Our Lady of Medjugorje Messages containing 'wachungaji'

Total found: 46
Wanangu wapendwa, ninyi ni nguvu yangu. Ninyi, mitume wangu, ambao, kwa upendo wenu, unyenyekevu na sala ya kimya kimya, mnamwezesha Mwanangu ajulikane. Ninyi mnaishi ndani yangu. Ninyi mnanibeba mioyoni mwenu. Ninyi mnajua ya kuwa mna Mama awapendaye na aliyekuja kuwaletea upendo. Nawatazama katika Baba wa Mbinguni, natazama fikira zenu, maumivu yenu, mateso yenu na kuyaleta kwa Mwanangu. Msiogope! Msipoteze matumaini, maana Mwanangu humsikiliza Mama yake. Yeye hupenda tangu alipozaliwa, na ndio furaha yangu ya kuwa wanangu wote wajue upendo huo; na wote wale ambao, kwa sababu ya maumivu yao na kutoelewa kwao, walimwacha waweze kurudi kwake, na wote wao wasiomjua wamjue. Kwa sababu hiyo ninyi hapa ni mitume wangu, nami pia pamoja nanyi kama Mama yenu. Salini ili kuwa imara katika imani, maana upendo na rehema hutoka katika imani imara. Kwa njia ya upendo na rehema mtawasaidia wale wote wasiofahamu ya kuwa wanachagua giza badala ya nuru. Salini kwa ajili ya wachungaji wenu, maana wao ni nguvu ya Kanisa ambayo Mwanangu aliwaachieni. Kwa njia ya Mwanangu wao ni wachungaji wa roho. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, fungueni mioyo yenu mkajaribu kuhisi jinsi ninavyowapenda na kutaka mpendeni Mwanangu. Nataka mpende zaidi kwa kuwa haiwezekani kumjua pasipo kumpenda, maana Yeye ndiye upendo. Wanangu, mimi nawajueni: najua maumivu yenu na mateso yenu maana niliyaishi. Nafurahi pamoja nanyi kwa furaha zenu. Nalia machozi pamoja nanyi katika maumivu yenu. Sitawaacheni kamwe. Nitaongea nanyi daima kwa upole wa kimama na, kama mama, nahitaji mioyo yenu ifumbuliwe, ili kwa hekima na unyofu mueneze upendo wa Mwanangu. Nawahitaji ninyi mfumbuliwe na kuwa wepesi kupokea mema na huruma. Nahitaji muungano wenu na Mwanangu, kwa maana nataka mpate kufanikiwa na kumsaidia kuleta heri kwa wanangu wote. Mitume wangu, nawahitaji, ili muwaonyeshe wote ukweli wa Mungu, ili moyo wangu, ulioteswa na kuteswa hata leo kupita kiasi, uweze kushinda katika upendo. Salini kwa ajili ya utakatifu wa wachungaji wenu, ili katika jina la Mwanangu, waweze kutenda maajabu, maana utakatifu hutenda maajabu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nataka kufanya kazi kwa njia yenu, wanangu, mitume wangu, ili mwishowe niweze kukusanya wanangu wote pale ambapo pameandaliwa tayari kwa ajili ya furaha yenu. Nawaombea, kusudi kwa matendo yenu muweze kugeuza, kwani muda umefika kwa matendo ya kweli, kwa ajili ya Mwanangu. Upendo wangu utafanya kazi ndani mwenu, nitawatumia ninyi. Muwe na imani nami, kwani yote ninayotamani, ninayatamani kwa ajili yenu, wema wa milele, ulioumbwa kwa njia ya Baba wa Mbinguni. Ninyi, wanangu, mitume wangu, muishi maisha ya duniani pamoja na wanangu ambao hawafahamu upendo wa Mwanangu, wale ambao hawaniiti mama. Lakini msiogope kushuhudia ukweli, kwa