Our Lady of Medjugorje Messages containing 'kuwa'

Total found: 109
Wanangu wapendwa, upendo na wema wa Baba wa mbinguni yanatoa mafunuo ili kwamba imani ikue, iweze kuelezwa, ilete amani, salama na matumaini. Hivi mimi nami, wanangu, kwa ajili ya upendo wenye rehema wa Baba wa mbinguni ninawaonyesha sikuzote tena njia ya kwenda kwa Mwanangu, kwa wokovu wa milele; kwa bahati mbaya, lakini, wanangu wengi hawataki kunisikiliza. Wanangu wengi wanasita. Lakini mimi, mimi, katika wakati na zaidi ya wakati, sikuzote nimemtukuza Bwana kwa mambo yale yote aliyoyatenda ndani yangu na kwa njia yangu. Mwanangu anajitolea kwenu, anamega mkate pamoja nanyi, anawaambieni maneno ya uzima wa milele ili muweze kuwaletea watu wote. Nanyi, wanangu, mitume wa upendo wangu, mnaogopa nini, ikiwa Mwanangu ni pamoja nanyi? Mwonyesheni nafsi zenu, ili Yeye aweze kuwa ndani yao na aweze kuwafanyeni kuwa vyombo vya imani, vyombo vya upendo. Wanangu, ishini Injili, ishini upendo wenye rehema kuelekea mwenzenu; lakini hasa ishini upendo kuelekea Baba wa mbinguni. Wanangu, hamkuungana kwa bahati tu. Baba wa mbinguni haunganishi watu kwa bahati tu. Mwanangu anaongea na nafsi zenu, nami ninaongea moyoni mwenu. Kama Mama ninawaambia: tembeeni nami! Pendaneni, na kutoa shuhuda! Hampasi kuogopa kulinda Ukweli, ambao ni Neno la Mungu, lililo la milele na lisilogeuka kamwe, kwa mifano yenu. Wanangu, yule anayetenda kazi katika mwanga wa upendo wenye rehema na ukweli, anasaidiwa sikuzote na Mbingu na hayuko peke yake. Mitume wa upendo wangu, waweze kuwatambua sikuzote katikati ya wengine wote katika maficho, upendo na utulivu wenu. Mimi nipo pamoja nanyi. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, ninawaita mitume wa upendo wangu. Ninawaonyesha Mwanangu, aliye amani ya kweli na upendo wa kweli. Kama Mama, kwa ajili ya neema ya kimungu, ninatamani kuwaongoza kwendea Yeye. Wanangu, kwa hiyo ninawaalika kujitazama ninyi wenyewe mkianzia kwa Mwanangu, kumtazama kwa moyo na kuona kwa moyo mahali mlipo na maisha yenu yanakwenda wapi. Wanangu, ninawaalika kuelewa ya kuwa mnaishi kwa ajili ya Mwanangu, kwa njia ya upendo wake na sadaka yake. Ninyi mnamwomba Mwanangu kuwa mwenye rehema nanyi, lakini mimi ninawaalika ninyi kuwa na rehema. Mnamwomba kuwa mwema nanyi na kuwasamehe, lakini tangu lini mimi ninawasihi ninyi, wanangu, kusamehe na kupenda watu wote mnaokutana nao! Mtakapoelewa kwa moyo maneno yangu, mtaelewa na kujua upendo wa kweli, na mtaweza kuwa mitume wa upendo ule, enyi mitume wangu, wanangu wapendwa. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, kama Mama ambaye anajua wana wake, ninajua ya kuwa mnamtamani Mwanangu. Ninajua ya kuwa mnatamani ukweli, amani, na kilicho chema wala si uovu. Kwa sababu hiyo mimi, kama Mama, kwa njia ya upendo wa Mungu ninawaita ninyi na kuwaalika ili, mkisali kwa moyo safi na wazi, mmtambue ninyi wenyewe Mwanangu, upendo wake, na Moyo wake wenye rehema. Mwanangu alikuwa akiona uzuri katika vitu vyote. Yeye anatafuta mema, hata yale mema madogo yanayofichika, katika roho zote, ili kusamehe maovu. Kwa hiyo, wanangu, mitume wa upendo wangu, ninawaalika kumwabudu, kumshukuru daima na kumstahili. Maana yeye aliwaambieni maneno ya kimungu, maneno ya Mungu, maneno yaliyo kwa watu wote na hata milele. Kwa hiyo, wanangu, ishini uchangamfu, umakini, umoja na muwe na mapenzi baina yenu. Haya mnapaswa kuwa nayo katika ulimwengu wa leo: hivyo mtakuwa mitume wa upendo wangu, hivyo mtashuhudia Mwanangu kwa jinsi ya haki. