalika nanyi, mitume wa upendo wangu, kusali kwa ajili ya Kanisa na watumishi wake, kwa wale ambao Mwanangu amewaita. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, Salini kila siku Tasbihi, taji lile la maua linaloniungana moja kwa moja kama Mama kwa maumivu yenu, mateso, mahitaji na matumaini. Mitume wa upendo wangu, Mimi nipo pamoja nanyi kwa njia ya neema na upendo wa Mwanangu, nanyi ninawaombeni sala. Sala zenu zinahitajika sana ulimwenguni, ili roho ziongoke! Fungueni wazi kwa imani timilifu mioyo yenu kwa Mwanangu, na yeye ataandika ndani yao muhtasari wa Neno lake, yaani upendo. Ishini muungano usiotenganika na Moyo Mtakatifu sana wa Mwanangu! Wanangu, kama Mama nawaambieni ya kwamba hakuna wakati wa kupoteza ili kupiga magoti mbele ya Mwanangu, kumkiri kama Mungu wenu, aliye kitovu cha maisha yenu. Mtoeni karama, zile anazozipenda zaidi, yaani upendo kwa jirani yako, rehema na mioyo safi. Mitume wa upendo wangu, wanangu wengi bado hawajamkiri Mwanangu kama Mungu wao, bado hawajajua upendo wake. Lakini ninyi, kwa njia ya sala yenu inayosema kwa moyo safi na wazi, pamoja na karama mnazotoa kwa Mwanangu, mtasababisha kwamba hata mioyo migumu zaidi ifunguke. Mitume wa upendo wangu, nguvu ya sala inayosemwa kutokana na moyo, ya sala yenye nguvu na iliyojaa upendo, hugeuza ulimwengu. Kwa hiyo, wanangu, salini, salini, salini! Mimi nipo pamoja nanyi.. Ninawashukuru.
Wanangu wapendwa, wakati huu uwe kwenu wakati wa sala. Bila Mungu hamwezi kuwa na amani. Kwa hiyo, wanangu, salini kwa ajili ya amani katika mioyo yenu na katika familia zenu ili Yesu aweze kuzaliwa ndani yenu na kuwapeni upendo wake na baraka yake. Ulimwengu uko katika vita kwa sababu mioyo imejaa machukio na wivu. Wanangu, wasiwasi unaonekana katika macho yenu kwa sababu hamkuruhusu Yesu kuzaliwa katika maisha yenu. Mtafuteni, ombeni na Yeye atajitoa kwenu katika yule Mtoto aliye furaha na amani. Mimi niko pamoja nanyi na ninasali pamoja nanyi. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, Leo ninawaalika kusali tena zaidi ili msikie katika mioyo yenu utakatifu wa msamaha. Katika familia lazima kuwepo utakatifu kwa sababu enyi wanangu, ulimwengu hauna wakati ujao bila upendo na utakatifu, kwa sababu katika utakatifu na katika furaha ninyi mjitolee kwa Mungu Mwumbaji anayewapendeni kwa upendo mkubwa sana. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, Katika wakati huu wa wasiwasi ambapo ibilisi anavuna nafsi ili kuwavuta kwake, niwaalika kwa sala ya kudumu ili katika sala mtambue Mungu wa upendo na wa matumaini. Wanangu, shikeni msalaba katika mikono yenu. Na uwatie moyo kwa kuwa upendo unashinda sikuzote hasa sasa ambapo msalaba na imani yamekataliwa. Ninyi muwe mwangwi na mfano kwa njia ya maisha yenu ya kuwa imani na matumaini bado hai na ulimwengu mpya wa amani unawezekana. Mimi nipo pamoja nanyi na ninawaombea mbele ya mwanangu Yesu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Wakati huu ndio wakati wa neema. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaalika tena, wanangu, mrudieni Mungu na kwa kusali ili sala iwe furaha kwenu. Enyi wanangu hamtakuwa na wakati ujao wala amani mpaka katika maisha yenu mtakapoanza kuishi maongezi ya binafsi na badiliko katika mema. Maovu yatakoma na amani itatawala katika mioyo yenu na katika ulimwengu. Kwa hiyo, wanangu, salini, salini, salini. Mimi nipo pamoja nanyi na ninawaombea kwa mwanangu Yesu kwa ajili ya kila mmoja wenu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Ninawatazama na kuwaalika: mrudieni Mungu maana Yeye ndiye upendo na kwa ajili ya upendo alinituma kwenu ili niwaongoze kwenye njia ya wongofu. Acheni dhambi na maovu, amueni kuwa watakatifu na furaha itatawala; nanyi mtakuwa mikono yangu iliyopanuliwa katika ulimwengu huu uliopotea. Ninatamani ya kuwa muwe sala na matumaini kwa wale ambao hawajamjua Mungu wa upendo. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Ninawaalika kuwa sala kwa wale wote wasiosali. Shuhudieni, wanangu, kwa njia ya maisha yenu furaha ya kuwa wangu na Mungu atajibu sala zenu na kuwapa amani katika ulimwengu huu wa wasiwasi ambamo kiburi na ubinafsi hutawala. Wanangu, ninyi muwe wakarimu na upendo wa upendo wangu ili wapagani wahisi ya kuwa ninyi ni wangu na waweze kuugeukia Moyo wangu Usio na dhambi ya asili. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Niko pamoja nanyi katika wakati huu wa rehema na ninawaalika nyote kuwa waleta amani na upendo katika ulimwengu huu, ambapo, wanangu, Mungu anawaalika kupitia Kwangu kuwa sala, upendo na kielelezo cha Paradiso, hapa duniani. Mioyo yenu na ijazwe na furaha na imani katika Mungu ili, wanangu, muwe na imani kamili katika mapenzi yake matakatifu. Hii ndiyo sababu mimi niko pamoja nanyi kwa sababu Yeye, Aliye Juu, ananituma kati yenu ili kuwahimiza ninyi kuwa na matumaini na mtakuwa waleta amani katika ulimwengu huu wenye wasiwasi. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Wakati huu na uunganishwe na sala kwa ajili ya amani na kwa matendo mema ili kusudi ionekane furaha ya kumngoja Mfalme wa amani mioyoni mwenu, ndani ya familia zenu na katika ulimwengu ambao hauna matumaini. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Ninawaletea Mwanangu ili aijaze mioyo yenu amani kwa sababu Yeye ni amani. Wanangu, mtafuteni Yesu katika ukimya wa mioyo yenu ili azaliwe upya. Ulimwengu unamhitaji Yesu, hivyo wanangu, mtafuteni kwa maombi maana anajitoa kila siku kwa kila mmoja wenu.
Mama yetu alikuja leo akiwa amevalia mavazi ya heshima akiwa na mtoto Yesu mikononi mwake. Yesu alinyoosha mkono wake kama ishara ya baraka na Mama yetu alituombea kwa lugha ya aramaika.
Wanangu wapendwa! Salini na mfanye upya moyo wenu ili lile jema mlilopanda lizae matunda ya furaha na ushirika na Mungu. Magugu yamechukua mioyo mingi na imekuwa tasa. Kwa hiyo ninyi, wanangu, muwe mwanga, upendo na mikono yangu iliyonyoshwa katika ulimwengu huu unaomtamani Mungu ambaye ni upendo. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
   




To compare Medjugorje messages with another language versions choose

For God to live in your hearts, you must love.

`