maana ikiwa ninyi hamtaogopa na kushuhudia ukweli kwa uhodari, ukweli utashinda kimuujiza. Kumbukeni: nguvu iko katika upendo. Wanangu, upendo ndio kutubu, kusamehe, kusali, kujitoa sadaka na rehema, maana mkijua kupenda kwa matendo mtawabadilisha na wengine, mtawezesha mwanga wa Mwanangu uingie katika mioyo yao. Nawashukuru. Muwaombee wachungaji wenu, wao ni mali ya Mwanangu. Yeye aliwaita. Salini ili wawe siku zote na nguvu na uhodari wa kung'aa kwa nuru ya Mwanangu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nawaalika kueneza imani katika Mwanangu, imani yenu. Ninyi wanangu, mlioangazwa na Roho Mtakatifu, mitume wangu, itangazeni imani kwa watu wengine, yaani kwa wasiosadiki, wasioijua na wasiotaka kuijua. Kwa sababu hiyo yawapasa kusali sana kwa ajili ya zawadi ya upendo, maana upendo ndio alama maalum ya imani ya kweli, na ninyi mtakuwa mitume wa upendo wangu. Upendo hufanya upya daima maumivu na furaha ya Ekaristi, hufanya upya maumivu ya Mateso ya Mwanangu, aliyewaonyesha upendo usio na kifani; hufanya upya furaha ya tendo la kuwaachia Mwili wake na Damu yake kwa ajili ya kuwalisha na hivyo kuwa kitu kimoja nanyi. Nikiwaangalia kwa wema nahisi upendo pasipo kiasi, ulioniimarisha katika hamu yangu ya kuwaongoza katika imani thabiti. Imani thabiti itawapa furaha na uchangamfu duniani, na mwishowe kuwaunganisha na Mwanangu. Hiyo ndiyo hamu yake. Kwa hiyo mwishi katika Yeye, na katika upendo, isheni katika nuru iliyowaangaza daima katika Ekaristi. Nawaombeni kusali sana kwa wachungaji wenu, kusali ili kupata upendo mkubwa kwa ajili yao, kwa maana Mwanangu aliwapeni ili waweze kuwalisha kwa Mwili wake na kuwafundisha upendo. Kwa hiyo wapendeni ninyi pia! Lakini, wanangu, kumbukeni: upendo maana yake ni kuvumilia na kutoa na kutohukumu kamwe. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, mimi, kama Mama apendaye wanawe, natambua jinsi ulivyo mgumu muda huu mnaouishi. Naona mateso yenu, lakini jueni kwamba hamko peke yenu: Mwanangu yu pamoja nanyi! Yeye yupo popote, asiyeonekana, lakini mtaweza kumwona ikiwa mtamwishi. Yeye ndiye nuru inayoangaza roho yenu na kuleta amani. Yeye ndiye Kanisa, mnalopaswa kulipenda, kuliombea na kulilinda daima: si kwa maneno tu, bali kwa matendo ya upendo. Wanangu, fanyeni yote ili Mwanangu ajulikane kwa watu wote, na aweze kupendwa, kwa maana ukweli ni katika Mwanangu, aliyezaliwa na Mungu, Mwana wa Mungu. Msipoteze muda kwa kufikiri mno; mtajitenganisha na ukweli. Pokeeni Neno lake kwa moyo mnyofu na kuliishi. Mkiishi Neno lake, mtasali. Mkiishi Neno lake, mtapenda kwa upendo wenye huruma, na mtapendana. Kwa kadiri mtakavyokuwa na upendo hivyo ndivyo mtakavyokuwa mbali na kifo. Kwa wale watakaoishi na kulipenda Neno la Mwanangu, kifo kitakuwa uhai kwao. Nawashukuru! Salini kwa ajili ya kuweza kuona Mwanangu katika wachungaji wenu. Salini kwa ajili ya kuweza kumkumbatia katika wao.