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Wakati huu ndio wakati wa neema, wakati wa rehema kwa kila mmoja wenu. Wanangu, msiruhusu upepo wa chukio na hofu utawale ndani yenu na karibu nanyi. Ninyi, wanangu, mmealikwa kuwa upendo na sala. Ibilisi ataka hofu na fujo lakini ninyi, wanangu, muwe furaha ya Yesu Mfufuka ambaye amekufa na kufufuka kwa ajili ya kila mmoja wenu. Yeye ameshinda kifo kwa kuwapeni uzima, uzima wa milele. Kwa hiyo, wanangu, mshuhudieni na muwe wenye fahari kwa kufufuliwa katika Yeye. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, Mungu kwa rehema yake alinijalia kuwa pamoja nanyi, ili kuwaelimisha na kuwaongoza kuelekea katika hatua ya wongofu. Wanangu, ninyi nyote mmeitwa kusali kwa moyo wenu wote ili mpango wa wokovu utimilike ndani mwenu na kwa njia yenu. Jueni wanangu, kwamba maisha ni mafupi na uzima wa milele unawangoja kwa kadiri ya mastahili yenu. Kwa hiyo salini, salini, salini ili muweze kuwa vyombo vya kufaa mikononi mwa Mungu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, moyo safi na wazi tu utawawezesha ninyi kumjua kweli Mwanangu, na wale wote wasiojua upendo wake kuujua kwa njia yenu. Upendo tu utawawezesha kuelewa kuwa ni wenye nguvu kuliko kifo, maana upendo wa kweli umeshinda kifo na umefanya hata kifo hakipo tena. Wanangu, msamaha ni mtindo bora wa upendo. Ninyi, kama mitume wa upendo wangu, yawapasa kusali kwa kuwa wenye nguvu katika roho na kuweza kuelewa na kusamehe. Ninyi, mitume wa upendo wangu, kwa njia ya ufahamu na msamaha, mnatoa mfano wa upendo na rehema. Kuweza kuelewa na kusamehe ni karama inayotokana na maombi na yatupasa kuitunza. Mkisamehe ninyi mnaonyesha ya kuwa mnajua kupenda. Tazameni, wanangu, kama Baba wa mbinguni anavyowapenda kwa upendo mkubwa, kwa ufahamu, kwa uelewa, msamaha na haki. Kama anavyowatolea mimi, Mama wa mioyo yenu. Na tazama: mimi nipo katikati yenu ili kuwabariki kwa baraka ya kimama; ili kuwaalika kusali na kufunga; ili kuwasihi kuamini, kutumaini, kusamehe, kuwaombea wachungaji wenu na hasa kupenda bila mipaka. Wanangu, nifuateni! Njia yangu ni njia ya amani na upendo, njia ya Mwanangu. Ndiyo njia ya kuongoza katika ushindi wa Moyo wangu. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa, kufuatana na matakwa ya Baba mwenye rehema, nimewapa na tena nitawapa ishara dhahiri za uwepo wangu wa kimama. Wanangu, ishara hizo ni kwa hamu yangu ya kimama ya kuziponya roho. Ishara hizo ni kwa hamu ya kuwa kila mwanangu awe na imani ya kweli, aishi mang’amuzi ya ajabu akinywa kwenye chemchemi ya Neno la Mwanangu, Neno la uhai. Wanangu, kwa njia ya upendo wake na sadaka, Mwanangu alichukua ulimwenguni mwanga wa imani na aliwaonyesheni njia ya imani. Maana, wanangu, imani huamsha huzuni na maumivu. Imani ya kweli hufanya sala kusisika zaidi, hutimiza matendo ya huruma: mazungumzo na matoleo. Wale wanangu walio na imani, imani ya kweli, ni wenye heri pamoja na yote, maana wanaishi duniani mwanzo wa heri ya Mbinguni. Kwa hiyo, wanangu, mitume wa upendo wangu, ninawaalika kutoa mfano wa imani ya kweli, kupeleka mwanga pale palipo giza, kumwishi Mwanangu. Wanangu, kama Mama ninawaambia: hamwezi kupitia njia ya imani na kumfuata Mwanangu pasipo wachungaji wenu. Salini ili wawe na nguvu na upendo kwa kuwaongoza. Sala zenu ziwe sikuzote pamoja nao. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa, Upendo wa Mwanangu ni mkubwa. Laiti mngeweza kujua ukuu wa upendo Wake, msingeacha kamwe kumwabudu na kumshukuru. Yeye ni sikuzote hai pamoja nanyi katika Ekaristi, maana Ekaristi ni moyo Wake, Ekaristi ni moyo wa imani. Yeye hakuwaacha kamwe: hata wakati ninyi mlipojaribu kwenda mbali Naye, Yeye hakuwaacha kamwe.

Kwa hiyo, moyo wangu wa kimama unafurahi wakati unapotazama jinsi mlivyojaa upendo mnapomrudia, wakati unapoona ya kuwa mnamrudia kwa njia ya upatanisho, upendo na matumaini. Moyo wangu wa kimama unajua ya kuwa ikiwa mngetembea katika njia ya imani, mngekuwa kama machipukizi, kama matumba na kwa njia ya sala na kufunga mngekuwa kama matunda, kama maua, mitume wa upendo wangu, mngekuwa waleta mwanga na mngeangaza kwa upendo na hekima pande zote karibu nanyi.

Wanangu, kama mama, ninawaomba: salini, fikirini na kutafakari. Yote yanayowatokea, mazuri, ya kuumiza na ya kufurahisha, hayo yote yawasababisha kukua kiroho, yawafanya kuwa Mwanangu akue ndani yenu. Wanangu mkabidhi kwake. Mumwamini na mtumainie upendo Wake. Na Yeye awaongoze. Na Ekaristi iwe mahali mtakapolisha roho zenu ili kueneza upendo na ukweli. Shuhudieni Mwanangu. Ninawashukuru.
Wanangu wapendwa, Fanyeni kazi na shuhudieni kwa upendo Ufalme wa Mbinguni ili muweze kuwa hamjambo hapa duniani. Wanangu, Mungu atabariki mara mia zaidi juhudi yenu na mtakuwa mashahidi katikati ya watu, roho za wale wasioamini zitahisi neema ya wongofu na Mbingu itazipokea taabu zenu na sadaka zenu. Wanangu, shuhudieni kwa tasbihi mkononi ili muwe wangu na kateni shauri kuwa watakatifu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, mapenzi na upendo wa Baba wa mbinguni hufanya mimi niwe katikati yenu, ili kusaidia kwa upendo wa kimama ukuaji wa imani katika mioyo yenu, ili kwamba muweze hakika kuelewa lengo la maisha ya kidunia na ukuu wa yale ya kimbingu. Wanangu, maisha ya kidunia ndiyo njia kuelekea umilele, kuelekea ukweli na uzima: kuelekea kwa Mwanangu. Kwa njia hii nataka kuwaongoza. Ninyi, wanangu, ninyi wenye sikuzote kiu ya upendo mkubwa zaidi, ukweli na imani, mjue ya kuwa moja tu ni chemchemi mnakoweza kunywa: imani katika Baba wa mbinguni, imani katika upendo wake. Mtegemee kabisa mapenzi yake wala msiogope: kila lililo bora kwa ajili yenu, kila linalowachukua kwenye uzima wa milele, mtapewa! Mtaelewa ya kuwa lengo la maisha si sikuzote kutaka na kutwaa, lakini kupenda na kutoa; mtakuwa na amani ya kweli na upendo wa kweli, mtakuwa mitume wa upendo. Kwa mfano wenu, mtawafanya wale wanangu wasiomjua Mwanangu na upendo wake watake kumjua. Wanangu, mitume wa upendo wangu, mwabuduni Mwanangu pamoja nami, na mpendeni juu ya vyote. Jaribuni sikuzote kuishi katika ukweli wake. Ninawashukuru.