Wanangu wapendwa, nipo hapa katikati yenu kuwatieni moyo, kuwajaza kwa upendo wangu, kuwaalika tena kuwa mashahidi wa upendo wa Mwanangu. Wanangu wengi hawana tumaini, hawana amani, hawana upendo. Wao wanatafuta Mwanangu lakini hawajui jinsi wala wapi ya kumpata. Mwanangu awafungulia mikono Yake, nanyi wasaidieni ili waje mikononi Mwake. Wanangu, kwa hiyo ni lazima msali kwa upendo, lazima msali sana, sana, ili kupata upendo zaidi na zaidi, kwa maana upendo hushinda mauti na hudumisha maisha. Watume wa upendo wangu, wanangu wenye moyo mnyofu na safi, jiungeni zaidi na zaidi katika kusali. Mnatengana sana! Jipeni moyo katika kukua kiroho, kama vile Mimi ninawapeni moyo. Ninawaangalia na nipo karibu nanyi kila mnaponifikiria. Waombeeni wachungaji wenu, wale walioacha yote kwa ajili ya Mwanangu. Wapendeni na waombeeni, Baba wa Mbinguni husikiliza sala zenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, mimi ni sikuzote pamoja nanyi, kwa maana Mwanangu alinikabidhi ninyi. Nanyi, wanangu, mnanihitaji mimi, mnitafute, mnijie na mfurahishe Moyo wangu wa kimama. Mimi ninawapenda na nitawapenda ninyi mnaoteseka na kutolea mateso yenu kwa ajili ya Mwanangu na kwa ajili yangu. Upendo wangu hutafuta upendo wa wanangu wote na wanangu wote hutafuta upendo wangu. Kwa njia ya upendo Yesu hutafuta ushirika kati ya Mbingu na dunia, kati ya Baba wa mbinguni na ninyi, wanangu, Kanisa lake. Kwa hiyo lazima kusali sana, kusali na kulipenda Kanisa ambalo ninyi ni wake. Sasa Kanisa linateseka na kuhitaji mitume ambao, wakipenda ushirika, wanaposhuhudia na kutoa, waonyeshe njia za Mungu. Kanisa linahitaji mitume ambao, wakiishi Ekaristi kwa moyo, watende matendo makuu. Kanisa linawahitaji ninyi, mitume wangu wa upendo. Wanangu, Kanisa limeteswa na kusalitiwa tangu siku zake za awali, lakini linazidi kukua siku hata siku. Kanisa halitaharibiki, kwa maana Mwanangu alilipa moyo: Ekaristi. Nuru ya ufufuo wake imeng’aa na itang’aa juu yake. Kwa hiyo msiogope! Waombeeni wachungaji wenu, ili wawe na nguvu na upendo kwa kuwa madaraja ya wokovu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, msiwe na mioyo migumu, iliyofungwa na iliyojaa hofu. Pokeeni upendo wangu wa kimama uiangaze na kuijaza mioyo yenu upendo na matumaini, ili, kama Mama, niyalainishe maumivu yenu: ninayajua, na nimeyaonja. Maumivu huinua nayo ni sala kuu kuliko zote. Mwanangu huwapenda hasa wanaopokea maumivu. Alinituma Mimi niyalainishe na kuwaletea matumaini. Mumwamini Yeye. Najua kuwa ni vigumu kwenu, maana mnaona giza linalozidi kuongeza karibu yenu pande zote. Wanangu, giza mtalivunja kwa njia ya sala na upendo. Yule anayesali na kupenda haogopi, ana matumaini na upendo wenye huruma: Anaona mwanga, na anamwona Mwanangu. Kama mitume wangu nawaalika mjaribu kuwa mfano wa upendo wenye huruma na wenye matumaini. Salini sikuzote tena kwa ajili ya kupata upendo mwingi kadiri muwezavyo, maana upendo huleta mwanga unaovunja kila giza, na humleta Mwanangu. Msiogope, ninyi si peke yenu: Mimi nipo pamoja nanyi! Ninawasihi waombeeni wachungaji wenu, ili wawe na upendo kila wakati na wawe na matendo ya upendo kwa Mwanangu, kwa njia yake na kwa kumkumbuka Yeye. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, kama Mama wa Kanisa, kama Mama yenu, ninatabasamu nikiwaona kunijia, kukusanyika kandokando yangu na kunitafuta. Ujio wangu katikati yenu ni onyesho la kadiri Mbingu inavyowapenda. Ujio wangu unawaonyesha njia ya kuelekea kwenye uzima wa milele, kuelekea wokovu. Mitume wangu, ninyi mnaojaribu kuwa na moyo safi na Mwanangu ndani yake, ninyi mpo katika njia njema. Ninyi mnamtafuta Mwanangu, mnatafuta njia njema. Yeye aliacha dalili nyingi za upendo wake. Ameacha tumaini. Ni rahisi kumpata, ikiwa mpo tayari kujitolea na kutubu, ikiwa mtakuwa na uvumilivu, rehema na upendo kwa jirani. Wanangu wengi hawaoni wala hawasikii maana hawataki. Hawapokei maneno na matendo yangu, lakini Mwanangu, kwa njia yangu, anawaalika wote. Roho yake huangaza wote katika mwanga wa Baba wa Mbinguni, katika ushirika kati ya Mbingu na dunia, katika upendano; maana upendo huita upendo na kutenda ili matendo yawe muhimu kuliko maneno. Kwa hiyo, mitume wangu, mliombee Kanisa lenu, lipende na tendeni matendo ya upendo. Ingawa limesalitiwa na kujeruhiwa, lipo hapa kwa sababu hutoka kwa Baba wa Mbinguni. Muwaombeeni wachungaji wenu, ili kuona ndani yao ukuu wa upendo wa Mwanangu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nimekuja kwenu, katikati yenu, ili mnipe mahangaiko yenu, niweze kuyaleta mbele ya Mwanangu na kuwaombeeni kwake kwa manufaa yenu. Najua kuwa kila mmoja wenu ana mahangaiko yake, majaribu yake. Kwa hiyo kwa moyo wa kimama nawaalikeni: Njooni kwenye Meza ya Mwanangu! Yeye humega mkate kwa ajili yenu, huwapa Yeye mwenyewe. Huwapa matumaini. Anawaomba kuwa na imani zaidi, matumaini zaidi, utulivu zaidi. Anawaomba mpigane ndani yenu dhidi ya ubinafsi, hukumu na udhaifu wa kibinadamu. Kwa hiyo Mimi, kama Mama, nawaambieni: salini, maana sala huwapa nguvu ya kupigana ndani yenu. Mwanangu, alipokuwa mtoto, aliniambia mara nyingi ya kuwa wengi watanipenda na kuniita "Mama". Mimi hapa, katikati yenu, nasikia upendo na kuwashukuru! Kwa njia ya upendo huu namwomba Mwanangu ili hakuna hata mmoja wenu, wanangu, arudiye nyumbani jinsi alivyokuja. Ili mlete matumaini, rehema na upendo kadiri muwezavyo; ili muwe mitume wa upendo wangu, wanaoshuhudia kwa maisha yao kwamba Baba aliye Mbinguni ni chemchemi ya uzima si ya mauti. Wanangu wapendwa, nawaomba tena kwa moyo wa kimama: waombeeni wateule wa Mwanangu, kwa ajili ya mikono yao iliyobarikiwa, kwa ajili ya wachungaji wenu, ili waweze kumhubiri Mwanangu kwa upendo mwingi wawezavyo, na hivyo kusababisha wongofu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, kulingana na mapenzi ya Mwanangu na upendo wangu wa kimama naja kwenu, wanangu, hasa kwa wale ambao hawajajua bado upendo wa Mwanangu. Ninakuja kwenu mnaonifikiria, mnaoomba msaada wangu. Ninawapa upendo wangu wa kimama na kuwaletea baraka ya Mwanangu. Mnayo mioyo safi na wazi? Mnaona dalili za uwepo wangu na upendo wangu? Wanangu, katika maisha yenu ya dunia igieni moyo na mfano wangu. Maisha yangu yalikuwa maumivu, ukimya, imani na matumaini pasipo mipaka katika Baba wa Mbinguni. Hakuna kitu cha bahati: si maumivu, si furaha, si mateso, si upendo. Hizo zote ni