Wanangu wapendwa, wakati huu uwe kwenu wakati wa sala. Bila Mungu hamwezi kuwa na amani. Kwa hiyo, wanangu, salini kwa ajili ya amani katika mioyo yenu na katika familia zenu ili Yesu aweze kuzaliwa ndani yenu na kuwapeni upendo wake na baraka yake. Ulimwengu uko katika vita kwa sababu mioyo imejaa machukio na wivu. Wanangu, wasiwasi unaonekana katika macho yenu kwa sababu hamkuruhusu Yesu kuzaliwa katika maisha yenu. Mtafuteni, ombeni na Yeye atajitoa kwenu katika yule Mtoto aliye furaha na amani. Mimi niko pamoja nanyi na ninasali pamoja nanyi. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, ninapowatazama ninyi mnaopenda Mwanangu, furaha inajaza Moyo wangu. Ninawabariki kwa baraka ya kimama. Pamoja na baraka ya kimama ninawabariki hata wachungaji wenu: ninyi mnaotangaza maneno ya Mwanangu, mnaobariki kwa mikono yake na mnaompenda hata kuwa tayari kufanya kwa furaha kila sadaka kwa ajili yake. Ninyi mfuateni Yeye, aliyekuwa Mchungaji wa kwanza, Mmisionari wa kwanza. Wanangu, mitume wa upendo wangu, kuishi na kufanya kazi kwa ajili ya wengine, kwa wale wote mnaopenda kwa njia ya Mwanangu, ni furaha na faraja ya maisha ya kidunia. Ikiwa kwa njia ya sala, upendo na sadaka Ufalme wa Mungu ni katika mioyo yenu, hapo kwa ninyi maisha ni yenye furaha na matulivu. Katikati ya wale wanaompenda Mwanangu na wanaopendana kwa ajili yake, maneno si ya lazima. Kutazamana kwatosha ili kusikia maneno yasiyonenwa na hisia zisizoonyeshwa. Pale panapotawala upendo, wakati hauna maana tena. Sisi ni pamoja nanyi! Mwanangu anawajua na kuwapenda. Upendo ni kilichowaongoza kwangu na, kwa njia ya upendo huu, mimi nitakuja kwenu na nitawaambieni kazi za wokovu. Ninataka ya kuwa wana wangu wote wawe na imani na wahisi upendo wangu wa kimama unaowaongoza kwa Yesu. Kwa hiyo ninyi, wanangu, ko kote mwendako angazeni kwa upendo na kwa imani, kama mitume wa upendo. Ninawashukuru.
Wanangu wapendwa, nilichaguliwa kuwa mama wa Mungu na mama yenu, kwa maamuzi na upendo wa Bwana, lakini pia kwa mapenzi yangu, kwa upendo wangu usio na kifani kwake Baba wa mbinguni na kwa imani yangu yote Kwake. Mwili wangu ulikuwa kikombe cha Mungu Mtu. Nilikuwa mtumishi wa ukweli, wa upendo na wokovu kama vile nilivyo sasa katikati yenu, ili kuwaalika, wanangu, mitume wa upendo wangu, kuwa waletaji ukweli, ili kuwaalika, kwa njia ya utashi na upendo yenu kumwelekea Mwanangu, ili kueneza maneno Yake, maneno ya wokovu na kuyaonyesha, kwa vitendo vyenu, kwa wale wote ambao hawajamjua mwanangu na upendo Wake. Nguvu mtaipata katika Ekaristi: Mwanangu awalisheni kwa mwili Wake na kuwaimarisha kwa damu Yake. Wanangu, wekeni mikono yenu pamoja kwa sala na tazameni kuelekea msalaba kwa ukimya. Kwa jinsi hii mtapata imani ili muweze kuieneza, mtapata ukweli ili muweze kuupambanua, mtapata upendo ili muweze kuelewa namna ya kupenda kwa uhakika. Wanangu, mitume wa upendo wangu, wekeni mikono yenu pamoja kwa sala na tazameni kuelekea msalaba: katika msalaba tu kuna wokovu. Ninawashukuru.
Wanangu wapendwa, katika miaka hii yote mimi nipo pamoja nanyi ili kuwaongoza kwenye njia ya wokovu. Rudieni kwa Mwanangu, rudieni katika sala na mfungo. Wanangu, mwachieni Mungu aongee na mioyo yenu kwa sababu shetani anatawala na anatamani kuangamiza maisha yenu na dunia mnamotembelea. Muwe na ujasiri na amueni kuwa watakatifu. Mtaona wongofu katika mioyo yenu na katika familia zenu, sala itasikilizwa, Mungu atayapokea maombi yenu na kuwapa amani. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwabariki nyote kwa baraka yangu ya kimama. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, wakati huu uwe kwenu himizo kwa wongofu wenu binafsi. Wanangu, ombeni katika upweke Roho Mtakatifu ili iwaimarishe katika imani na katika kumsadiki Mungu ili kuweza kuwa mashahidi wa upendo ambao Mungu anawapa kupitia uwepo wangu. Wanangu, msiruhusu majaribu yafanye mioyo yenu kuwa migumu na sala kuwa kama jangwa. Muwe mwangi wa upendo wa Mungu na mshuhudieni Yesu Aliyefufuka kwa njia ya maisha yenu. Mimi nipo pamoja nanyi na ninawapenda nyote kwa upendo wangu wa kimama. Asanteni kwa kuitikia wito wangu”.
Wanangu wapendwa, Katika wakati huu wa wasiwasi ambapo ibilisi anavuna nafsi ili kuwavuta kwake, niwaalika kwa sala ya kudumu ili katika sala mtambue Mungu wa upendo na wa matumaini. Wanangu, shikeni msalaba katika mikono yenu. Na uwatie moyo kwa kuwa upendo unashinda sikuzote hasa sasa ambapo msalaba na imani yamekataliwa. Ninyi muwe mwangwi na mfano kwa njia ya maisha yenu ya kuwa imani na matumaini bado hai na ulimwengu mpya wa amani unawezekana. Mimi nipo pamoja nanyi na ninawaombea mbele ya mwanangu Yesu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Mimi ni pamoja nanyi kwa muda mrefu kwa maana Mungu ni mkuu katika upendo wake na katika uwepo wangu. Wanangu, ninawaalika kurudi kwa Mungu na kwa sala. Kipimo cha kuishi kwenu kiwe upendo na msisahau, wanangu, kwamba maombi na kufunga hufanya miujiza ndani yenu na kuwazunguka. Yote mnayoyafanya yawe kwa ajili ya utukufu wa Mungu na hapo Mbingu itajaza moyo wenu na furaha mkahisi ya kuwa Mungu anawapenda na kunituma ili kuokoa ninyi na Dunia ambayo juu yake mnaishi. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Ninawaletea Mtoto Yesu anayewaletea amani, Yule aliye wakati uliopita, wakati wa sasa na wakati ujao wa kuishi kwenu. Wanangu, msiruhusu imani yenu na matumaini yenu katika wakati ujao ulio bora yazimike, kwa maana ninyi mmechaguliwa kwa kuwa mashahidi wa matumaini katika kila hali. Kwa ajili hiyo mimi ni hapa pamoja na Yesu ili awabariki kwa amani yake. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Katika wakati huo ninawaalika kusali, kufunga na kujikana ili muweze kuwa wenye nguvu zaidi katika imani. Huu ni wakati wa mwamko na wa kuzaliwa upya. Kama vitu vya asili vinavyojitoa nanyi wanangu, fikirini juu ya mambo mliyopokea. Muwe waletaji wa amani na wa upendo wenye furaha ili kuishi vizuri duniani. Tamanini Mbingu kwa sababu Mbinguni hakuna wala huzuni wala machukio. Kwa hiyo, wanangu, amueni tena kuongoka, na utakatifu utawale katika maisha yenu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Mungu ameniruhusu kuwa pamoja nanyi leo pia kwa kuwaalika kusali na kufunga. Ishini wakati huu wa neema na muwe mashahidi wa tumaini maana, ninawaambia tena wanangu, kwa kusali na kufunga hata vita vinaweza kuisha. Wanangu, aminini na kuishi katika imani na kwa imani wakati huu wa neema na Moyo wangu usio na dhambi ya asili haumwachi yeyote kati yenu katika wasiwasi ikiwa ananikimbilia. Ninawaombea mbele ya Yeye aliye juu na ninasali ili amani iwepo katika mioyo yenu na kwa ajili ya tumaini katika wakati ujao. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
   




To compare Medjugorje messages with another language versions choose

For God to live in your hearts, you must love.

`