neema ambazo Mwanangu anawapeni na zinazowaongoza kwenye uzima wa milele. Mwanangu anawaomba mapendo na sala ndani yake. Kupenda na kusali ndani yake maana yake — kama Mama nataka kuwafundisha — ni kusali katika ukimya wa nafsi zenu, si kusema kwa midomo tu. Ni tendo dogo zuri litendwalo kwa jina la Mwanangu; ni uvumilivu, rehema, upokeaji wa maumivu na kujitolea kwa ajili ya wengine. Wanangu, Mwanangu huwatazama. Ombeni ili ninyi pia muuone uso wake, na ili uso huo uweze kufunuliwa kwenu. Wanangu, mimi nawafunulia ukweli halisi wa pekee. Salini kwa kuyaelewa na kuweza kueneza mapendo na matumaini, kwa kuweza kuwa mitume wa upendo wangu. Moyo wangu wa kimama hupenda hasa wachungaji. Iombeeni mikono yao iliyobarikiwa. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, Roho Mtakatifu, kwa njia ya Baba wa Mbinguni, amenifanya Mama: Mama wa Yesu na, kwa hiyo, Mama yenu vilivile. Kwa hiyo nawajilia niwasikilize, niwafungulie mikono yangu ya kimama, niwapeni Moyo wangu na kuwaalika kukaa pamoja nami, kwa maana kutoka juu ya msalaba Mwanangu amenikabidhi ninyi. Kwa bahati mbaya wanangu wengi hawakujua upendo wa Mwanangu, wengi hawataka kumjua. Loo, wanangu, mabaya mengi yatoka kwa wale ambao hawana budi ya kuona na kuelewa ili kuamini! Kwa hiyo, wanangu, mitume wangu, katika kimya ya moyo wenu sikilizeni sauti ya Mwanangu, ili moyo wenu uwe makazi yake wala usiwe giza na huzuni, bali uangaziwe na mwanga wa Mwanangu. Tafuteni matumaini kwa imani, maana imani ni maisha ya roho. Ninawaalika tena: salini! Salini ili kuishi imani katika unyenyekevu, katika amani ya kiroho na mkiangaziwa na mwanga. Wanangu, msijaribu kuelewa yote mara moja, maana Mimi nami sikuelewa yote mara moja, lakini niliyaamini maneno ya kimungu aliyoyasema Mwanangu, Yeye aliyekuwa mwanga wa kwanza na mwanzo wa Ukombozi. Enyi mitume wa moyo wangu, ninyi mnaosali, mnaojitolea, mnaopenda wala msiohukumu: ninyi nendeni mkaeneze ukweli, maneno ya Mwanangu, Injili. Ninyi kweli, ni Injili iliyo hai, ninyi ni miali ya mwanga wa Mwanangu. Mwanangu na mimi tutakuwa karibu nanyi, tutawatia moyo na kuwajaribu. Wanangu, ombeeni daima na hasa baraka ya wale ambao Mwanangu amebariki mikono yao, yaani Wachungaji wenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, Mwanangu alikuwa chemchemi ya upendo na mwanga alipoongea na watu wa mataifa yote. Mitume wangu, fuateni mwanga wake, si rahisi, yawapasa kuwa wadogo, yawapasa kuwa wadogo kuliko wengine wote na kwa msaada wa imani kujazwa na upendo wake. Hakuna mtu duniani, pasipo imani, awezaye kuwa na uzoefu wa mwujiza. Mimi nipo pamoja nanyi, ninajionyesha kwa matokeo hayo, kwa maneno hayo, nataka kuwashuhudia upendo wangu na utunzaji wangu wa kimama. Wanangu, msipoteze wakati mkiweka maswali ambayo hamtapata kamwe majibu, maisha yenu duniani yatakapomalizika Baba wa Mbinguni atawajibu. Mjue daima ya kuwa Mungu hujua yote, Mungu huona, Mungu hupenda. Mwanangu mpenzi sana huangaza maisha na kupasua giza. Upendo wa kimama unaonileta kwenu hauelezeki, umefichwa lakini ni halisi, ninawaonyesheni hisia zangu, upendo, hisani na ukarimu wangu wa kimama. Kutoka kwenu, mitume wangu, ninatafuta sala zenu: mawaridi yaliyo matendo ya upendo, hizo ndizo kwa moyo wangu wa kimama sala za kunipendeza sana, haya ninayaletea Mwanangu aliyezaliwa kwa ajili yenu. Yeye anawatazama ninyi na kuwasikia. Sisi tupo kila siku karibu nanyi kwa upendo wenu ambao huita, huunga, huongoa, hutia moyo na kujaza. Kwa hiyo mitume wangu pendaneni daima, lakini hasa mpende Mwanangu, hii ni njia ya pekee ya wokovu kuelekea uzima wa milele, hiyo ni sala ya kunipendeza ambayo kama harufu nzuri ajabu ya mawaridi, hujaa moyo wangu. Ombeni daima, waombeeni wachungaji wenu ili wapate nguvu ya kuwa mwanga wa Mwanangu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, mitume wa upendo wangu, inawapasa ninyi kuujulisha upendo wa Mwanangu kwa wale wote ambao hawakumjua. Inawapasa ninyi, mianga midogo ya ulimwengu, ambao mimi ninaifunza kwa upendo wa kimama ili ing'ae waziwazi kwa mwangaza kamili. Sala itawasaidia, maana sala huwaokoa ninyi, sala huuokoa ulimwengu. Kwa hiyo, wanangu, salini kwa maneno, kwa moyo, kwa upendo wenye huruma na kwa sadaka. Mwanangu aliwaonyesha njia: Yeye aliyejimwilisha na kunifanya kuwa kalisi ya kwanza; Yeye ambaye kwa sadaka yake isiyo na kifani aliwaonyesha kama inavyopaswa kupenda. Kwa hiyo, wanangu, msiogope kusema kweli. Msiogope kujigeuza wenyewe na ulimwengu ili kueneza mapendo, mkitenda kila jinsi kusudi Mwanangu aweze kujulikana na kupendwa kwa kuwapenda wengine kwa ajili yake. Mimi, kama mama, nipo daima pamoja nanyi. Namwomba Mwanangu awasaidie ili katika maisha yenu upendo utawale: upendo uishio, upendo uvutao, upendo utoao uzima. Huo ndio upendo ninaowafundisha, upendo safi. Inawapasa ninyi, mitume wangu, kuutambua, kuuishi, kuueneza. Waombeeni wachungaji wenu kwa moyo, ili waweze kumshuhudia Mwanangu kwa upendo. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nawaalika kusali pasipo kuomba, bali mkitoa sadaka, mkijitolea wenyewe. Nawaalika kuleta habari ya ukweli na upendo wenye rehema. Ninamwomba Mwanangu kwa ajili yenu, kwa imani yenu, inayoendelea kupunguka katika mioyo yenu. Ninamwomba awasaidieni kwa Roho ya Mungu, kama vile mimi nami ninavyotaka kuwasaidieni kwa roho ya kimama. Wanangu, itawabidi kujiboresha! Wale tu walio safi, wanyenyekevu na wamliojaa upendo wanautegemeza ulimwengu, wanaokoa ulimwengu na wao wenyewe. Wanangu, Mwanangu ndiye moyo wa ulimwengu: lazima kumpenda na kumwomba, na si kumsaliti daima tena. Kwa hiyo ninyi, mitume wa upendo wangu, mstawishe imani katika mioyo ya watu kwa mfano wenu, kwa sala yenu na kwa upendo wenye rehema. Mimi nipo karibu nanyi na nitawasaidia. Salini ili wachungaji wenu wapate mwanga zaidi kadiri wawezavyo, ili waweze kuangaza wale wote wanaoishi gizani. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, ninaongea nanyi kama Mama, kwa maneno rahisi, lakini yamejaa wingi wa upendo na wa bidii kwa wanangu, ambao kwa njia ya Mwanangu wamekabidhiwa kwangu. Mwanangu, ambaye anakuja kutoka umilele na hata sasa, anaongea nanyi kwa maneno ya uzima na anapanda upendo katika mioyo wazi. Kwa hiyo nawaomba, mitume wa upendo wangu: muwe na mioyo iliyo wazi sikuzote kurehemu na kusamehe. Wasameheni sikuzote wenzenu kama Mwanangu, kwa vile hivyo amani itakuwa ndani yenu. Wanangu, lindeni nafsi yenu, maana hiyo ndiyo ukweli wa pekee ulio wenu bila shaka. Mmeanza kusahau umuhimu wa familia. Familia haipaswi kuwa mahali pa mateso na maumivu, bali mahali pa uelewano na huruma. Familia wanaojaribu kuishi kama apendavyo Mwanangu, wanaishi wakipendana. Tangu alipokuwa angali mtoto, Mwanangu aliniambia ya kuwa watu wote kwake ni ndugu zake. Kwa hiyo kumbukeni, enyi mitume wa upendo wangu, watu wote mnaowaona ni kwenu familia yenu, ndugu kama apendavyo Mwanangu. Wanangu, msipoteze muda kufikiria na kuhangaikia mambo yajayo. Kitu chenu kimoja cha kuhangaikia kwenu kiwe vipi kuishi vema kila dakika kadiri ya Mwanangu, na tazama hiyo ndiyo ni amani! Wanangu, msisahau kabisa kuwaombea wachungaji wenu. Salini ili waweze kupokea watu wote kama wanao, ili, kama apendavyo Mwanangu, wawe kwao kama baba za kiroho. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, nikiwatazama hapa mmekusanyika kunizunguka, Mama yenu, ninaona nafsi safi nyingi. Ninawaona wanangu wengi wanaotafuta upendo na faraja lakini hakuna mtu anayewapa. Ninawaona hata wale wanaotenda mabaya maana hawana mifano myema, maana hawajamjua mwanangu. Mwanangu anawatuma ninyi kwangu, Mama, sawa kwa wote, niwafundisheni kupenda, ili muelewe ya kuwa ninyi ni ndugu. Ninatamani kuwasaidia. Mitume wa upendo wangu, kwa mwanangu yamtosha tamaa hai ya imani na upendo na atayakubali, lakini mnapaswa kustahili, kuwa na tamaa na mioyo wazi, Mwanangu huingia katika mioyo wazi. Mimi kama Mama ninatamani kwamba mjue Mwanangu katika kweli: Mungu aliyezaliwa na Mungu, kwamba mjue ukuu wa Upendo wake, ambao mnahitaji. Yeye amezichukua juu yake dhambi zenu, ameupata Ukombozi wenu, na badala yake anaomba mpendane ninyi kwa ninyi. Mwanangu ni upendo, Yeye anawapenda watu wote bila tofauti, watu wote wa nchi zote, wa mataifa yote. Ikiwa ninyi, wanangu, mngeishi upendo wa Mwanangu, ufalme wake ungekwisha kuwa duniani. Kwa hiyo, Mitume wa upendo wangu, salini, salini ili Mwanangu na upendo wake wawe ndani yenu nanyi muweze kuwa mfano wa upendo na muweze kuwasaidia wote wale ambao hawajamjua Mwanangu. Msisahau kamwe kwamba Mwanangu, mmoja na utatu, anawapendeni. Pendeni na wombeeni wachungaji wenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, Baba wa Mbinguni amenifanyia makuu, jinsi anavyowafanyia wale wote wanaompenda sana na kwa wema na uaminifu na wanaomtumikia kwa ibada. Wanangu, Baba wa Mbinguni anawapenda na kwa ajili ya upendo wake mimi nipo hapa pamoja nanyi. Ninasema nanyi: kwa nini hamtaki kuona ishara? Pamoja naye yote ni rahisi zaidi: hata mateso, tunayoishi pamoja naye, ni mepesi zaidi, maana kuna imani. Imani husaidia mateso, na maumivu pasipo imani huongoza katika kukata tamaa. Mateso tunayoyaishi na kuyatolea kwa Mungu, huinua mtu. Je, Mwanangu hakuukomboa ulimwengu kwa njia ya mateso yake makali? Mimi, kama mama yake, katika maumivu na mateso nilikaa pamoja naye, kama vile ninavyokaa pamoja nanyi. Wanangu, mimi nipo pamoja nanyi katika maisha: katika maumivu na mateso, katika furaha na upendo. Kwa hiyo muwe na matumaini: matumaini ndiyo yanayotuwezesha kuelewa ya kuwa hapa, kwenye mateso, ni uhai. Wanangu, mimi nasema nanyi; sauti yangu inasema na nafsi yenu, Moyo wangu unasema na moyo wenu: Enyi, mitume wa upendo wangu, Moyo wangu wa kimama jinsi gani unavyowapenda. Mambo haya nataka kuwafundisha. Jinsi gani Moyo wangu unataka muwe wakamilifu, lakini mtakuwa hivyo tu wakati nafsi, mwili na upendo yatakapoungana ndani yenu. Kama wanangu nawaombeni: salini sana kwa ajili ya Kanisa na kwa wahudumu wake, kwa wachungaji wenu, ili Kanisa liwe kama Mwanangu anavyolitaka: safi kama maji ya chemchemi na limejaa upendo. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, ninawaalika kupokea kwa unyofu wa moyo maneno yangu, ninayowaambieni kama Mama ili muende katika njia ya mwanga kamili, wa usafi, wa upendo wa pekee wa Mwanangu, mtu na Mungu. Raha, mwanga usioelezeka kwa maneno ya kibinadamu utaingia nafsini mwenu, na mtashikwa na amani na upendo wa Mwanangu. Ninataka hayo kwa wanangu wote. Kwa hiyo ninyi, mitume wa upendo wangu, ninyi mnaojua kupenda na kusamehe, ninyi msiohukumu, ninyi ambao mimi ninahimiza, muwe mfano kwa wale wote wasiokwenda katika njia ya mwanga na upendo au waliotengana nayo. Kwa njia ya maisha yenu waonyesheni ukweli, waonyesheni upendo, maana upendo hushinda matatizo yote, na wanangu wote wana kiu ya upendo. Ushirika wenu wa upendo ni zawadi kwa Mwanangu na kwangu. Lakini, wanangu, kumbukeni ya kuwa kupenda maana yake ni kupenda mwenzako na kutakia wongofu wa nafsi yake. Ninapowatazama mmekusanyika karibu nami, moyo wangu unahuzunika kwa sababu ninaona upendo haba wa kidugu, upendo wenye huruma. Wanangu, Ekaristi, Mwanangu hai katikati yenu, na maneno yake yatawasaidia kuelewa. Neno lake, kweli, ni uhai, Neno lake huburudisha nafsi, Neno lake huwajulisha upendo. Wanangu wapenzi, ninawaombeni tena, kama Mama apendaye wana wake: wapendeni wachungaji wenu, waombeeni… Nawashukuru!
Wanangu wapendwa, kwa upendo wa kimama ninawaalika kuifunua mioyo kwa imani, kuifunua mioyo kwa Mwanangu, ili katika mioyo yenu upendo kwa Mwanangu uimbe. Hakika, kutoka upendo huo tu, amani huingia nafsini. Wanangu, najua kwamba mna wema, najua kwamba mna upendo, upendo wenye rehema. Wanangu wangu wengi, lakini, wana moyo uliofungwa. Wanadhani kuweza kutenda pasipo kumwelekezea mawazo yao Baba wa mbinguni anayeangaza, pasipo kumwelekezea Mwanangu aliye daima pamoja nanyi katika Ekaristi na ataka kuwasikiliza. Wanangu, mbona hamzungumzi naye? Maisha ya kila mmoja wenu ni muhimu na ya thamani, maana ni zawadi ya Baba wa mbinguni kwa umilele. Kwa hiyo msisahau kamwe kumshukuru. Zungumzeni naye! Najua, enyi wanangu, ya kuwa mambo yatakayokuja hayajulikani kwenu lakini, mambo yenu ya mbele yatakapotokea, mtapata majibu yote. Upendo wangu wa kimama unataka muwe tayari. Wanangu, kwa maisha yenu wekeni katika mioyo ya watu mnaokutana hisia za amani, za mema, za upendo na msamaha. Kwa ajili ya sala, sikilizeni yanayowaambieni Mwanangu na tendeni namna hiyo. Ninawaalika tena kuwaombea wachungaji wenu, wale ambao Mwanangu aliwaita. Kumbukeni ya kuwa wanahitaji sala na upendo. Nawashukuru.
   




To compare Medjugorje messages with another language versions choose

For God to live in your hearts, you must love.

`